Wednesday, June 13, 2018

MGOGORO WA KIDIPIOMASIA KATI YA KENYA NA UGANDA WANUKIA TENA

Mgogoro mwingine wa kidiplomasia kati ya Kenya na Uganda unanukia. Hii ni baada ya makumi ya wahamiaji haramu raia wa Uganda kukamatwa na maafisa wa polisi wa Kenya katika mpaka wa nchi mbili hizo.
Wambua Katiithi, Kamanda Mkuu wa Polisi katika mji wa Bumula, kaunti ya Busia amesema wahajiri haramu 53 wa Uganda wamekatwa wakiwa hawana vyeti vinavyohitajika vya usafiri, wakiwa njiani kuelekea mjini Nairobi kwa kutumia usafiri wa basi.
Tukio hilo lilifanyika hapo jana, ikiwa ni chini ya masaa 24 baada ya polisi ya Uganda kuwatia mbaroni askari polisi watatu wa Kenya na wavuvi kadhaa kati ya visiwa vya Mageta na Hama katika Ziwa Victoria.
Kenya na Uganda zimekuwa zikivutana kwa miaka kadhaa sasa kuhusu masuala kadha wa kadha na haswa umiliki wa kisiwa cha Migingo, kilichoko katika mpaka wa nchi mbili hizo za Afrika Mashariki.
Kisiwa cha Migingo kinachozozaniwa na Kenya na Uganda
Mwaka jana, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alisema kisiwa cha Migingo katika Ziwa Victoria ni milki ya Kenya.
Mgogoro wa kisiwa cha Migingo ulianza mwaka 2008 baada ya wanajeshi wa Uganda kukivamia na kuwatimua Wakenya ingawa kimekuwa kikitambuliwa kuwa ni milki ya Kenya.
Makubaliano ya awali kati ya Kenya na Uganda kuhusu kisiwa hiki yalifanyika 2016, na kwa sasa maafisa wa usalama kutoka nchi zote mbili wanalinda doria katika kisiwa hicho.

Tuesday, June 12, 2018

TRUMP NA KIM WATIA SAINI MAKUBALIANO YA KIHISTORIA

Rais wa Marekani Donald Trump na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un wamekubaliana kuondoa kabisa silaha za kinyuklia katika  rasi ya Korea katika makubaliano ya  pamoja  ya kihistoria.

     Singapore Summit Donald Trump Kim Jong Un Unterzeichnung (Reuters/J. Ernst)
Viongozi  hao  walikamilisha siku ya kihistoria ambayo ilishuhudia viongozi hao wawili wakikutana kwa  mara  ya  kwanza kabisa.
Katika  mkutano  huo Trump  ameahidi  kuipatia  Korea  kaskazini  uhakikisho  wa  usalama wake  pamoja  na  kutangaza  katika  mkutano  na  waandishi  habari baadaye  kwamba  Marekani  na  Korea  kusini  zitaacha  luteka  ya pamoja  ya  kijeshi kama Korea kaskazini  inavyodai.
Singapur Gipfel Kim Jong Un Donald Trump (Reuters/A. Wallace)
Kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un (kushoto) na rais wa Marekani Donald Trump wakipeana mikoni
Katika  waraka  wenye vipengee  vinne, Marekani  na  Korea kaskazini  zimeazimia  kuweka  uhusiano  mpya  kati  ya  nchi  hizo mbili, kujenga   utawala  imara  na  endelevu  kuelekea  amani akisisitiza  azimio  la  Panmunjeom  kutoka  Aprili  27.
Katika  mkutano  na  waandishi  habari leo rais  Donald Trump  wa Marekani  amesema  kwamba  jeshi  la  Marekani  litaacha  kufanya mazowezi  ya  pamoja  na  Korea  kusini  yakiilenga  Korea kaskazini, akisema  yanaongeza  hali  ya  wasi  wasi na  kuyasitisha kutasaidia  kuhifadhi  fedha  nyingi  zinazotumika  katika  mazowezi hayo. Pia  amesema  atamwalika  kiongozi  wa  Korea  kaskazini katika  ikulu  ya  marekani White house na  kwamba   binafsi angependa  kutembelea  mji mkuu  wa  Korea  kaskazini  Pyongyang.
Nchi  hizo  mbili  hufanya  mazowezi  ya  kijeshi  kila  mwaka  ambayo yanaikera  Korea  kaskazini , ambayo  imekuwa  kwa  muda  mrefu ikidai kusitishwa  kwa  mazowezi  hayo na  mara  nyingi  hujibu  kwa kuchukua  hatua  zake, na  kusababisha  kuongezeka  kwa  hali  ya wasi  wasi. 
Singapur - Präsident Donald Trump gemeinsam Unterschriebenes Dokument nach Treffen mit Kim Jong Un (Reuters/J. Ernst)
Rais Trump akionesha waraka uliotiwa saini baina yake na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un
Kim amshukuru  Trump
Wakati  wa  kutia  saini  makubaliano  hayo  kati  ya Trump  na  Kim leo  asubuhi, rais  Trump  alisema  pande  zote  mbili zimefurahi  kutia  saini  makubaliano  hayo.
"Tunatia  saini  waraka  muhimu  sana, waraka  ambao una maelezo mapana. na  tutajadili  hili  kwa  kina. Kwa  hivi  sasa naamini  mtapata nakala kwa  niaba  ya  mwenyekiti Kim  na mimi. Na wote tunafahari  kubwa  kutia  saini  waraka  huu. Asante."
Kwa  upande  wake  kiongozi  wa  Korea  kaskazini  Kim Jong Un alimshukuru  rais  Trump  kwa  kukubali  kufanyika  mkutano  huo.
"Leo tulikuwa  na  mkutano  wa  kihistoria  na  kuamua  kuacha nyuma  yaliyopita. Na  tuko  tayari  kutia  saini  waraka  huu  wa kihistoria. Dunia  itaona  mabadiliko  makubwa. Napenda kueleza  shukurani  zangu  kwa  rais Trump  kwa  kufanikisha mkutano  huu. Asante.
Kuhusu  vikwazo  dhidi  ya  Korea  kaskazini  rais  Trump  amesema kwa  hivi  sasa  vikwazo  hivyo  vitaendelea , lakini  anaangalia uwezekano  wa  kuviondoa.
Donald Trump Pressekonferenz Singapur (Reuters/J. Ernst)
Rais Trump akiwa katika mkutano na waandishi habari baada ya kutia saini makubaliano na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un
Rais  wa  Marekani  amesema  pia  kwamba  kiongozi  wa  Korea kaskazini  Kim Jong Un ana  nia  thabiti  ya  kuharibu  kabisa maeneo  ambayo  nchi  hiyo  inafanyia  majaribio  silaha  zake.
Kwa  upande  mwingine waziri  mkuu  wa  Japan  Shinzo  Abe  na mwenzake  wa  Malaysia  mahathir Mohammed wamekubaliana  leo kufanyakazi  kwa  pamoja  kupambana  na  mipango  ya  kinyuklia  na makombora  ya  Korea  kaskazini. Viongozi  hao  wamesema wanataka  kutuma  ujumbe  mkali  kwa  Korea  kaskazini  kuhusu suala  hilo.  Waliysema  hayo  katika  mkutano  na  waandishi  habari kufuatia  mkutano  wao  mjini  Tokyo

MAGAZETI YA UJERUMANI YAMKOSOA TRUMP, YAMWITA "MPUMBAVU"

Magazeti ya Ujerumani yamemtaja Rais Donald Trump wa Marekani kuwa ni mtu asiyejua mipaka yake wala asiye na mantiki na yamezitaka nchi zote za Ulaya kuacha kumfuata kiongozi huyo.
Gazeti la Ujerumani la Süddeutsche Zeitung limeripoti kuwa, kila mtu aliyekuwa anaamini kuwa Rais wa Marekani ni mtu mwenye mantiki na anayetilia maanani uhakika wa mambo anapaswa kuzika matumaini hayo kwa sababu kuwepo kwa mtu huyo asiye na adabu na mbumbavu hakuifanyi dunia kuwa sehemu bora na yenye amani zaidi.
Gazeti hilo la Ujerumani limeongeza kuwa: Trump anaendelea kuzitishia nchi nyingine kwa kutumia mabavu na silaha ya uchumi, na suala hilo ni hatari sana kwa Ujerumani.
Trump na Macron
Süddeutsche Zeitung limeandika kuwa: Nchi za Magharibi zimekumbwa na mgawanyiko katika masuala ya kisiasa na uhakika huo umeonekana waziwazi katika mkutano wa viongozi wa nchi 7 zilizopiga hatua kiviwanda wa G7 huko Canada ambao kimsingi ulibadilika na kuwa G6. 
Rais Donald Trump wa Marekani siku chache zilizopita aliwaacha bumbuazi viongozi wengine wa G7 katika mkutano wa Canada baada ya kuondoka ghafla katika mkutano huo na kufuta saini yake katika hati ya mwisho ya mkutano huo. 

WITO WA MSHIKAMANO WA NCHI ZA ULAYA KATIKA KUKUBALIANA NA MAREKANI

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amebainisha masiktiko yake baada ya Rais Donald Trump wa Marekani kukataa kuidhinisha taarifa ya mwisho ya kikao cha viongozi wa nchi tajiri kiviwanda G7 ambacho kilimalizika juzi huko Quebec, nchini Canada. Merkel amebainisha wazi kuwa nchi za Ulaya hazipaswi kuitegemea tena Marekani.
Naye Heiko Maas Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani amesisitiza kuwa, jibu la  Ulaya kuhusu uamuzi huo wa Trump linapaswa kuwa ni mshikamano na ukuruba zaidi katika Umoja wa Ulaya.
Mass ameongeza kuwa uamuzi wa Trump wa kutoafiki taarifa ya mwisho ya kikao cha G7 haukuzishangaza sana nchi shiriki kwani Trump amekiuka mapatano mengine muhimu ya utunzaji mazingira  na mapatano ya nyuklia ya Iran.
Baada ya mkutano wa viongozi wa kundi la G7, kumedhihirika hitilafu kubwa na za wazi baina ya Rais Trump na viongozi wa Canada, Ufaransa na Ujerumani. Trump aliondoka mapema kabla ya kikao hicho kumalizika kama ishara ya kubainisha kuchukizwa kwake na tamko la Waziri Mkuu wa Canada Justin Trudeau na kusema hataunga mkono taarifa ya mwisho ya kikao hicho. Uamuzi huo wa Trump umetajwa kuwa ni pigo kubwa kwa kundi la G7 ambalo linajumuisha  Marekani, Canada, Ujerumani, Uingereza,Ufaransa, Italia na Japan.

Trump amejiondoa katika mapatano ya kulinda mazingira duniani ya Paris 

Hatua hiyo ya Trump itatoa pigo kubwa kwa ushirikiano wa pande mbili za Bahari ya Atlantiki na pia ni pigo kubwa kwa uhusiano wa kistratijia wa Canadan na Marekani. Kwa hatua yake hiyo, Trump analenga kung'oa mizizi ya uhusiano na mshikamano wa miongo kadhaa wa kiuchumi, kibiashara, na kiusalama baina ya Marekani na Ulaya. Wakuu wa Ulaya wanajaribu kuzuia hali ya mambo kuwa mbaya zaidi na wanasema hatua ya Trump kutosaini taarifa ya mwisho haimaanishi kila kitu kimekwisha. Kuhusiana na hili, Angela Merkel amesema: "Hatua ya Trump kutangaza kuwa hatatia saini taarifa ya mwisho ya G7 kupitia Twitter ni jambo la kusikitisha. Ameongeza kuwa, 'kikao cha viongozi wa G7 huko Canada hakikuwa mwisho wa ushirikiano wa Ulaya na Marekani lakini akaongeza kuwa, nchi za Ulaya hazipaswi kuitegemea tena Marekani na zinapaswa zenyewe zijiamulie  hatima yao.'
Ingawa suala la Marekani kujiondoa G7 halijapewa uzito mkubwa lakini kwa kuzingatia utendaji kazi wa Trump katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu wa urais wake, nchi zingine sita za kundi la G7 hazitashangaa iwapo Trump ataendeleza mwenendo wake huo wa kupuuza na kubatilisha mikataba ya kimataifa, na hivyo aamue kujiondoa katika kundi hilo. Kwa hivyo nchi hizo sita zinajitayarisha kwa hali kama hiyo.
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa anasema hivi kuhusu suala hilo:"Pengine Trump hajali iwapo atatengwa lakini hata tukibadilika na kuwa kundi la  G6 bado tutakuwa nguvu kubwa. Iwapo Trump ataamua kuiondoa Marekani katika nafasi yake duniani, jambo hilo litakuwa na matokeo hasi kwa uchumi na hadhi ya Marekani duniani. Trump anafahamu hili."

Trump amejiondoa katika maptano ya nyuklia ya Iran maarufu kama JCPOA

Mtazamo wa Trump kuhusu masuala ambayo yamepelekea kuibuka hitilafu baina ya Marekani na Ulaya ni jimbo linaloonyesha kuwa hana nia ya kulegeza msimamo wake bali hata ametoa vitisho kwa kwa nchi za Ulaya na Canada hasa katika masuala ya kibiashara. Trump ameongeza kwa kiwango kikubwa ushuru wa bidhaa zinazoingizwa Marekani kutoka Ulaya, Canada na Mexico hasa bidhaa za chuma.
Hatua hizo za Trump zimepelekea kuongezeka hitilafu kubwa baina ya Marekani na nchi hizo na kuwepo hatari ya kuibuka vita vya kibiashara kati ya Marekani na nchi hizo. Hali kadhalika nchi za Ulaya pia zimekasirishwa na hatua ya Trump ya kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya Iran maarufu kama JCPOA na mapatano mengine muhimu ya mazingira maarufu kama Mapatano ya Tabianchi ya Paris.
Kwa mtazamo wa nchi muhimu katika Umoja wa Ulaya, si tu kuwa sera za Trump zitaidhuru dunia bali zitapelekea kutengwa zaidi Marekani katika uga wa kimataifa.

Sunday, May 27, 2018

WATU 30 WAUAWA KATIKA MAPIGANO MASHARIKI MWA KONGO DR

Watu 30 wameuawa katika mapigano kati ya jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na wanamgambo wa Mai-Mai mashariki mwa nchi hiyo.
Duru za eneo hilo zimeripoti kuwa katika mapigano hayo yaliyotokea jana na kuendelea kwa saa kadhaa wanajeshi 18 waliuawa akiwemo afisa mmoja na kamanda wa polisi wa polisi wa eneo hilo.
Kwa mujibu wa duru hizo, wanamgambo wanane waliohusika katika hujuma hiyo pamoja na raia watatu pia waliuawa katika mapigano hayo. Raia hao waliuliwa kwa risasi walipokuwa wakikimbia mapigano.


Mnamo siku ya Alkhamisi iliyopita, wanamgambo wa kundi la Mai-Mai walilidhibiti eneo lenye utajiri wa madini la Salamambila mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, lakini wakalazimika kuliacha na kukimbia baada ya vikosi vya jeshi la serikali kufika katika eneo hilo.
Wanamgambo wa Mai-Mai wanatokana na makundi ya wabeba silaha waliopata mafunzo ya kijeshi katika eneo la mashariki mwa Kongo DR ambalo limekuwa uwanja wa mapigano kwa zaidi ya miaka 20 sasa.../

RAIS ROUHSNI: HATUA ZILIZOCHUKULIWA HADI SASA NI CHANYA KWA AJILI YA KUENDELEZA JCPOA

Rais Hassan Rouhani amesema, baada ya Marekani kujitoa kwenye makubaliano ya JCPOA waliowengi katika jamii ya kimataifa wameipa haki Iran na kuyatetea makubaliano hayo na kuongeza kwamba hatua zilizochukuliwa hadi sasa ni nzuri kwa ajili ya kuendeleza makubaliano hayo ya nyuklia.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyaeleza hayo mbele ya hadhara ya maulamaa na wanazuoni wa mjini Tehran na kubainisha kuwa: Leo akthari ya nchi zinaitakidi kuwa njia iliyofuata Iran ilikuwa sahihi na Marekani ndio iliyofanya makosa, na hayo ni mafanikio makubwa.
Rais Rouhani amefafanua kuwa Marekani inatoa mashinikizo kwa nchi za Ulaya kwamba zichague kati ya Marekani na Iran lakini nchi hizo zinasema 'sisi tunachagua makubaliano ya JCPOA'.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa msingi inaofungamana nao Iran ni kwamba kama itaweza kupata haki zake kwa kubaki kwenye makubaliano ya JCPOA itaendelea kufungamana na makubaliano hayo ya kimataifa.
Rais Hassan akihutubia hadhara ya maulamaa
Ikumbukwe kuwa, Rais Donald Trump wa Marekani alitangaza Mei 8 kuwa nchi yake imejiondoa katika mapatano hayo ya nyuklia ya Iran ambayo rasmi yanajulikana kama JCPOA. Trump aidha alisema ataiwekea Jamhuri ya Kiislamu vikwazo vya nyuklia katika kipindi cha miezi mitatu hadi sita ijayo.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza kusikitishwa mno na uamuzi huo wa upande mmoja uliochukuliwa na rais wa Marekani.
Hii ni katika hali ambayo nchi zilizosalia katika JCPOA, yaani Uingereza, Ufaransa, Russia, China, Ujerumani na Umoja wa Ulaya, zimesisitiza kuwa zitandelea kuunga mkono mapatano hayo.
Wakati huohuo katika siku za karibuni Iran na nchi za Ulaya zimefanya mazungumzo kadhaa kwa lengo la kuyaendeleza makubaliano ya JCPOA baada ya Washington kujiondoa kwenye makubaliano hayo ya kimataifa.
Inafaa kukumbusha pia kuwa mnamo siku ya Jumatano iliyopita Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Khamenei alibainisha masharti ya Iran kuendelea kubakia katika JCPOA na kusisitiza kuwa: "Nchi za Ulaya zinapaswa kuwasilisha azimio dhidi ya Marekani katika Baraza la Usalama, ziahidi pia kuwa kadhia za makombora na ushawishi wa Iran katika eneo hazitajadiliwa na pia zikabiliane na vikwazo vyovyote vya Marekani dhidi ya Iran." Aidha Kiongozi Muadhamu aliongeza kuwa nchi za Ulaya zinapaswa kutoa dhamana ya kununua mafuta ya Iran kwa kiwango ambacho Iran inahitaji na pia benki za Ulaya zinapaswa kutoa dhamana ya kutekeleza malipo ya kifedha kwa ajili ya biashara na serikali pamoja na sekta binafsi ya  Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.../

BAYTU ZAKAT YA KUWAIT YAZINDUA PROGRAMU YA DOLA 26400 KWA AJILI YA KUFUTURISHA KATIKA MWEZI WA RAMADHAN NCHINI TANZANIA


 Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Mhe. Jasem Al-Najem anashiriki katika utekelezaji wa programu ya kufuturisha ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan ambayo inafadhiliwa na Chombo cha Baytu Zakat, Wakfu na Mali ya Amana ya Kuwait. Programu kama hii huandaliwa kila mwaka kutoka kwa wasamaria wa nchi ya Kuwait.  
Programu hii thamani yake ni dola elfu 26 na mia nne sawa na shilingi milioni 60.
Awamu ya kwanza ya programu hii ilikuwa ni kugawa vikapu 400 vyenye vyakula kama mchele, sukari,unga,mafuta ya kula, tende na sukari ambapo katika moja ya zoezi la ugawaji alihudhuria Mkuu wa Wilaya ya Ilala. Bi Sophia Mjema.
Ubalozi wa Kuwait umedhamiria mwaka huu kuwasilisha misaada ya futari katika miji, vitongoji, kata, mitaa, vijiji na maeneo ya mbali kote Tanzania ambapo hadi sasa mikoa ya Tanga, Iringa, Dar es salaam na visiwa vya Zanzibar imefaidika na misaada hiyo ambayo Ubalozi hushirikiana na asasi zisizokuwa za kiserikali za Tanzania katika kuwafikia walengwa.