Sunday, July 30, 2017

KIONGOZI: HIJA NI FURSA YA KUTANGAZA MSIMAMO KUHUSU MSIKITI WA AL-AQSA NA UWEPO WENYE MALENGO MAOVU WA MAREKANI KATIKA ENEO

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema Hija ni fursa bora ya mahali na wakati kwa Umma wa Kiislamu kutangaza misimamo kuhusu kadhia ya Palestina, msikiti wa Al-Aqsa na uwepo wenye malengo maovu wa Marekani katika eneo la Mashariki ya Kati.
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo katika mkutano na viongozi na watendaji wa masuala ya Hija na kuongeza kuwa, Hija ni fursa ya kutangaza misimamo kuhusu maudhui zinazokubaliwa na Umma wa Kiislamu. Amefafanua kwa kusema: Moja ya maudhui hizo ni kadhia ya msikiti wa Al-Aqsa na Quds ambayo inazungumziwa na kupewa uzito zaidi wakati huu kutokana na jeuri, utovu wa haya na ukhabithi wa utawala ghasibu na bandia wa Kizayuni.
Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa haifai kwa namna yoyote ile kughafilika na suala la Palestina ambalo ni mhimili mkuu wa masuala ya Ulimwengu wa Kiislamu na akaongezea kwa kusema: Kuna mahali gani bora zaidi kuliko Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu, Makka, Madina, Arafat, Mash'ar na Mina kwa mataifa ya Waislamu kudhihirisha mitazamo yao na kubainisha misimamo yao kuhusu Palestina na msikiti wa Al-Aqsa.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, uwepo wenye malengo maovu wa Marekani katika nchi za Kiislamu na eneo kwa ujumla na kuanzisha makundi ya kigaidi na kitakfiri, ni maudhui nyengine muhimu  ambayo mataifa ya Waislamu yanapaswa kutangaza msimamo wao juu yake katika Hija. Ameongeza kuwa: Utawala wenyewe wa Marekani ni shari kubwa zaidi na khabithi zaidi kuliko hata makundi ya kigaidi uliyoyaanzisha. 
Viongozi na wasimamizi wa ibada ya Hija wakisikiliza hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
Katika sehemu nyengine ya hotuba yake, Ayatullah Khamenei ameeleza kuwa maudhui ya umoja ni jambo jengine muhimu zaidi na la dharura kwa mataifa ya Waislamu, na akafafanua kwa kusema: Wakati mabilioni ya dola zinatumika kuzusha mifarakano, hitilafu na uadui baina ya Waislamu, Waislamu wenyewe wanapaswa wajihadhari na kufanya mambo yatakayosaidia uzushaji huo wa hitilafu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa: Takwa muhimu zaidi na la kila mara la Jamhuri ya Kiislamu ni kudhaminiwa usalama, izza na huduma bora kwa mahujaji wote hususan wa Kiirani; na kudhamini usalama wa Hija ni jukumu la nchi yenye mamlaka ya Haram Mbili Tukufu.../

MAKUMI WAUAWA NA KUJERUHIWA KATIKA MRIPUKO WA MOMU MOGADISHU, SOMALIA

Watu sita wameuawa na wengine zaidi ya 20 wamejeruhiwa baada ya bomu lililokuwa limetegwa ndani ya gari kuripuka katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.
Meja Mohamed Hussein, afisa mwandamizi wa polisi nchini humo ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa bomu hilo limeripuka katika barabara yenye shughuli nyingi ya Makatul Mukaramah.
Amesema aghalabu ya wahanga wa hujuma hiyo inayoaminika kufanywa na kundi la kigaidi la al-Shabaab, ni wapita njia na watu waliokuwa ndani ya maduka yaliyoko kandokando ya barabara hiyo.
Afisa huyo wa polisi ya Somalia ameongeza kuwa, yumkini idadi ya vifo ikaongezeka, kutokana na majeraha mabaya waliyopata baadhi ya wahanga wa shambulizi hilo. 
Askari wa AMISOM
Wakati huohuo, makabiliano makali kati ya askari wa Kikosi cha Kusimamia Amani cha Umoja wa Afrika nchini Somalia AMISOM na wanamgambo wa kundi la kigaidi na kitakfiri la al-Shabaab yameripotiwa katika wilaya ya Bulamareer, eneo la Shabelle ya Chini, yapata kilomita 140 kusini magharibi mwa mji mkuu Mogadishu.
Hakuna taarifa rasmi iliyotolewa na AMISOM au jeshi la Somalia kuhusu idadi ya wahanga wa mapigano hayo, ingawaje genge la al-Shabaab linadai kuwa limeua makumi ya askari wa Umoja wa Afrika.
AbdiAziz Abu Musab, msemaji wa operesheni za kijeshi za al-Shabaab amedai kuwa, kundi hilo la kigaidi limeua wanajeshi 39 wa AMISOM akiwemo kamanda wao.

Friday, July 28, 2017

MAREKANI YARUSHA KOMBORA KUIJIBU KOREA KASKAZINI

Korea Kusini na Marekani wamefanya zoezi la pamoja la kurusha makombora ya ardhini baada ya Korea Kaskazini kufanya jaribio jingine la kombora. Afisa wa Ulinzi wa Marekani alithibitisha kufanyika kwa zoezi hilo la kulipiza kisasi bila ya kutoa taarifa zaidi. Korea Kaskazini ilirusha kombora la masafa marefu linaloweza kuruka kutoka bara moja hadi jingine hapo jana, ambalo wataalamu wanasema lina uwezo wa kufikia miji kadhaa ya Marekani. Wizara ya Ulinzi ya Marekani Pentagon imesema kombora hilo la Korea Kusini liliruka umbali wa kilomita 1,000 kabla ya kuanguka katika Bahari ya Japan. Rais wa Marekani Donald Trump amelilaani jaribio hilo la pili la Korea Kaskazini la kombora la kuruka kutoka bara moja hadi jingine na kulitaja kuwa ni kitisho kwa ulimwengu.

TRUMP AMTEUA KELLY KUWA MKUU WA UTUMISHI WA SERIKLI

Rais wa Marekani Donald Trump amemteua Waziri wa Usalama wa Ndani John Kelly kuwa mkuu wa utumishi wa serikali baada ya kumwachisha kazi Reince Priebus aliyehudumu katika wadhifa huo kwa miezi sita

Kombobild Reince Priebus und John Kelly (Reuters/J. Roberts)
Baada ya miezi kadhaa ya uvumi kuhusu hatima ya Priebus, Trump alitangaza uamuzi wake kwenye mtandao wa Twitter wakati aliwasili mjini Washington baada ya kutoa hotuba jijini New York ambayo aliitumia kummwagia sifa Kelly kwa kazi anayofanya katika wizara ya Usalama wa Ndani.
Alisema "nna furaha kuwafahamisheni kuwa nimemteua Jenerali/Waziri John F Kelly kuwa Mkuu wa Utumishi wa serikali katika Ikulu ya White House".
Wakati ujumbe huo ulianza kusambaa mjini Washington, Priebus aliondoka katika ndege ya rais Air Force One wakati mvua kubwa ikinyesha na akaingia kwenye gari pamoja na maafisa waandamizi wa Ikulu ya White House Steven Miller na Dan Scavino.
Muda mfupi baadaye, Miller na Scavino walitoka nje ya gari hilo na kuingia kwenye gari jingine. Gari lililombeba Priebus kisha likaondoka pamoja na msafara wa rais.
Priebus, kiongozi wa zamani wa Kamati ya Kitaifa ya chama cha Republican, amekuwa akilengwa na uvumi wa mara kwa mara kuhusu usalama wa kazi yake wakati kukiwa na malumbano ya kindani na sintofahamu ndani ya Ikulu ya White House.
Trump ermuntert Polizisten zu mehr Gewalt (Reuters/J. Ernst)
Trump amewafuta kazi maafisa waandamizi wanane tangu alipoingia madarakani
Mnamo siku ya Alhamisi, alishambuliwa hadharani na mkurugenzi mkuu mpya wa mawasiliano katika Ikulu ya White House aliyeteuliwa na Trump, Anthony Scaramucci ambaye alimtuhumu Prebius kwa kutoa habari za kumharibia jina kwa vyombo vya habari.
Priebus alisema aliwasilisha ombi la kujiuzulu kwake siku ya Alhamisi na kuwa rais alikubali ijapokuwa wale walio karibu na rais huyo walisema kutimuliwa kwake kumekuwa kukishughulikiwa kwa wiki kadhaa sasa.
"nadhani rais alitaka kwenda mkondo tofauti," Priebus aliiambia televisheni ya CNN saa chache tu baada ya kutangazwa kutimuliwa kwake. Aliongeza kuwa anakubali kwamba Ikulu ya White House huenda ikanufaika na hatua ya kufanyiwa marekebisho na akasema "mimi daima ntakuwa shabiki wa Trump. Niko kwenye Team Trump."
Kelly ataapishwa rasmi kuchukua wadhifa huo siku ya Jumatatu. Wizara yake ya Usalama wa Ndani inahusika na kuweka usalama mipakani na amechukua msimamo mkali kuhusu wahamiaji walioko ndani ya Marekani.
Tangu alipoingia katika Ikulu ya White House miezi sita iliyopita, Trump amewaachisha kazi mshauri wake wa usalama wa taifa, naibu mshauri wa usalama wa taifa, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Upelelezi la Marekani – FBI, msemaji wa ikulu, mkurugenzi wa mawasiliano, naibu mwaneshiria mkuu, naibu mkuu wa utumishi wa serikali na sasa mkuu wa utumishi wa serikali, mabadiliko ya viongozi wakuu ambayo hayajawahi kushuhudiwa katika historia ya kisiasa nchini Marekani.

MAREKANI YAIWEKEA TENA VIKWAZO IRAN

Marekani imeendeleza uadui wake dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa kuziwekea vikwazo taasisi 6 za Kiirani.
Wizara ya Fedha ya Marekani usiku wa kuamkia leo imeziwekea vikwazo taasisi hizo sita za Kiirani kwa kisingizio cha majaribio yaliyofanywa juzi na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ya roketi la kutuma satalaiti angani la Simorgh ambayo inahusiana kikamilifu na masuala ya kielimu na kisayansi.
Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Fedha ya Marekani imesema kuwa: Mali na milki za taasisi hizo sita za Iran katika ardhi ya Marekani zinazuiliwa, na taasisi za fedha za kigeni zinazuiwa kufanya muamala wowote na taasisi hizo.
Roketi la kubeba satalaiti angani la Simorgh lilizinduliwa Alkhamisi iliyopita kwa mafanikio katika Kituo cha Masuala ya Anga cha Imam Khomeini. Roketi hilo lina uwezo wa kupeleka angani satalaiti yenye uzito wa kilo 250 umbali wa kilomita 500 kutoka ardhini. 
Uzinduzi wa roketi la Simorgh, Iran
Siku chache zilizopita pia Kongresi ya Marekani ilipasisha mpango wa vikwazo vipya dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Vilevile tarehe 18 mwezi huu wa Julai Wizara ya Fedha ya Marekani iliwawekea vikwazo watu na taasisi 18 za Iran na nchi za kigeni kwa kutumia visingizio mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwa na uhusiano na miradi ya kutengeneza makombora ya Iran. 
Tangu iliposhika madaraka nchini Marekani, Serikali ya Donald Trump imezidisha uhasama na uadui dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.  

Friday, July 21, 2017

AL AZHAR YAONYA KUHUSU KUENDELEA ISRAEL KUUVUNJIA HESHIMA MSIKITI WA AL AQSA

  • Askari wa Israel hawawahurumii hata akinamama wanaokwenda kusali Masjidul Aqswa
Chuo Kikuu cha al Azhar cha nchini Miri kimeuonya utawala wa Kizayuni wa Israel kutokana na jinai unazozifanya pambizoni mwa Msikiti wa al Aqsa kwani jinai hizo zinawaumiza Waislamu wote duniani.
Chuo Kikuu cha al Azhar cha nchini Misri kilitoa tamko hilo jana Ijumaa huku taifa madhlumu la Palestina likiendelea kusimama kidete kukihami Kibla cha Kwanza cha Waislamu.
Wanajeshi wa Israel wakiwapiga risasi waandamanaji wa Palestina.
Katika tamko lake hilo al Azhar imeutaka ulimwengu wa Kiarabu na Kiislamu na taasisi za kieneo na kimataifa kuchukua hatua za haraka za kuuokoa Msikiti wa al Aqsa mbele ya jinai za utawala wa Kizayuni.
Tamko la chuo kikuu hicho cha Kiislamu cha nchini Misri limeongeza kuwa, al Azhar inalaani kwa nguvu zake zote uchochezi wote unaofanywa na utawala wa Kizayuni dhidi ya Waislamu wa Palestina waliokuwa wanasali na vile vile vitendo vya kikatili na kinyama vya Wazayuni ambavyo vimepelekea kujeruhiwa makumi ya Waislamu wa Palestina akiwemo khatibu wa Masjidul Aqswa, Sheikh Ekrima Sa'id Sabri.
Baada ya vijana watatu wa Kipalestina kufanya operesheni ya kujitolea kufa shahidi dhidi ya Wazayuni katika mji wa Quds siku ya Ijumaa ya tarehe 14 Julai, utawala wa Kizayuni wa Israel uliufunga msikiti huo na kuwazuia Waislamu kuingia msikitini humo kwa muda wa siku mbili.
Vijana wa Palestina wakikabiliana na wanajeshi wa Israel waliojizatiti kwa silaha nzito. Licha ya kuwa mikono mitupu, Wapalestina wameapa kusimama imara kukilinda Kibla cha Kwanza cha Waislamu

Siku ya Jumapili, wanajeshi wa Israel walifungua milango ya msikiti huo lakini kwa masharti magumu ambayo Waislamu wa Palestina wameyapinga na kwa mara ya kwanza, jana Ijumaa, Wazayuni walizuia kusaliwa Sala ya Ijumaa ndani ya msikiti huo mtakatifu. Waislamu walimiminika katika maeneo ya karibu na msikiti huo kutekeleza ibada ya Sala ya Ijumaa, lakini hata hivyo hawakusalimika na ukatili wa Wazayuni.
Viongozi wengi wa nchi za Kiislamu na kimataifa wamelaani jinai hizo za Wazayuni na kuilaumu Israel kwa kutekeleza njama zake za muda mrefu dhidi ya Kibla cha Kwanza cha Waislamu kwa kutumia kisingizio cha opereseheni ya kujitolea kufa shahidi vijana hao watatu wa Palestina. 

Thursday, July 6, 2017

MAGENDO YA MIHADARATIM TATIZO LISILO NA UFUMBUZI

Ongezeko la uzalishaji wa mihadarati na magendo ya madawa ya kulevya linaonekana kuitia wasi wasi dunia nzima, hata hivyo kile kinachopelekea ongezeko hilo na kulifanya jambo hilo kuwa tatizo lisilo na mwisho, ndicho chenye kutia wasi wasi zaidi.
Suala hilo ndilo lilikuwa nukta kuu iliyojadiliwa katika kongamano lililofanyika siku ya Jumanne ya tarehe 4 Julai mwaka huu hapa mjini Tehran, kwa mnasaba wa siku ya kimataifa ya kupambana na madawa ya kulevya. Katika kongamano hilo, Ali Larijani, Spika wa Majlis ya Ushauri ya Kiislamu yaani bunge la Iran, alisema: "Magendo ya madawa ya kulevya yameangamiza maisha ya watu wengi, na kusababisha matatizo makubwa kifamilia na kijamii. Alisema: Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inafanya juhudi kubwa za kupambana na tatizo hilo, hivyo nchi nyingine nazo zinatakiwa ziwe na fikra moja kuhusiana na suala hilo. Kwani si sahihi gharama zote za kupambana na madawa ya kulevya zibebwe na Tehran peke yake." Mwisho wa kunukuu.
Askari wa Marekani katika moja ya mashamba ya mipopi inayozalisha mihadarati nchini Afghanistan
Hivi sasa na kwa mujibu wa makadirio ya dunia, ugaidi na uzalishaji madawa ya kulevya, ni mambo mawili yanayohesabiwa kuwa hatari kubwa kwa usalama wa taifa kieneo na kimataifa. Afghanistan ambayo ina mpaka mkubwa na Iran inahesabika kuwa chimbuko la uzalishaji wa madawa ya kulevya. Imepita miaka 16 sasa tangu Wamarekani walipoivamia nchi hiyo hapo mwaka 2001 kwa madai ya kile walichokisema kuwa ni kupambana na madawa ya kulevya na ugaidi. Katika kipindi chote hicho, askari wa Muungano wa Kijeshi wa Nchi za Magharibi (NATO) na hasa hasa askari wa Uingereza, ambayo ina jukumu la kupambana na madawa ya kulevya nchini Afghanistan, hawajaweza kufikia mafanikio yoyote yale, kama ambavyo pia hawajapata maendeleo yoyote hata katika uga wa kupambana na ugaidi na harakati za makundi yenye misimamo ya kuchupa mipaka nchini humo.
Askari wa nchi za Asia wakiwa katika kiwanda cha kutengeneza madawa ya kulevya
Suala la kutia wasi wasi mkubwa katika uwanja huo ni kwamba, magendo ya madawa ya kulevya yamegeuka kuwa sehemu ya chanzo cha kifedha cha makundi ya kigaidi, fedha ambazo baadaye hutumiwa kuathiri usalama wa nchi za eneo hili zima na duniani kiujumla. Andrei Kazantsev, mchambuzi wa masuala ya kimataifa wa nchini Russia anasema: "Hali ya Afghanistan imekuwa na taathira kubwa kwa usalama wa nchi za Asia ya Kati. Kwa ujumla ni kwamba kadri inavyoendelea kuwa tishio kwa usalama wa eneo hilo, ndivyo pia huathiri usalama wa Russia." Mwisho wa kunukuu. Katika hilo kunaibuka swali kwamba, hivi juhudi nchi kadhaa za eneo ikiwemo Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kupambana na madawa ya kulevya, zinaweza kuwa na taathira inayotakiwa? Na je, ni kweli nchi zinazounga mkono ugaidi zina azma ya dhati ya kupambana na madawa ya kulevya. Ukweli wa kushtusha ni huu kwamba, hadi sasa takwimu zinaonyesha kwamba, watu milioni 10 wanajishughulisha na magendo ya madawa ya kulevya duniani, ambapo pesa zinazotokana na biashara hiyo zinafikia kiasi cha Dola Bilioni 1500 kwa mwaka.
Raia wa Afghanistan akiendelea kuhudumia shamba la madawa ya kulevya
Kwa mujibu wa ripoti zilizotolewa, mwaka jana 2016 uzalishaji wa madawa ya kulevya nchini Afghanistan ulifikia tani 5600, ambapo karibu asilimia 35 ya madawa hayo yalivushwa na wafanya magendo hao kupitia mipaka ya Iran kwenda nchi nyingine. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikiwa katika mstari wa mbele wa kupambana na madawa ya kulevya duniani, imeshapoteza zaidi ya askari 3500 waliouawa shahidi na zaidi ya wengine elfu 10 kujeruhiwa katika mapambano na wafanya magendo ya madawa hayo ya kulevya. Katika kongamano jingine la kimataifa la kupambana na madawa ya kulevya lililofanyika mwaka huu mjini Tehran, Salamat Azimi, Waziri wa Kupambana na Madawa ya Kulevya wa Afghanistan sambamba na kuipongeza sana Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kutokana na juhudi zake kubwa za kukabiliana na janga hilo, alisema: "Tunataraji kuziona nchi majirani na Afghanistan zitatekeleza ahadi zao za kufunga mipaka yao na kupambana na wafanya magendo ya madawa ya kulevya kama inavyofanya Iran ya Kiislamu." Mwisho wa kunukuu.
Mamilioni ya Dola za madawa ya kulevya yaliyonaswa
Inafaa kuashiria kuwa, uzalishaji wa madawa ya kuvya nchini Afghanistan ni tishio ambalo si tu linahatarisha usalama wa eneo hili, bali ni hatari kubwa kwa usalama wa ulimwengu mzima. Na katika kudhamini usalama wa dunia kutokana na uzalishaji wa hatari hiyo nchini Afghanistan, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imepoteza nguvukazi nyingi kama alivyosema Spika wa Majlis ya Ushauri kwamba: "Hakuna irada ya kimataifa na ya kivitendo vya kupambana na mihadarati. Hivyo isitarajiwe kuwa Iran itakuwa tayari kugharamika peke yake katika mapambano ya madawa ya kulevya."

WATU 80 WAPOTEZA MAISHA KATIKA AJALI YA BARABARANIJAMHURI YA AFRIKA YA KATI

Ajali ya lori moja la mizigo huko Jamhuri ya Afrika ya Kati CAR imesababisha vifo vya zaidi ya watu 80, wengi wao wakiwa ni wachuuzi waliokuwa wakielekea sokoni mjini Bambari.
Duru za madaktari zinasema kuwa, lori hilo lilipata ajali likiwa limepakia watu na mizigo kupita kiasi na kwamba, ajali hiyo imetokea yapata kilomita 10 hivi nje ya mji wa Bambari.
Wafanyabiashara hao wakiwa na bidhaa zao za biashara walikuwa wakielekea katika soko moja la kila wiki katika kijiji cha Maloum. Taarifa zaidi zinasema kuwa, zaidi ya watu 80 wameaga dunia kufuatia ajali hiyo huku wengine zaidi ya 72 wakijeruhiwa.
Mashuhuda wanasema kuwa, lori hilo lilikuwa limebeba watu wengi na kupakia mizigo kupindukia lilipata ajali  na kupinduka huku likiendeshwa kwa mwendo wa kasi.
Kawaida malori katika Jamhuri ya Afrika ya Kati hupakia watu na mizigo namna hii
Ripoti zinaonyesha kuwa, kumekuwa kukitokea ajali kama hizo katika maeneo ya katikati na magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati huku chanzo cha ajali hizo kikitajwa kuwa ni ukiukaji wa sheria za barabarani.
Polisi ya usalama barabarani nchini humo inalaumiwa kutokana nja kutowachukulia hatua kali madereva wasioheshimu sheria za barabarani.
Baadhi ya duru zinasema kuwa, kikosi cha usalama barabarani kimekuwa kikipokea rushwa na hivyo kufumbia macho makosa ya madereva hasa ya mwendo wa kasi na kupakia abiria na mizigo kupita kiasi.