Tuesday, June 27, 2017

PROPAGANDA ZA KITOTO ZA MAREKANI DHIDI YA SYRIA

Mapema jana asubuhi, Ikulu ya Marekani (White House) ilitoa tamko lisilo na mashiko ikidai kuwa serikali ya Syria ina nia ya kufanya shambulio la silaha za kemikali.
Katika tamko lake hilo, Ikulu ya Marekani imezungumzia matokeo ya shambulio ambalo hata halijafanyika na kudai kuwa: Eti Washington imegundua mpango wa serikali ya Syria wa kufanya shambulio la silaha za kemikali lenye nia ya kuua kwa umati raia wakiwemo watoto wadogo wasio na hatia. 
al Shairat, Syria

Marekani imedai pia kuwa, eti harakati za hivi sasa za serikali ya Syria zinafanana na zile za kabla ya shambulio la kemikali la rehe 4 Aprili 2017. White House imekumbushia shambulio la kemikali lililotokea katika eneo la Khan Sheikhun katika mkoa wa Idlib nchini Syria ambapo makumi ya watu waliuawa. Marekani na madola ya Magharibi yaliituhumu serikali ya Syria kuwa ilifanya shambulio hilo na hapo hapo Washington ikashambulia kambi ya jeshi la anga la Syria cha Shayrat katika mkoa wa Homs kwa makombora ya Tomahawk kabla ya hata kuthibitishwa iwapo ni kweli shambulio hilo lilitokea au la. Marekani ilifanya shambulizi hilo bila ya hata idhini ya Umoja wa Mataifa na licha ya kwamba mwaka 2014, Umoja wa Mataifa uliwatangazia walimwengu wote kuwa Syria haina tena silaha za kemikali. 
Seymour Hersh ni mwandishi wa habari maarufu wa nchini Marekani. Amesema kuhusiana na jambo hilo kwamba, kinyume kabisa na madai mapya ya wanasiasa wa Ikulu ya Marekani (White House) wanaodai kuwa serikali ya Syria inajiandaa kufanya shambulizi la kemikali; kwa upande wao, maafisa wa kijeshi wa Marekani wanasema hawana taarifa zozote za jambo hilo. Seymour Hersh amejibu madai hayo mapya ya serikali ya Marekani dhidi ya Syria kwa kusema: Maafisa wa kijeshi wa Marekani wamesema kwamba, hawana taarifa yoyote ya kujiandaa Damascus kufanya shambulio la kemikali.

Madai ya wanasiasa wa Marekani ya kwamba serikali ya Syria inajiandaa kufanya shambulio la kemikali yametolewa katika hali ambayo, duru mbalimbali za Marekani ikiwemo taasisi ya nchi hiyo ya utafiti kuhusu magaidi wa Daesh inayojulikana kwa jina la IHS imetangaza mara nyingi kuwa, tangu mwaka 2014 hadi hivi sasa, genge la kigaidi la Daesh (ISIS) limefanya makumi ya mashambulio ya kemikali katika nchi za Syria na Iraq. Wimbi la propaganda mpya za Marekani dhidi ya Damascus limezushwa katika hali ambayo jeshi Syria na vikosi vya kujitolea vya wananchi, linazidi kupata ushindi katika medani za kupambana na magenge ya kigaidi nchini humo. Katika wiki za hivi karibuni, maeneo mengi ya Syria yamekombolewa kutoka kwenye makucha ya magenge ya kigaidi yanayopata misaada ya kila namna kutoka nje ya nchi hiyo. Kwa kuzingatia hayo, jeshi la Syria halina haja yoyote ya kutumia silaha za kemikali kwani linazidi kupata ushindi katika medani za mapambano. Pande ambazo zina uwezekano mkubwa wa kufanya mashambulizi ya kemikali ni zile zinazozidi kushindwa na kupoteza maeneo ziliyokuwa zinayashikilia. Hakuna anayepinga kuwa, magenge ya kigaidi nchini Syria, hayasiti hata kidogo kufanya jinai yoyote ile. Hivyo kutumia magenge hayo ya kigaidi, silaha za kemikali yalizopewa na nchi za Magharibi, ni jambo rahisi sana. 
Serikali ya Syria imekumbwa na wimbi jipya la propaganda za kitoto za Marekani katika hali ambayo, tarehe 27 Septemba, 2017, Syria ilikabidhi kwa Umoja wa Mataifa silaha zake zote za kemikali kwa mujibu wa azimio nambari 2118 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, na umoja huo ukaishukuru rasmi serikali ya Syria kwa ushirikiano wake huo mzuri. 
Rais Bashar al Assad wa Syria akikagua wanajeshi walioko mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya magaidi

Kwa kweli si jambo la kushanga kuiona Marekani na waungaji mkono wengine wa makundi ya kigaidi, wakiyakingia kifua magenge hayo ya kikatili kwa njia yoyote ile, ikiwa ni pamoja na kuisakama kwa kila aina ya propaganda serikali halali ya Syria. Hii pia si mara ya kwanza kwa waungaji mkono hao wa magaidi, kuyaunga mkono magenge hayo ya wakufurishaji kwa kila aina ya uungaji mkono, hasa pale wanapoona yameelemewa na mashambulio ya ukombozi wa ardhi ya Syria yanayoendeshwa na serikali ya Rais Bashar al Assad na waitifaki wake. Tusisahau pia kuwa, hivi karibuni, muungano unaoongozwa na  Marekani wa eti kupambana na ISIS umekuwa ukifanya mauaji makubwa ya raia huko Syria na Iraq. Weledi wa mambo wanaamini kuwa, propaganda mpya za kitoto za Marekani dhidi ya Syria zina mfungamano wa moja kwa moja na njama za Marekani za kuficha jinai zake dhidi ya wananchi wa Syria. 

IRAN YALAANI UAMUZI WA MAHAKAMA KUU YA MAREKANI DHIDI YA WAISLAMU

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amepinga uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu ya Marekani dhidi ya Waislamu na kusema kuwa, kutokana na mitazamo yake finyu ya kibiashara, Washington imefumbia jicho wasababishaji halisi wa ugaidi nchini Marekani na kutoa ujumbe usiofaa.
Bahram Qassemi amesema kuwa, uamuzi uliotolewa na Mahakama Kuu ya Marekani dhidi ya Waislamu ni kielelezo cha mienendo ya kibaguzi ya serikali ya Washingon dhidi ya Waislamu na mtazamo usio wa kiadilifu kuhusu wafuasi wa dini hiyo. 
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesisitiza kuwa, mtazamo wa watawala wa Marekani kuhusu Waislamu wanaofanya safari au wanaoishi nchini Marekani daima umekuwa mbaya, wa dharau na kuwadhalilisha wafuasi wa dini hiyo ya Mwenyezi Mungu ambao kwa mujibu wa ushahidi wa historia wamekuwa wakiheshimu sheria, kuishi kwa amani na kujiehpusha na vitendo vya utumiaji mabavu na misimamo mikali.
Maandamano ya kupinga amri ya Trump, Marekani
Mahakama Kuu ya Marekani Jumatatu iliyopita iliiruhusu serikali ya Rais Donald Trump wa nchi hiyo kutekeleza sehemu ya amri ya kuwazuia Waislamu wa nchi kadhaa kuingia katika ardhi ya nchi hiyo. 
Amri hiyo ya Trump haikuwahusisha raia kutoka nchi kama Saudi Arabia na washirika wake ambazo ndiyo waleaji na waungaji mkono wa makundi ya kigaidi. 

IRAN: NJAMA MPYA ZA MAREKANI DHIDI YA SYRIA NI KWA MANUFAA YA MAGAIDI

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kitendo cha Marekani cha kuzusha vurugu mpya nchini Syria kwa kutegemea madai ya uongo, si kwa faida ya yeyote isipokuwa magaidi wa ISIS.
Itakumbukwa kuwa, mapema leo alfajiri, Sean Spicer, msemaji wa Ikulu ya Marekani (White House) amedai bila ya ushahidi wowote kwamba, iwapo Syria itafanya shambulio la kemikali, basi italazimika kutoa gharama kubwa ya shambulio hilo.
Chuki za kidini dhidi ya Waislamu zimeongezeka sana nchini Marekani hasa baada ya kuingia madarakani Donald Trump mwenye chuki kubwa na Waislamu
Shirika la habari la IRIB limemnukuu Mohammad Javad Zarif, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran akisema kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Tweeter kwamba, njama za Marekani za kuzusha vurugu mpya nchini Syria kwa madai ya uongo ni kwa manufaa ya magaidi wa Daesh tu tena katika wakati huu ambapo genge hilo linazidi kuangamizwa na wananchi wa Iraq na Syria.
Kambi ya jeshi la anga ya Shayrat nchini Syria

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran aidha amesema kuwa uamuzi wa Mahakama Kuu ya Marekani wa kuruhusu kutekelezwa siasa za rais wa Marekani, Donald Trump za kupiga marufuku raia wa nchi za Kiislamu kuingia nchini Marekani, hauwezi kuidhaminia Marekani usalama wake. Pia amesema, inachotakiwa kufanya Marekani ni kuachana na siasa za misimamo mikali na kujiunga na wale wanaopambana kikweli na misimamo hiyo.
Licha ya rais wa Marekani kuwa na chuki kubwa dhidi ya Waislamu, lakini viongozi wa Saudi Arabia walimkaribisha Riyadh kwa heshima zote. Hapa mfalme Salman wa Saudi Arabia akicheza ngoma kwa furaha tele pamoja na Trump mjini Riyadh

Jana Jumatatu, Mahakama Kuu ya Marekani iliiruhusu serikali ya Donald Trump itekeleze marufuku yake ya siku 90 ya kuingia nchini Marekani raia wa nchi za Kiislamu za Iran, Libya, Somalia, Sudan, Syria na Yemen. Katika miezi ya Januari na Machi 2017, Trump alitoa amri ya kuzuiwa kuingia Marekani raia wa nchi hizo sita za Kiislamu. Hata hivyo hadi hivi sasa amri hiyo ilikuwa imekwama kutokana na majimbo mbalimbali ya Marekani kukataa kuitekeleza.  

Monday, June 26, 2017

KIONGOZI MUADHAMU. MATUKIO YA YEMEN NA BAHRAIN NI JERAHA KUBWA KWA ULIMWENGU WA KIISLAMU

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, matukio yanayojiri nchini Yemen na Bahrain ni jeraha kubwa linaoukabili umma wa Kiislamu na ameutaka ulimwengu wa Kiislamu kulisaidia kwa hali na mali taifa ya Yemen.
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo asubuhi katika hotuba aliyoitoa baada ya swala ya Iddil-Fitri iliyoswaliwa leo hapa mjini Tehran ambapo ameutaka umma wa Kiislamu kusimama imara na kuisaidia Yemen kwa namna ya wazi  kabisa kutokana na ukatili inaofanyiwa. Amesisitiza kwa kusema: "Ni lazima maulamaa wa Kiislamu wachukue hatua kuhusiana na kinachojiri katika baadhi ya nchi za Kiislamu hata kama suala hilo litawakasirisha makafiri."
Kiongozi Muadhamu Sayyid Ali Khamenei akiswalisha swala ya Iddil-Fitri
Kadhalika amezungumzia mafanikio mbalimbali ya kimaanawi yaliyopatikana ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhani uliomalizika jana Jumapili, yakiwemo matendo ya ibada na kusema kuwa, shambulio la Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran SEPAH dhidi ya magaidi katika mji wa Deir Ezzor nchini Syria, ni amali tukufu ya Siku ya Kimataifa ya Quds na kushiriki kwa wingi watu katika matembezi ya siku hiyo tukufu ni miongoni mwa matukio muhimu yaliyotokea ndani ya mwezi humo mtukufu wa Ramadhani. Swala ya Iddul-Fitri nchini Iran imeswalishwa kitaifa na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei hapa Tehran, ambapo idadi kubwa ya Waislamu wa mji wa Tehran wameshiriki swala hiyo.
Mashambulizi makali yanayofanywa na Saudia, Israel na Marekani dhidi ya Yemen
Ni zaidi ya miaka mitatu sasa ambapo taifa la Yemen linashuhudia mashambulizi makali na mzingiro wa kila upande wa Saudia na washirika wake wa nchi Kiarabu kwa baraka kamili za Marekani, Israel na baadhi ya nchi za Ulaya.

Tuesday, June 13, 2017

WATU 15 BAADA YA JENGO KUPOROMOKA

Watu 15 hadi sasa hawajulikano waliko baada ya jengo la ghorofa saba kuporomoka katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi Jumatatu usiku.
Kamanda wa Polisi Nairobi Japheth Koome anasema watu 121 waliokolewa punde baada ya jingo hilo kuporomoka saa nne usiku katika mtaa wa Kware eneo la Embakasi mashariki mwa Nairobi.
Koome amesema kuna wakaazi takribani 15 wa jengo hilo ambao hawajulikano waliko kwani baadhi walikataa kuondoka wakati walipotakiwa kufanya hivyo jengo lilipoonekana linaelekea kuporomoka.



Msemaji wa Idara ya Kitaifa ya Kukabiliana na Maafa  Pius Masai amesema familia nyingi zilishirikiana na kuweza kuondolewa katika jengo hilo lakini bado waokoaji wanajaribu kuwatafuta watu wanaoaminika kufunikwa na vifusi.
Gavana wa Nairbi Evans Kidero alitembelea eneo la tukio na kusema jengo hilo limejengwa kinyume cha sharia. Aidha amesema majengo 30,000 Nairobi yanatakiwa kubomolewa kwa sababu yamejengwa kwa viwango duni na ni hatari kwa maisha ya wakazi. Mwaka jana watu 50 walipoteza maisha wakati jengo lilipoporomoka katika mtaa wa Huruma mjini Nairobi.

Monday, June 12, 2017

MACRON ANYEMELEA USHINDI UCHAGUZI WA BUNGE UFARANSA

Wapiga kura nchini Ufaransa wamerudi tena vituoni Jumapili (11.06.2017) kwa duru ya kwanza ya uchaguzi wa bunge ambayo inatabiriwa utakipa chama cha mrengo wa wastani cha Rais Emmanuel Macron wingi wa viti bungeni.

Frankreich Staatspräsident Macron wählt in Le Touquet (Reuters/C. Petit Tesson)
Wapiga kura nchini Ufaransa wamerudi tena vituoni Jumapili (11.06.2017) kwa duru ya kwanza ya uchaguzi wa bunge ambayo inatabiriwa utakipa chama cha mrengo wa wastani cha Rais Emmanuel Macron wingi wa viti bungeni.
Macron amekuwa akifurahia fungate ya kisiasa tokea alipomshinda mgombea wa sera kali za mrengo wa kulia Marine Le Pen na kuja kuwa rais kijana kabisa wa Ufaransa kuwahi kutokea hapo Mei 7 na kutangaza baraza la mawaziri lisilojikita katika mgawanyiko ulioko  kati ya sera za mrengo wa kulia na kushoto pamoja na kuonekana kujiamini katika mikutano yake na Rais Donald Trump wa Marekani na Rais Vladimir Putin wa Urusi.
Lakini rais huyo amefanya nusu tu ya kazi.Chama chake cha Republique en Marche (Republic on the Move REM) ambacho amekiasisi miezi 14 tu iliopita kinahitaji kuwa na wingi wa viti katika Bunge la Taifa ili kuweza kupitisha mageuzi aliyoahidi wakati wa kampeni yake.
Uchunguzi wa maoni mara kadhaa umeonyesha kwamba chama cha Macron ambacho hakikuwahi kujaribiwa kinaweza kujinyakulia asilimia 30 ya kura katika duru ya kwanza na kukiweka katika njia ya kunyakuwa ushindi wa kishindo katika duru ya pili Ijumapili ijayo.
Chama cha sera za mrengo wa kati kulia cha Republicans na kile cha Socialist vinahofia kushindwa vibaya baada ya wagombea wao kushindwa kufikia ngazi ya marudio ya uchaguzi wa rais kwa mara ya kwanza katika historia ya Ufaransa baada ya kipindi cha vita.
REM yatabiriwa kupata wingi wa viti
Frankreich Wahlen Nationalversammlung Emmanuel Macron (Reuters/P. Wojazer)
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa akisalimiana na watu.
Baadhi ya utabiri unaashiria kwamba chama cha REM kinaweza kushinda kama viti 400 katika bunge hilo lenye viti 477 kutokana na azma ya wapiga kura kutaka kumpa rais huyo mpya mamlaka yenye nguvu.
Chama hicho tayari kinaongoza katika majimbo ya uchaguzi 19 kati ya 11 ya himaya za Ufaransa nchi za nje ambayo yamefanya duru yao ya kwanza ya uchaguzi mwishoni mwa juma lililopita.
Hapo Jumapili Macron baada ya kusalimana kwa kupeana mikono na watu waliomtakia heri na kupiga nao picha za simu ya mkononi alipiga kura yake katika mji wa kitalii wa kaskazini wa Le Touqet ambapo yeye na mke wake mwenye umri wa mika 64 Brigitte wana nyumba yao.
Usalama waimarishwa
Frankreich Wahlen Nationalversammlung (Getty Images/AFP/F. Tanneau)
Zoezi la kupiga kura ya bunge.
Wabunge wachache wanatazamiwa kuchaguliwa katika duru ya kwanza.Iwapo hakuna mgombea atakayepata zaidi ya asilimia 50,wagomea wawili wa juu wanaongoza wataingia duru ya pili sawa na mgombea aliyejikusanyia angalau asilimia 12.5 ya wapiga kura waliojiandikisha.
Vituo vya kupiga kura katika miji mkubwa vitakuwa wazi hadii saa mbili usiku ambao matokeo ya awali yataanza kutolewa muda mfupi baada ya hapo.
Kufikia mchana asilmia 19.24 miongoni mwa wapiga kura milioni 47 wanaostahili kupiga kura ilikuwa imejitokeza ikiwa ni chini kwa asilimia 21.06 katika wakati kama huo wakati wa uchaguzi wa bunge mwaka 2012.
Zaidi ya polisi 50,000 walikuwa katika doria katika nchi ambayo bado iko katika wasi wasi baada ya wimbi la mashambulizi ya wapiganaji wa jihadi kuuwa zaidi ya watu 230 tokea mwaka 2015.
Katika tuko la hivi karibuni kabisa Mualgeria aliyejipandikiza itikadi kali mwenye umri wa miaka 40 alipigwa risasi na kujeruhiwa baada ya kumshambula polisi na nyundo nje ya kanisa la Notre Dame mjini Paris.

SAUDIA YAWAPIGA MARUFUKU RAIA WA QATAR KUINGIA MASJID AL-HARAM

Mgogoro wa kidiplomasia ulioibuka kati ya Saudi Arabia ikishirikiana na nchi kadhaa za Kiarabu dhidi ya Qatar unaonekana kuchukua sura mpya baada ya watawala wa Aal Saud kuwazuia raia wa Qatar kuingia katika msikiti wa Makka.
Ripoti zinasema kuwa, baada ya kuzuka mgogoro huo raia wa Qatar wamekuwa wakizuiwa kuingia katika Masjid al-Haram.
Gazeti la al-Sharq limemnukuu afisa mmoja wa kamati ya taifa ya haki za binadamu ya Qatar akitangaza kuwa, raia wa nchi hiyo wamezuiwa na Saudia kuingia katika msikiti wa Makka. Aidha vyombo vya usalama vya Saudia vimewataka raia hao kuondoka nchini humo mara moja.
Ali bin Samikh Al Marri, Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Haki za Binadamu ya Qatar amelaani vikali hatua hiyo ya Saudia ya kuingiza masuala ya kisiasa katika ibada na kubainisha kwamba, hatua iliyochukuliwa na baadhi ya nchi za Kiarabu ya kuiwekea vikwazo Qatar ni jinai ya kimataifa.
Mfalme Salman wa Saudia na Rais al Sisi wa Misri
Ameongeza kuwa, kamati yao imeshapokea mashtaka 700 ya raia wa nchi hiyo waliodhurika na mzingiro wa Saudia na washirika wake dhidi ya Qatar.
Siku chache zilizopita nchi za Saudi Arabia, Imarati, Misri na Bahrain zilikata uhusiano wao wa kidiplomasia na Qatar na kuzuia safari za anga, nchi kavu na baharini kuelekea katika nchi hiyo. Nchi nyingine kadhaa ambazo ni vibaraka wa Saudia nazo zimejiunga na nchi hizo.
Serikali ya Qatar imetangaza kuwa, Saudia na baadhi ya nchi za Kiarabu zinataka  kuiweka nchi hiyo chini ya udhibiti wao suala ambalo linakiuka kikamilifu haki ya kujitawala na kusisitiza kuwa, jambo hilo kamwe haliwezi kukubalika.

11 WAUAWA HUKU WAFUNGWA WAPATAO ELFU MOJA WAKITOROKA JELA KONGO DR

Watu wasiopungua 11 wameuawa huku wafungwa 930 wakitoroka jela wakati watu wenye silaha wasiojulikana walipovamia jela moja iliyoko kwenye mji wa Beni, kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Gavana wa mkoa wa Kivu Kaskazini Julien Paluku ametangaza kupitia taarifa kuwa katika uvamizi huo uliotokea jana, washambuliaji hao walitumia silaha nzito nzito na kuwaua walinzi wanane wa jela hiyo.
Shambulio hilo la jana ni la nne kwa akali la utorokaji jela kutokea nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ndani ya kipindi cha mwezi mmoja uliopita, likionyesha ni jinsi gani hali ya ukosefu wa usalama ilivyoongezeka nchini humo tangu Rais Joseph Kabila alipokataa kungátuka madarakani baada ya muhula wake wa uongozi kumalizika mwezi Desemba mwaka jana.

Rais Joseph Kabila 

Teddy Kataliko, ambaye ni mwanaharakati katika mkoa wa Kivu Kaskazini amesema haijaweza kufahamika ni nani hasa waliofanya shambulio hilo la kuvamia jela kwa sababu wanamgambo wengi wanaojihami kwa silaha ambao wanajulikana kama Mai Mai wanaendesha harakati zao katika mji wa Beni.
Kwa mujibu wa Polisi, wafungwa wapatao 4,000 walitoroka jela mwezi uliopita katika jela yenye ulinzi na usalama wa hali juu iliyoko kwenye mji mkuu wa Kongo DR, Kinshasa ambapo kundi la watu wanaopigania kujitenga lilihusishwa na hujuma hiyo. Wafungwa wengine wasiopungua watatu walitoroka katika jela nyengine ya mjini Kinshasa siku ya Jumamosi iliyopita.../

Saturday, June 10, 2017

THRRESA MAY AUNDA SERIKALI YA WINGI MDOGO

Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May anakabiliwa na msururu wa ukosoaji baada ya kampeni ya uchaguzi iliyoshindwa na kusababisha kupungukiwa na wingi katika bunge na anatarajia kuwania kulinda nafasi yake ya uongozi 

London Theresa May Seeks Queen's Permission To Form A UK Government (Getty Images/S. Rousseau)
Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May
 Wakati  akipambana kulinda  nafasi  yake ya uongozi  lakini dakika zinayoyoma  kuelekea kuanza mazungumzo ya Uingereza  kujitoa  kutoka  Umoja  wa Ulaya.
Kamari aliyocheza  May kwamba  angeweza  kutumia mapenzi  ya watu  wa  Uingereza  kujitoa  kutoka  Umoja  wa  Ulaya  na  kile kilichoonekana  kuwa  ni  udhaifu  wa  chama  cha  upinzani  cha Labour ilimrudia  mwenyewe  siku  ya  Alhamis  wakati wapiga  kura walipomuondolea  wingi  wake  katika  bunge.
Großbritannien Wahlen 2017 – Jeremy Corbyn (picture alliance/PA Wire/D. Lipinski)
Kiongozi wa chama cha upinzani nchini Uingereza cha Labour Jeremy Corbyn
Matokeo  hayo  ya  kushangaza, ambayo  yamesababisha  sarafu ya  pauni  kuporomoka thamani, yamemlazimisha  May  kuunda serikali  yenye  wingi  mdogo, na  kumuacha  kutegemea  kundi  dogo la  wabunge wa  Ireland  ya  kaskazini, ikiwa  ni  siku  tisa  tu  kabal ya  Uingereza  kuanza  majadiliano  ya  kupata  makubaliano ya kujitoa  kutoka  Umoja  wa  Ulaya.
Vyombo  vya  habari  vya  Uingereza  ambavyo  kwa  kawaida  vina msimamo  wa  siasa za  mrengo  wa  kulia  vimemrarua  May kuhusiana  na  matokeo  ya  uchaguzi, vikihoji  iwapo  ataweza kuendelea  kubaki  madarakani  baada  ya  matokeo  ambayo yanamuweka  katika  hali  ya  kutegemea  kuyaunganisha  makundi hasimu  ndani  ya  chama  chake ili  kuweza  kufanikisha  Brexit.
"May anatumbua macho katika anga tupu," limeandika gazeti la Jumamosi la The Times wakati Daily Mail limeandika "Wahafidhina wamgeukia Theresa".
Großbritannien David Davis Verhandlungsführer Brexit (picture-alliance/Zumapress/R. Pinney)
David Davis waziri wa Uingereza atakayeongoza mazungumzo ya Brexit
Gazeti  la Telegraph  limeandika  wahafidhina  waandamizi  ikiwa  ni pamoja  na  waziri  wa  mambo  ya  kigeni Boris Johnson , waziri  wa mambo  ya  ndani Amber Rudd  na  waziri  wa  Brexit David Davis wanaangalia  uwezekano  iwapo  wamuondoe  madarakani.
May bado akakamaa
"Wakati  nikitafakari  kuhusiana  na  matokeo  nitatafakari  kuhusu kile tunachotakiwa  kufanya  hapo  baadaye  ili  kukipeleka  chama mbele," May  amesema  jana  Ijumaa  katika  taarifa   iliyotolewa katika  televisheni.
Gazeti  linalouzwa  kwa  wingi  nchini  Uingereza la  Sun  limesema wanachama  waandamizi  wa  chama  chake  wameapa  kumuondoa madarakani, lakini  watasubiri  kwa  takriban miezi  sita  kwasababu wanawasi wasi kwamba mvutano  wa  kuwania  uongozi  kwa  hivi sasa  kunaweza  kumuingiza  madarakani  kiongozi  wa  chama  cha Labour Jeremy Corbyn.
"Theresa  May bila  shaka  ni  kiongozi  imara  ambaye  tunaye  hivi sasa ," David Davis , waziri wa  Brexit, ameliambia  shirika  la habari  la  BBC. Amesema  kuwa  itakuwa  vigumu kutabiri iwapo bado  atakuwa  waziri mkuu mwishoni  mwa  mwaka  huu.
Großbritannien Protest gegen Brexit (Getty Images/AFP/N. Hallen)
Maandamano dhidi ya kujitoa kutoka Umoja wa Ulaya yaliyofanyika Julai 2, 2016 mjini London
Wabunge  kadhaa walidai kujiuzulu  kwa  washauri  wa  ngazi  ya  juu wa  May, ambao  wamekuwa wakilaumiwa kwa sera  mbovu kuwafanya  wazee kulipa fedha  zaidi  kwa  ajili ya matunzo  yao  na kampeni  iliyoonekana kuwa  iko  mbali  mno  na  watu  wa  kawaida na  inayolenga  mno  kuwashambulia  wapinzani  wao.
Baada  ya  kuthibitisha  jana  Ijumaa (09.06.2017) kwamba  mawaziri wake  wa  juu wataendelea  na  nyadhifa  zao , ikiwa  ni  pamoja  na waziri  wa  fedha Philip hammond , May anatarajiwa  kuendelea kuliteua  baraza  lake  la  mawaziri  ambalo  litafanya  moja  kati  ya majadiliano  magumu  kabisa  katika  historia  ya  Uingereza.
Mazungumzo kuanza  kama yalivyopangwa
May amesema  mazungumzo  ya  Brexit  yataanza  rasmi  Juni  19 kama  ilivyopangwa, siku  hiyo  hiyo  ambayo  bunge  litafunguliwa rasmi. Lakini matokeo  ya  uchaguzi  yana maana  haiko  wazi  iwapo mpango  wake  kuitoa  Uingereza  kutoka  katika  soko  la  pamoja na  Umoja  wa  Ulaya  pamoja  na  umoja  wa  forodha  unaweza  pia kuendelea.
Wanasiasa wa  Uingereza, ikiwa  ni  pamoja  na  wa  chama  cha May  binafsi, wanatofautiana  kwa  kiasi  kikubwa  kuhusiana  na  kile wanachotaka   kutoka  katika  mchakato  wa  majadiliano  ya  Brexit.
Großbritannien Wahlen 2017 – Auszählung (picture-alliance/AP Photo/F. Augstein)
Kura zikihesabiwa katika uchaguzi wa Juni 9 , 2017
Iwapo atafanikiwa  kufikisha  mwisho  wa  uanachama  wa Uingereza  katika  Umoja  wa  Ulaya ambapo  asilimia  52  ya Waingereza  walitaka mwaka  jana, ni  lazima  atafute  njia  kuweza kupata  uungwaji  kamili  mkono  wa  chama  chake  kwasababu atahitaji  kura  zao  kuweza  kupitisha  sheria  inayotayarisha uidhinishaji  wa  hatua  hiyo  ya  kujitoa.
May pia atahitaji  uungwaji  mkono  wa  wahafidhina wanaopendelea masuala  ya  kijamii, chama  cha  siasa  za  kizalendo  cha Democratic Unionist kinachopendelea  kujitoa  kutoka  Umoja  wa Ulaya (DUP) ambacho  kimeshinda  viti  10  katika  Ireland ya kaskazini.

Friday, June 9, 2017

MBUNGE MAREKANI: HUJUMA ZA KIGAIDI TEHRAN NI STRATEJIA YA TRUMP

Mbunge katika chama tawala cha Republican nchini Marekani amesema hujuma za hivi karibuni za kundi la kigaidi la ISIS mjini Tehran inaweza kuwa stratijia ya Rais Donald Trump.
Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Dana Rohrabacher, ambaye anawakilisha California katika Bunge la Kongresi, ametoa matamshi hayo katika kikao cha Alhamisi cha Kamati ya Sera za Kigeni ya Kongresi ambayo ilikuwa ikijadili kuhusu Harakati ya Hizbullah ya Lebanon.
Dana Rohrabacher ambaye alionekana kuunga mkono hujuma za kigaidi za Jumatano dhidi ya watu wa Iran alisema kundi la kigaidi lililotekeleza hujuma hiyo linapaswa kuchochewa zaidi kuishambulia Iran.
Ikumbukwe kuwa siku ya Jumatano, timu ya magaidi wa Daesh (ISIS) walishambulia Haram ya Imam Khomeini MA na eneo la Bunge la Iran mjini Tehran na kuwaua shahidi watu 17 huku wengine karibu 50 wakijeruhiwa. Magaidi watano waliotekeleza hujuma hiyo waliangamizwa na maafisa wa usalama huku wahusika wengine 41 wakikamatwa katika maeneo mbali mbali ya Iran.
Gaidi wa ISIS akiwamiminia raia risasi katika ukumbi wa wageni wa jengo la idara ya Bunge la Iran
Mbunge huyo mwenye misimamo mikali wa chama cha Republican amesema iwapo stratijia ya Trump ni kuchochea hujuma za kigaidi Iran basi anaunga mkono jambo hilo. Amesema anaunga mkono Marekani kushirikiana na ISIS katika vita dhidi ya Iran na kutoa mfano wa namna Marekani ilivyoshirikiana na Joseph Stalin, aliyemtaja kuwa muovu, katika kumuangusha Adolf Hitler katika Ujerumani ya Wanazi.
Ifahamike kuwa kundi la ISIS lilianzishwa miaka kadhaa iliyopita kwa uungaji mkono wa kifedha na kijeshi wa Marekani na waitifaki wake wa Kiarabu hasa Saudi Arabia. Kundi hilo limetenda jinai za kuogofya katika nchi kadhaa hasa Iraq na Syria lakini katika miezi ya hivi karibuni limeanza kupata pigo na kupoteza ardhi ambazo lilikuwa limeziteka katika nchi hizo mbili.

MAY ATAKA KUUNDA SERIKALI NA DEMOCRATIC UNIONIST

Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May amesema atabakia madarakani na kuunda serikali,  baada ya uchaguzi mkuu hapo jana ambapo chama chake cha Conservative kilipoteza wingi wake bungeni.

London Theresa May (picture-alliance/empics/J. Brady)
Waziri Mkuu May alielezea uamuzi wake wa kuunda serikali licha ya chama cha Conservative kutokuwa na wingi bungeni, katika taarifa yake kwa waandishi habari nje ya makao yake makuu ya Nambari 10 mtaa wa Downing mjini London, na baada ya kuonana na Malkia Elizabeth kwenye kasri la Buckingham na kumuomba ampe nafasi ya kuunda serikali mpya.
May ameahidi kushirikiana na wale aliowaita marafiki na washirika na hasa katika Chama cha  Democratic Unionist (DUP), ambacho ndicho kikubwa kabisa katika Ireland ya Kaskazini na kinaweza kumpa May uungaji mkono wa kutosha kuweza kutawala.
"Vyama vyetu hivi viwili vimekuwa na uhusiano imara kwa miaka mingi na nina matumaini kuwa tutaweza kufanya kazi pamoja kwa maslahi ya Uingereza," alisema May. 
DUP kinachotetea jimbo hilo libakie kuwa sehemu ya Uingereza na chenye msimamo wa kihafidhina panapohusika masuala ya kijamii, kimeongeza idadi yake ya viti kufikia 10. Chama cha Conservative kimepata viti 318 , Labour 261, Scotish Nationalist (SNP) 35 na Liberal Democrats viti 12.
May ajipanga upya kwa Brexit
London Labour Führer Jeremy Corbyn (Getty Images/C. Furlong)
Kiongozi wa chama cha Labour, Jeremy Corbyn, ambaye chama chake kimeongeza viti bungeni licha ya kushindwa kupata wingi wa kutosha kuunda serikali.
Akizungumzia majadiliano ya kujitoa katika Umoja wa Ulaya, mchakato unaojulikana kama Brexit, yatakayoanza tarehe 19 mwezi huu, Waziri Mkuu huyo aliyeitisha uchaguzi wa mapema kwa lengo la kujipa nguvu za kusimama imara kwenye mazungumzo hayo alisema serikali yake mpya itaiongoza nchi kupitia mazungumzo muhimu kwa kutekeleza "maamuzi ya umma wa Uingereza kwa kuitoa kwenye Umoja wa Ulaya".
"Nitafanya kazi kuiweka nchi yetu katika hali ya usalama kwa kutekeleza malengo niliyoyaweka baada ya  mashambulizi ya Manchester na London," amesisitiza May.
Mapema leo chama cha DUP kilikataa kutamka lolote kuhusiana na ripoti kwamba kimekubali kukiunga mkono chama tawala cha Waziri Mkuu May, ingawa kilikubali kuwa tayari mazungumzo baina yao yameanza.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanaashiria huenda serikali ya May isidumu muda mrefu na wanafikiri kuna uwezekano wa kuitishwa uchaguzi mwengine. 
Kivutio kikubwa katika uchaguzi wa safari hii kuwania viti 650 ni kuchaguliwa kwa idadi kubwa ya wanawake kuliko wakati mwengine wowote, ambapo jumla ya wabunge wanawake 207 wamechaguliwa ikilinganishwa na 196 katika uchaguzi wa 2015. 

WATU 39 WAUAWA KATIKA MASHAMBULIO YA MABOMU YA MAGAIDI WA DAESH IRAQ

Kwa akali watu 39 wameuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa kufuatia mashambulio ya mabomu yaliyofanywa hii leo na kundi la kigaidi la Daesh katika miji ya Babil na Karbala nchini Iraq.
Vyombo vya usalama vya Iraq vimetangaza kuwa, watu wasiopungua 30 wameuawa katika shambulio la kwanza katika mji wa Babil ambapo mtu aliyekuwa amejifunga mabomu alijiripua katikati ya watu. Taarifa zaidi zinasema kuwa, watu 33 wamejeruhiwa katika shambulio hilo la kujitolea muhanga huku hali za baadhi ya majeruhi zikiripotiwa kuwa mbaya.
Mlipuko huo ulitokea katika mlango wa kuingia katika soko la eneo la al-Musayyib na kwamba, kuna uwezekano wa kuongezeka idadi ya wahanga wa shambulio hilo la kigaidi. Taarifa za awali zinasema, mwanamke mmoja ndiye aliyetekeleza shambulio hilo kwa kujiripua katika mji huo ambao wakazi wake wengi ni Waislamu wa madhehebu ya Shia.
Wanachama wa kundi la kigaidi al Daesh nchini Iraq
Aidha katika tukio jengine watu wengine 9 wanaripotiwa kufariki dunia na makumi ya wengine kujeruhiwa baada ya mtu mmoja kujiripua ndani ya kituo cha mabasi ya mji wa Karbala.
Kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh limetangaza kuwa, wanachama wake ndio waliohusika na mashambulio ya leo ya kigaidi nchini Iraq.
Kwa mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa, raia 354 wameuawa nchini Iraq na wengine 470 kujeruhiwa kufuatia mashambulio ya kigaidi katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo yaliyofanywa na makundi ya kigaidi.

MOHAMMADI- GOLPAYEGANI: MAADUI HAWAWEZI KULIKATISHA TAMAA TAIFA LA IRAN KWA KUFANYA MAUAJI

Mkuu wa ofisi ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, hatua ya maadui ya kufanya mauaji katu haiwezi kulikatisha tamaa taifa la Iran.
Hujjatul Islam Walmuslmiin Muhammad Muhammadi-Golpayegani, amebainisha kuwa, sababu ya mashambulio ya juzi ya kigaidi hapa mjini Tehran ni safari ya hivi karibuni ya Rais Donald Trump wa Marekani nchini Saudi Arabia.
Akizungumza katika shughuli ya kuiaga miili ya mashahidi wa mashambulio ya kigaidi ya siku ya Jumatano hapa mjini Tehran, mkuu wa ofisi ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, katika safari ya hivi karibuni ya Trump nchini Saudia kuliratibiwa mipango ya kutoa pigo dhidi ya Iran.
Muhammad Muhammadi Golpeygani, Mkuu wa ofisi ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
Aidha Hujjal Islam Walmuslimiin Muhammad Muhammadi Golpeygani alisoma ujumbe wa rambirambi wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kwa mnasaba wa mashambulizi ya kigaidi yaliyofanyika siku chache zilizopita mjini Tehran akisisitiza kuwa, jinai hiyo haiwezi kutia doa katika irada na azma ya taifa la Iran.
Akizungumza katika hafla hiyo ya kuaga miili mitoharifu ya mashahidi wa mashambulio hayo ya kigaidi, Ali Larijani, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, mashambulio hayo ya kigaidi yameonyesha jinsi magaidi walivyojikita zaidi katika kulenga mhimili mkuu wa mfumo wa utawala wa kidini nchini Iran wenye ridhaa ya wananchi.

Thursday, June 8, 2017

UN: WAPIGANAJI WA DAESH WANAWAUA WATOTOWANAO KIMBIA VITA MOSUL

Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa, wanachama wa kundi la kigaidi la Daesh wanawapiga risasi watoto wanaokimbia vita na mapigano katika mji wa Mosul huko kaskazini mwa Iraq.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa imetahadharisha kuwa, mauaji yanayofanywa na kundi la Daesh dhidi ya raia wanaokimbia mapigano katika mji wa Mosul yamekifikia kiwango cha kutia wasiwasi.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, katika siku chache zilizopita tu raia 231 waliokuwa wakikimbia mapigano huko Mosul wameuawa kwa kupigwa risasi na wapiganaji wa Daesh.
Daesh inaua watoto wa Iraq 
Taarifa ya Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa pia imesema mauaji ya raia yanayosababishwa na mashambulizi ya anga yanatia wasiwasi. Mashambulizi hayo yanafanywa na Marekani na washirika wake.
Wakati huo huo mjumbe wa Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF) nchini Iraq amesema kuwa inakadiriwa kuwa, zaidi ya Wairaq laki moja wanasumbuliwa na hali mbaya kupita kiasi katika mji wa Mosul. 
Raia wanaokimbia vita Mosul
Jeshi la Iraq linaendeleza operesheni ya kukomboa mji huo kutoka kwenye makucha ya kundi la kigaidi la Daesh. Operesheni hiyo ilianza tarehe 19 Februari mwaka huu.  

MAWAHABI WADHANIWA KUFANYA MASHAMBILIZI YA KIGAIDI MJINI TEHRANI, IRAN

Wizara ya Usalama wa Taifa ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imesema kuwa, magaidi waliofanya mashambulizi jana Jumatano hapa Tehran wametambuliwa. Imesema, magaidi hao walikuwa na uhusiano wa moja kwa moja na magenge ya Kiwahabi nje ya Iran.
Wizara ya Usalama wa Taifa ya Iran imesema hayo leo katika taarifa yake maalumu na kuongeza kuwa, timu ya magaidi hao wa Daesh (ISIS) ambao jana walishambulia Haram ya Imam Khomeini MA na eneo la Bunge la Iran walikuwa ni magaidi watano ambao wana historia ya vitendo vya uhalifu na walikuwa wanachama wa magenge ya Kiwahabi ya wakufurishaji.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, baada ya kujiunga na genge la kigaidi la Daesh, magaidi hao walishiriki kwenye jinai za genge hilo huko Mosul, kaskazini mwa Iraq na Raqqah, kaskazini mwa Syria. 
Operesheni ya kupambana na magaidi wa Daesh katika majengo ya Bunge mjini Tehran, Jumatano, Juni 8, 2017

Taarifa ya Wizara ya Usalama wa Taifa ya Iran imeongeza kuwa, katika msimu wa joto wa mwaka jana, magaidi hao waliingia nchini Iran wakiongozwa na Abu Ayesheh, mmoja wa makamanda wa ngazi za juu wa magaidi wa Daesh kwa lengo la kufanya mashambulio kadhaa ya kigaidi katika miji ya kidini ya Iran. Hata hivyo maafisa usalama wa Iran walisambaratisha kikamilifu kundi hilo ikiwa ni pamoja na kumwangamiza Abu Ayesheh. Baadhi ya magaidi wa timu hiyo walifanikiwa kutoroka wakiwemo magaidi hao watano waliofanya mashambulizi ya kigaidi jana Jumatano hapa mjini Tehran.
Magaidi hao walioangamizwa jana mjini Tehran wametambuliwa kwa majina ya: Seriyas, Fereydoun, Qayyoum, Abu Jahad na Ramin. Jana Jumatano tarehe 8 Juni 2017, mji wa Tehran ulishuhudia mashambulizi mawili ya kigaidi katika Haram ya Imam Khomeini (quddisa sirruh) na jengo la kiidara la Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran). 

Wednesday, June 7, 2017

MAPIGANO BUNGENI IRAN

kundi linalojiita Dola la Kiislamu limedai kuhusika na mashambulizi mawili yaliyoteka kwa mfululizo leo hii mjini Tehran, Iran ambayo yanatajwa kusababisha vifo vya hadi watu saba na kuwajeruhi wengine kadhaa.

[No title] (Ilna)
Kundi linajiita Dola la Kiislamu limedai kuhusika na mashambulizi mawili yaliyoteka kwa mfululizo leo hii mjini Tehran, Iran ambayo yanatajwa kusababisha vifo vya hadi watu saba na kuwajeruhi wengine kadhaa. 
Washambuliaji kadhaa wamelishambulia bunge la Iran na mtu alijitoa muhanga alilenga eneo la kaburi la mwanzilishi wa mapinduzi ya Iran hayati Ayatollah Ruhollah Khomeini na kusababisha kifo cha mlinzi na kujeruhi watu wengine 12 katika kile kinachotajwa kuwa mashambulizi ya nadra kutokea. Hayo yanafanyika wakati mizizimo ya risasi ikiendelea katika jengo la bunge.
Kundi la linalojiita dola la Kiislamu IS limedai kuhusika na mashambulizi hayo kupitia mtandao wake wa habari wa AMAQ. Kwa mujibu wa shirika la habari la Iran IRNA-tukio hilo lisilo la kawaida lililotokea katika mji mkuu wa Iran, Tehran, limesababisha Wizara ya Ulinzi kuitisha mkutano wa usalama wa  dharura. Vyombo vya habari nchini humo vinasema helikopta za polisi zinazunguka jengo la bunge na kwamba mawasiliano ya simu zote za mkononi kwa walio ndani ya jengo hilo yamekatwa.
Sakata katika eneo la  bunge
Iran Angriff auf das Parlament in Teheran (Reuters/TIMA)
Askari wakiwa katika doria katika eneo la bunge
Nalo shirika la habari la ISNA linasema milango yote ya kuingilia na kutoka imefungwa na wabunge na waandishi wa habari ambao walikuwemo katika jengo hilo wakati vikao vikiendelea wameamriwa kutulia katika eneo maalumu. Lakini Televisheni ya serikali baadae ilisema waashambuliaji wanne wanahusika katika shambulizi la bungeni, na kwamba watu wanane wamejeruhiwa. Televisheni hiyo ilimnukuu mbunge mmoja Elias Hazrati aliyesema washambuliaji hao walikuwa wamejihami kwa bunduki aina ya Kalashnov.
Vilevile televisheni hiyo ilisema mlinzi aliuwawa na watu wengine wanne wamejeruhiwa katika shambulizi hilo la kwenye eneo la kaburi la Khomeini. Mmoja ya washambuliaji aliuliwa na mlinzi na kuna mwanamke aliyetiwa mbaroni. Chombo hicho kiliwaelezea washambuliaji katika eneo la kaburi kama "magaidi" na kuongeza kuwa mmoja alifanya shambulizi la kujitoa muhanga pasipo kutoa ufafanuzi zaidi.
Pamoja na shambulizi katika eneo la kaburi la Khomeini hatari lakini kaburi la kiongozi huyo limekuwa alama muhimu kwa taifa hilo. Kama kiongozi wa kwanza wa Iran, Khomeini alikuwa kuongozi muhimu wa taiifa hilo na alikuwa kiongozi wa kimapinduzi ya mwaka 1979.
Afisa mwanadamizi ambaye hakutaka kutaja jina lake ameilezea hali kuwa mbaya na kuyataja mashambulizi hayo kuwa pigo kwa rais wa nchi hiyo Hassan Rouhani, akihoji inakuwaje bunge lenye ulinzi mkali likashambuliwa.
Rouhani alisalia madarakani baada ya ushindi wa kishindo dhidi ya mgombea mwenye msimamo mkali wa kihafidhina na vikosi vya ulinzi wa Jamhuri, ambavyo ndiyo vyenye nguvu zaidi nchini Iran. Televisheni ya Iran imesema bunge limerejea shughuli zake na kuonyesha picha za kile ilichosema ni kikao cha ufunguzi kikiendelea kama kawaida.

HASIRA ZA ISRAEL BAADA YA UMOJA WA MATAIFA KUUNGA MKONO KUUNDWA NCHI HURU YA PALESTINA

Danny Danon Balozi wa Utawala wa Kizayuni katika Umoja wa Mataifa amekosoa vikali matamshi ya katibu mkuu wa umoja huo Antonio Gutterres ambaye ameunga mkono uundwaji nchi huru ya Palestina.
Dannon amesema Umoja wa Mataifa unapaswa kujizuia kueneza kile alichodai kuwa ni urongo na kuangazia uhalisia wa mambo katika eneo.
Mjumbe huyo wa utawala wa Kizayuni amedai kuwa ni kichekesho kutuhumiwa kwa ugaidi utawala pekee wa kidemokrasia katika eneo.
Madai hayo ya Dannon kuwa eti utawala wa Kizayuni wa Israel ndio "utawala pekee wa kidemokrasia" Mashariki ya Kati na jitihada za utawala huo za kupotosha ukweli katika eneo hili zinajiri wakati ambao utawala huo umezidisha sera zake za uvamizi na utumiaji mabavu katika eneo. Hivi sasa utawala haramu wa Israel unatambulika kimataifa katika dhihirisho la ukaliaji mabavu, mienendo iliyo dhidi ya binadamu na ubaguzi. Sera hizo za Israel zimezua radiamali za kimataifa.
Kuhusiana na hilo Antonio Guterres Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Jumanne alitaka kuundwe nchi huru ya Palestina na kusema hilo limekuwa takwa la walimwengu kwa muda wa miaka 70 sasa.
Quds Tukufu inayokaliwa kwa mabavu na Israel
Guterres alikuwa akizungumza kwa munasaba wa mwaka wa 50 wa maafa ya 1967 ya kukaliwa kwa mabavu ardhi zaidi za Palestina. Katika taarifa aliyotoa kwa munasaba huo, Gutteres ameitaka Israel ihitimishe ukaliaji wake wa mabavu wa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, Quds Mashariki na Miinuko ya Golan.
Aidha amesisitiza kuwa, kadhia ya Palestina na Wazayuni inapaswa kutatuliwa kwa msingi wa maazimio ya Umoja wa Mataifa na sheria za kimataifa.
Utawala wa Kizayuni umekasirishwa na kauli ya Guterres katika hali ambayo ukatili wa utawala huo ghasibu umesajiliwa katika nyaraka za Umoja wa Mataifa na walimwengu hawatasahau ukatili huo wa Wazayuni.
Utawala wa Kizayuni ni utawala haramu ambao unaungwa mkono na madola ya Magharibi na uliasisiwa mwaka 1948 kwa lengo la kutekeleza sera za kigaidi dhidi ya Wapalestina na kukalia kwa mabavu ardhi za Palestina ikiwa ni pamoja na Quds Tukufu. Kwa hivyo tokea kuasisiwa kwake, utawala huo umekuwa ni utawala wa shari na vamizi katika eneo la Mashariki ya Kati.
Katika fremu hiyo katika vita vya mwaka 1967, utawala wa Kizayuni katika vita vyake na nchi za Kiarabu ulikalia kwa mabavu ardhi zaidi za Palestina ikiwa ni pamoja na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na sehemu ya Baitul Maqqdis na sehemu ya ardhi za nchi za Kiarabu ikiwa ni pamoja na Miinuko ya Golan ya Syria. Kwa hivyo utambulisho wa kivita wa utawala huo uko wazi kwa walimwengu.
Miinuko ya Golan ya Syria inayokaliwa kwa mabavu na Israel
Utawala huo umekuwa ukijaribu kubadilisha fikra za walimwengu kwa kutoa tuhuma zisizo na msingi dhidi ya taasisi za kimataifa.
Maazimio kadhaa ya taasisi za kimataifa hasa Umoja wa Mataifa dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel hasa kulaani sera za ukaliaji mabavu za utawala huo ni jambo linaloonyesha kuwa jamii ya kimataifa haikubali sera za kujitanua za utawala huo.
Matukio ya kimataifa yanaonyesha jamii ya kimataifa haiwezi kustahamili tena kushuhudia jinai za utawala huo wa Kizayuni ambao ni utawala haramu na ambao unapata himaya ya nchi za Magharibi.
Maazimio mbali mbali ya Umoja wa Mataifa ikiwa ni pamoja na azimio 242 na 338 yamebainisha wazi kuwa utawala wa Kizayuni unapaswa kuondoka katika ardhi unaozikalia kwa mabavu.
Katika miaka ya hivi karibuni kumeshuhudiwa harakati za kimataifa za kuunga mkono haki za watu wa Palestina ikiwa ni pamoja na kuinua hadhi ya Palestina katika Umoja wa Mataifa.
Aghalabu ya nchi za dunia zinaunga mkono kuundwa nchi huru ya Palestina mji wake mkuu ukiwa ni Quds Tukufu na kuna uwezekano kuwa mwaka huu wa 2017 nchi huru ya Palestina itaundwa
Mchakato huu umeutia wasi wasi utawala haramu wa Israel na ndio sababu wakuu wa utawala huo wameanza kutoa matamshi dhidi ya Umoja wa Mataifa kutokana na sisitizo la umoja huo kuhusu ulazima wa utawala huo wa Kizayuni kusitisha ukaliaji mabavu ili taifa huru la Palestina liundwe.