Shirika la kimkataifa la kutetea haki za binaadamu la 
Amnesty International limesema serikali ya Syria imewaua zaidi ya watu 
13,000 tangu kuanza kwa vuguvugu la mapinduzi ya umma mwaka wa 2011
 
Katika ripoti ya utafiti uliofanywa kati ya 2011 na 2015, Amnesty 
International imesema kati ya watu 20-50 walinyongwa kila wiki katika 
gereza la Saydnaya, mauaji yaliyoidhinishwa na maafisa wa ngazi za juu 
serikalini, wakiwemo wasaidizi wa Rais Bashar al Assad, na kufanywa na 
jeshi la polisi.
Ripoti hiyo iliyataja mauaji hayo kuwa ni 
"kampeni iliyopangwa ya mauaji ya kinyume cha sheria”. Naibu mkurugenzi 
wa utafiti wa ofisi ya kikanda ya Amnesty mjini Beirut Lynn Maalouf 
amesema shirika hilo limeorodhesha karibu mbinu 35 tofauti za mateso 
nchini Syria tangu mwishoni mwa miaka ya 80, vitendo ambavyo 
vimeongezeka tangu mwaka wa 2011. "Amnesty international inafichua 
kampeni ya mpangilio ya mauaji ya kinyume cha sheria kwa njia kuwanyonga
 watu wengi kila wiki, yanayofanywa Jumatatu na Jumatano. Kati ya watu 
20 na 50, hutolewa kwenye vyumba vyao, na kupelekwa katika jumba jingine
 mjini Sednaya na kunyongwa".
  
Mashirika
 mengine ya haki za binaadamu yamepata ushahidi wa mateso makubwa 
yaliyosababisha vifo katika magereza ya Syria: katika ripoti yake mwaka 
jana, Amnesty iligundua kuwa zaidi ya watu 17,000 waliuawa kwa kuteswa 
wakatiwa kizuizini kote Syria tangu mwaka wa 2011, ikiwa ni kiwango cha 
wastani cha zaidi ya watu 300 kwa mwezi. Takwimu hizo zinaweza 
kulinganishwa na vifo vilivyotokea katika viwanja vya mapambano vya 
Aleppo, mojawapo ya maeneo makali ya vita nchini Syria, ambako watu 
21,000 waliuawa kote mkoani humo tangu 2011. Maalouf anasema hakuna 
sababu ya kuamini kuwa dhuluma hizo zimekomeshwa tangu mwaka wa 2015, 
maana huenda maelfu ya watu wameuawa.
Ameongeza kuwa mauaji haya 
hufanyika baada ya kuendeshwa kesi ya uongo inayodumu dakika moja au 
mbili, lakini yanaidhinishwa na maafisa wakuu akiwemo Mufti mkuu, na 
waziri wa ulinzi. Maalouf ametoa wito wa kuchunguzwa madai hayo "Tunatoa
 mwito kwa Umoja wa Mataifa kuanzisha uchunguzi wa huru na wazi kuhusu 
kinachotokea Sednaya na kwa hili kufanyika katika njia ya mafanikio, 
tunaitaka serikali ya Syria kuwaruhusu waangalizi wake, waangalizi wa 
Umoja wa Mataifa ambao wako huru, kuingia Sednaya, lakini pia katika 
magereza yote na vituo vya kuwazuilia watu kote Syria".
Huwa 
nadra kwa maafisa wa serikali ya Syria kuzungumzia madai haya ya mateso 
na mauaji ya watu wengi. Katika siku za nyuma, walipinga ripoti za 
mauaji ya kikatili yaliyoorodheshwa na mashirika ya kimataifa ya haki za
 binaadamu, wakiritaja kuwa ni propaganda. Matokeo ya ripoti iliyotolewa
 leo yalitokana na mahojiano yaliyofanyiwa wafungwa wa zamani 31 na 
maafisa wengine 50 na watalaamu, wakiwemo walinzi wa zamani wa magereza 
na majaji.
No comments:
Post a Comment