Wednesday, June 13, 2018

MGOGORO WA KIDIPIOMASIA KATI YA KENYA NA UGANDA WANUKIA TENA

Mgogoro mwingine wa kidiplomasia kati ya Kenya na Uganda unanukia. Hii ni baada ya makumi ya wahamiaji haramu raia wa Uganda kukamatwa na maafisa wa polisi wa Kenya katika mpaka wa nchi mbili hizo.
Wambua Katiithi, Kamanda Mkuu wa Polisi katika mji wa Bumula, kaunti ya Busia amesema wahajiri haramu 53 wa Uganda wamekatwa wakiwa hawana vyeti vinavyohitajika vya usafiri, wakiwa njiani kuelekea mjini Nairobi kwa kutumia usafiri wa basi.
Tukio hilo lilifanyika hapo jana, ikiwa ni chini ya masaa 24 baada ya polisi ya Uganda kuwatia mbaroni askari polisi watatu wa Kenya na wavuvi kadhaa kati ya visiwa vya Mageta na Hama katika Ziwa Victoria.
Kenya na Uganda zimekuwa zikivutana kwa miaka kadhaa sasa kuhusu masuala kadha wa kadha na haswa umiliki wa kisiwa cha Migingo, kilichoko katika mpaka wa nchi mbili hizo za Afrika Mashariki.
Kisiwa cha Migingo kinachozozaniwa na Kenya na Uganda
Mwaka jana, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alisema kisiwa cha Migingo katika Ziwa Victoria ni milki ya Kenya.
Mgogoro wa kisiwa cha Migingo ulianza mwaka 2008 baada ya wanajeshi wa Uganda kukivamia na kuwatimua Wakenya ingawa kimekuwa kikitambuliwa kuwa ni milki ya Kenya.
Makubaliano ya awali kati ya Kenya na Uganda kuhusu kisiwa hiki yalifanyika 2016, na kwa sasa maafisa wa usalama kutoka nchi zote mbili wanalinda doria katika kisiwa hicho.

Tuesday, June 12, 2018

TRUMP NA KIM WATIA SAINI MAKUBALIANO YA KIHISTORIA

Rais wa Marekani Donald Trump na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un wamekubaliana kuondoa kabisa silaha za kinyuklia katika  rasi ya Korea katika makubaliano ya  pamoja  ya kihistoria.

     Singapore Summit Donald Trump Kim Jong Un Unterzeichnung (Reuters/J. Ernst)
Viongozi  hao  walikamilisha siku ya kihistoria ambayo ilishuhudia viongozi hao wawili wakikutana kwa  mara  ya  kwanza kabisa.
Katika  mkutano  huo Trump  ameahidi  kuipatia  Korea  kaskazini  uhakikisho  wa  usalama wake  pamoja  na  kutangaza  katika  mkutano  na  waandishi  habari baadaye  kwamba  Marekani  na  Korea  kusini  zitaacha  luteka  ya pamoja  ya  kijeshi kama Korea kaskazini  inavyodai.
Singapur Gipfel Kim Jong Un Donald Trump (Reuters/A. Wallace)
Kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un (kushoto) na rais wa Marekani Donald Trump wakipeana mikoni
Katika  waraka  wenye vipengee  vinne, Marekani  na  Korea kaskazini  zimeazimia  kuweka  uhusiano  mpya  kati  ya  nchi  hizo mbili, kujenga   utawala  imara  na  endelevu  kuelekea  amani akisisitiza  azimio  la  Panmunjeom  kutoka  Aprili  27.
Katika  mkutano  na  waandishi  habari leo rais  Donald Trump  wa Marekani  amesema  kwamba  jeshi  la  Marekani  litaacha  kufanya mazowezi  ya  pamoja  na  Korea  kusini  yakiilenga  Korea kaskazini, akisema  yanaongeza  hali  ya  wasi  wasi na  kuyasitisha kutasaidia  kuhifadhi  fedha  nyingi  zinazotumika  katika  mazowezi hayo. Pia  amesema  atamwalika  kiongozi  wa  Korea  kaskazini katika  ikulu  ya  marekani White house na  kwamba   binafsi angependa  kutembelea  mji mkuu  wa  Korea  kaskazini  Pyongyang.
Nchi  hizo  mbili  hufanya  mazowezi  ya  kijeshi  kila  mwaka  ambayo yanaikera  Korea  kaskazini , ambayo  imekuwa  kwa  muda  mrefu ikidai kusitishwa  kwa  mazowezi  hayo na  mara  nyingi  hujibu  kwa kuchukua  hatua  zake, na  kusababisha  kuongezeka  kwa  hali  ya wasi  wasi. 
Singapur - Präsident Donald Trump gemeinsam Unterschriebenes Dokument nach Treffen mit Kim Jong Un (Reuters/J. Ernst)
Rais Trump akionesha waraka uliotiwa saini baina yake na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un
Kim amshukuru  Trump
Wakati  wa  kutia  saini  makubaliano  hayo  kati  ya Trump  na  Kim leo  asubuhi, rais  Trump  alisema  pande  zote  mbili zimefurahi  kutia  saini  makubaliano  hayo.
"Tunatia  saini  waraka  muhimu  sana, waraka  ambao una maelezo mapana. na  tutajadili  hili  kwa  kina. Kwa  hivi  sasa naamini  mtapata nakala kwa  niaba  ya  mwenyekiti Kim  na mimi. Na wote tunafahari  kubwa  kutia  saini  waraka  huu. Asante."
Kwa  upande  wake  kiongozi  wa  Korea  kaskazini  Kim Jong Un alimshukuru  rais  Trump  kwa  kukubali  kufanyika  mkutano  huo.
"Leo tulikuwa  na  mkutano  wa  kihistoria  na  kuamua  kuacha nyuma  yaliyopita. Na  tuko  tayari  kutia  saini  waraka  huu  wa kihistoria. Dunia  itaona  mabadiliko  makubwa. Napenda kueleza  shukurani  zangu  kwa  rais Trump  kwa  kufanikisha mkutano  huu. Asante.
Kuhusu  vikwazo  dhidi  ya  Korea  kaskazini  rais  Trump  amesema kwa  hivi  sasa  vikwazo  hivyo  vitaendelea , lakini  anaangalia uwezekano  wa  kuviondoa.
Donald Trump Pressekonferenz Singapur (Reuters/J. Ernst)
Rais Trump akiwa katika mkutano na waandishi habari baada ya kutia saini makubaliano na kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong Un
Rais  wa  Marekani  amesema  pia  kwamba  kiongozi  wa  Korea kaskazini  Kim Jong Un ana  nia  thabiti  ya  kuharibu  kabisa maeneo  ambayo  nchi  hiyo  inafanyia  majaribio  silaha  zake.
Kwa  upande  mwingine waziri  mkuu  wa  Japan  Shinzo  Abe  na mwenzake  wa  Malaysia  mahathir Mohammed wamekubaliana  leo kufanyakazi  kwa  pamoja  kupambana  na  mipango  ya  kinyuklia  na makombora  ya  Korea  kaskazini. Viongozi  hao  wamesema wanataka  kutuma  ujumbe  mkali  kwa  Korea  kaskazini  kuhusu suala  hilo.  Waliysema  hayo  katika  mkutano  na  waandishi  habari kufuatia  mkutano  wao  mjini  Tokyo

MAGAZETI YA UJERUMANI YAMKOSOA TRUMP, YAMWITA "MPUMBAVU"

Magazeti ya Ujerumani yamemtaja Rais Donald Trump wa Marekani kuwa ni mtu asiyejua mipaka yake wala asiye na mantiki na yamezitaka nchi zote za Ulaya kuacha kumfuata kiongozi huyo.
Gazeti la Ujerumani la Süddeutsche Zeitung limeripoti kuwa, kila mtu aliyekuwa anaamini kuwa Rais wa Marekani ni mtu mwenye mantiki na anayetilia maanani uhakika wa mambo anapaswa kuzika matumaini hayo kwa sababu kuwepo kwa mtu huyo asiye na adabu na mbumbavu hakuifanyi dunia kuwa sehemu bora na yenye amani zaidi.
Gazeti hilo la Ujerumani limeongeza kuwa: Trump anaendelea kuzitishia nchi nyingine kwa kutumia mabavu na silaha ya uchumi, na suala hilo ni hatari sana kwa Ujerumani.
Trump na Macron
Süddeutsche Zeitung limeandika kuwa: Nchi za Magharibi zimekumbwa na mgawanyiko katika masuala ya kisiasa na uhakika huo umeonekana waziwazi katika mkutano wa viongozi wa nchi 7 zilizopiga hatua kiviwanda wa G7 huko Canada ambao kimsingi ulibadilika na kuwa G6. 
Rais Donald Trump wa Marekani siku chache zilizopita aliwaacha bumbuazi viongozi wengine wa G7 katika mkutano wa Canada baada ya kuondoka ghafla katika mkutano huo na kufuta saini yake katika hati ya mwisho ya mkutano huo. 

WITO WA MSHIKAMANO WA NCHI ZA ULAYA KATIKA KUKUBALIANA NA MAREKANI

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amebainisha masiktiko yake baada ya Rais Donald Trump wa Marekani kukataa kuidhinisha taarifa ya mwisho ya kikao cha viongozi wa nchi tajiri kiviwanda G7 ambacho kilimalizika juzi huko Quebec, nchini Canada. Merkel amebainisha wazi kuwa nchi za Ulaya hazipaswi kuitegemea tena Marekani.
Naye Heiko Maas Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani amesisitiza kuwa, jibu la  Ulaya kuhusu uamuzi huo wa Trump linapaswa kuwa ni mshikamano na ukuruba zaidi katika Umoja wa Ulaya.
Mass ameongeza kuwa uamuzi wa Trump wa kutoafiki taarifa ya mwisho ya kikao cha G7 haukuzishangaza sana nchi shiriki kwani Trump amekiuka mapatano mengine muhimu ya utunzaji mazingira  na mapatano ya nyuklia ya Iran.
Baada ya mkutano wa viongozi wa kundi la G7, kumedhihirika hitilafu kubwa na za wazi baina ya Rais Trump na viongozi wa Canada, Ufaransa na Ujerumani. Trump aliondoka mapema kabla ya kikao hicho kumalizika kama ishara ya kubainisha kuchukizwa kwake na tamko la Waziri Mkuu wa Canada Justin Trudeau na kusema hataunga mkono taarifa ya mwisho ya kikao hicho. Uamuzi huo wa Trump umetajwa kuwa ni pigo kubwa kwa kundi la G7 ambalo linajumuisha  Marekani, Canada, Ujerumani, Uingereza,Ufaransa, Italia na Japan.

Trump amejiondoa katika mapatano ya kulinda mazingira duniani ya Paris 

Hatua hiyo ya Trump itatoa pigo kubwa kwa ushirikiano wa pande mbili za Bahari ya Atlantiki na pia ni pigo kubwa kwa uhusiano wa kistratijia wa Canadan na Marekani. Kwa hatua yake hiyo, Trump analenga kung'oa mizizi ya uhusiano na mshikamano wa miongo kadhaa wa kiuchumi, kibiashara, na kiusalama baina ya Marekani na Ulaya. Wakuu wa Ulaya wanajaribu kuzuia hali ya mambo kuwa mbaya zaidi na wanasema hatua ya Trump kutosaini taarifa ya mwisho haimaanishi kila kitu kimekwisha. Kuhusiana na hili, Angela Merkel amesema: "Hatua ya Trump kutangaza kuwa hatatia saini taarifa ya mwisho ya G7 kupitia Twitter ni jambo la kusikitisha. Ameongeza kuwa, 'kikao cha viongozi wa G7 huko Canada hakikuwa mwisho wa ushirikiano wa Ulaya na Marekani lakini akaongeza kuwa, nchi za Ulaya hazipaswi kuitegemea tena Marekani na zinapaswa zenyewe zijiamulie  hatima yao.'
Ingawa suala la Marekani kujiondoa G7 halijapewa uzito mkubwa lakini kwa kuzingatia utendaji kazi wa Trump katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu wa urais wake, nchi zingine sita za kundi la G7 hazitashangaa iwapo Trump ataendeleza mwenendo wake huo wa kupuuza na kubatilisha mikataba ya kimataifa, na hivyo aamue kujiondoa katika kundi hilo. Kwa hivyo nchi hizo sita zinajitayarisha kwa hali kama hiyo.
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa anasema hivi kuhusu suala hilo:"Pengine Trump hajali iwapo atatengwa lakini hata tukibadilika na kuwa kundi la  G6 bado tutakuwa nguvu kubwa. Iwapo Trump ataamua kuiondoa Marekani katika nafasi yake duniani, jambo hilo litakuwa na matokeo hasi kwa uchumi na hadhi ya Marekani duniani. Trump anafahamu hili."

Trump amejiondoa katika maptano ya nyuklia ya Iran maarufu kama JCPOA

Mtazamo wa Trump kuhusu masuala ambayo yamepelekea kuibuka hitilafu baina ya Marekani na Ulaya ni jimbo linaloonyesha kuwa hana nia ya kulegeza msimamo wake bali hata ametoa vitisho kwa kwa nchi za Ulaya na Canada hasa katika masuala ya kibiashara. Trump ameongeza kwa kiwango kikubwa ushuru wa bidhaa zinazoingizwa Marekani kutoka Ulaya, Canada na Mexico hasa bidhaa za chuma.
Hatua hizo za Trump zimepelekea kuongezeka hitilafu kubwa baina ya Marekani na nchi hizo na kuwepo hatari ya kuibuka vita vya kibiashara kati ya Marekani na nchi hizo. Hali kadhalika nchi za Ulaya pia zimekasirishwa na hatua ya Trump ya kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya Iran maarufu kama JCPOA na mapatano mengine muhimu ya mazingira maarufu kama Mapatano ya Tabianchi ya Paris.
Kwa mtazamo wa nchi muhimu katika Umoja wa Ulaya, si tu kuwa sera za Trump zitaidhuru dunia bali zitapelekea kutengwa zaidi Marekani katika uga wa kimataifa.

Sunday, May 27, 2018

WATU 30 WAUAWA KATIKA MAPIGANO MASHARIKI MWA KONGO DR

Watu 30 wameuawa katika mapigano kati ya jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na wanamgambo wa Mai-Mai mashariki mwa nchi hiyo.
Duru za eneo hilo zimeripoti kuwa katika mapigano hayo yaliyotokea jana na kuendelea kwa saa kadhaa wanajeshi 18 waliuawa akiwemo afisa mmoja na kamanda wa polisi wa polisi wa eneo hilo.
Kwa mujibu wa duru hizo, wanamgambo wanane waliohusika katika hujuma hiyo pamoja na raia watatu pia waliuawa katika mapigano hayo. Raia hao waliuliwa kwa risasi walipokuwa wakikimbia mapigano.


Mnamo siku ya Alkhamisi iliyopita, wanamgambo wa kundi la Mai-Mai walilidhibiti eneo lenye utajiri wa madini la Salamambila mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, lakini wakalazimika kuliacha na kukimbia baada ya vikosi vya jeshi la serikali kufika katika eneo hilo.
Wanamgambo wa Mai-Mai wanatokana na makundi ya wabeba silaha waliopata mafunzo ya kijeshi katika eneo la mashariki mwa Kongo DR ambalo limekuwa uwanja wa mapigano kwa zaidi ya miaka 20 sasa.../

RAIS ROUHSNI: HATUA ZILIZOCHUKULIWA HADI SASA NI CHANYA KWA AJILI YA KUENDELEZA JCPOA

Rais Hassan Rouhani amesema, baada ya Marekani kujitoa kwenye makubaliano ya JCPOA waliowengi katika jamii ya kimataifa wameipa haki Iran na kuyatetea makubaliano hayo na kuongeza kwamba hatua zilizochukuliwa hadi sasa ni nzuri kwa ajili ya kuendeleza makubaliano hayo ya nyuklia.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyaeleza hayo mbele ya hadhara ya maulamaa na wanazuoni wa mjini Tehran na kubainisha kuwa: Leo akthari ya nchi zinaitakidi kuwa njia iliyofuata Iran ilikuwa sahihi na Marekani ndio iliyofanya makosa, na hayo ni mafanikio makubwa.
Rais Rouhani amefafanua kuwa Marekani inatoa mashinikizo kwa nchi za Ulaya kwamba zichague kati ya Marekani na Iran lakini nchi hizo zinasema 'sisi tunachagua makubaliano ya JCPOA'.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa msingi inaofungamana nao Iran ni kwamba kama itaweza kupata haki zake kwa kubaki kwenye makubaliano ya JCPOA itaendelea kufungamana na makubaliano hayo ya kimataifa.
Rais Hassan akihutubia hadhara ya maulamaa
Ikumbukwe kuwa, Rais Donald Trump wa Marekani alitangaza Mei 8 kuwa nchi yake imejiondoa katika mapatano hayo ya nyuklia ya Iran ambayo rasmi yanajulikana kama JCPOA. Trump aidha alisema ataiwekea Jamhuri ya Kiislamu vikwazo vya nyuklia katika kipindi cha miezi mitatu hadi sita ijayo.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza kusikitishwa mno na uamuzi huo wa upande mmoja uliochukuliwa na rais wa Marekani.
Hii ni katika hali ambayo nchi zilizosalia katika JCPOA, yaani Uingereza, Ufaransa, Russia, China, Ujerumani na Umoja wa Ulaya, zimesisitiza kuwa zitandelea kuunga mkono mapatano hayo.
Wakati huohuo katika siku za karibuni Iran na nchi za Ulaya zimefanya mazungumzo kadhaa kwa lengo la kuyaendeleza makubaliano ya JCPOA baada ya Washington kujiondoa kwenye makubaliano hayo ya kimataifa.
Inafaa kukumbusha pia kuwa mnamo siku ya Jumatano iliyopita Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Khamenei alibainisha masharti ya Iran kuendelea kubakia katika JCPOA na kusisitiza kuwa: "Nchi za Ulaya zinapaswa kuwasilisha azimio dhidi ya Marekani katika Baraza la Usalama, ziahidi pia kuwa kadhia za makombora na ushawishi wa Iran katika eneo hazitajadiliwa na pia zikabiliane na vikwazo vyovyote vya Marekani dhidi ya Iran." Aidha Kiongozi Muadhamu aliongeza kuwa nchi za Ulaya zinapaswa kutoa dhamana ya kununua mafuta ya Iran kwa kiwango ambacho Iran inahitaji na pia benki za Ulaya zinapaswa kutoa dhamana ya kutekeleza malipo ya kifedha kwa ajili ya biashara na serikali pamoja na sekta binafsi ya  Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.../

BAYTU ZAKAT YA KUWAIT YAZINDUA PROGRAMU YA DOLA 26400 KWA AJILI YA KUFUTURISHA KATIKA MWEZI WA RAMADHAN NCHINI TANZANIA


 Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Mhe. Jasem Al-Najem anashiriki katika utekelezaji wa programu ya kufuturisha ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan ambayo inafadhiliwa na Chombo cha Baytu Zakat, Wakfu na Mali ya Amana ya Kuwait. Programu kama hii huandaliwa kila mwaka kutoka kwa wasamaria wa nchi ya Kuwait.  
Programu hii thamani yake ni dola elfu 26 na mia nne sawa na shilingi milioni 60.
Awamu ya kwanza ya programu hii ilikuwa ni kugawa vikapu 400 vyenye vyakula kama mchele, sukari,unga,mafuta ya kula, tende na sukari ambapo katika moja ya zoezi la ugawaji alihudhuria Mkuu wa Wilaya ya Ilala. Bi Sophia Mjema.
Ubalozi wa Kuwait umedhamiria mwaka huu kuwasilisha misaada ya futari katika miji, vitongoji, kata, mitaa, vijiji na maeneo ya mbali kote Tanzania ambapo hadi sasa mikoa ya Tanga, Iringa, Dar es salaam na visiwa vya Zanzibar imefaidika na misaada hiyo ambayo Ubalozi hushirikiana na asasi zisizokuwa za kiserikali za Tanzania katika kuwafikia walengwa.







Monday, May 21, 2018

KIMBUNGA CHA KITROPIKI CHAIKUMBA SOMALILAND; WATU WASIOPUNGUA 15B WAAGA DUNIA

Watu wasiopungua 15 wameaga dunia huko Somaliland baada ya mvua kubwa zilizosababishwa na kimbunga cha kitropiki kwa jina la Sagar kuiathiri nchi hiyo ya Pembe ya Afrika mwishoni mwa wiki.
Somaliland ilijitenga  na Somalia mwaka 1991. Abdirahman Ahmed Ali Gavana wa eneo la Awdal amesema kuwa mvua kubwa zilizonyesha katika muda wa masaa 24 yaliyopita zimeua watu 16 katika wilaya za Lughaya na Baki. Serikali ya Somaliland tayari imeanza kutoa misaada ya dharura kwa wahanga wa kimbunga hicho. Wakati huo huo upepo mkali uliosababishwa na kimbunga cha Sagar umewasomba wanaume wawili pamoja na gari yao huko katika mji wa Bosaso katika eneo la Puntland, huko kaskazini mashariki mwa Somalia. Hayo yameelezwa na Yusuf Mohamed Waeys Gavana wa Bari katika eneo la Puntland.
Wakati huo huo Ofisi ya Umoja wa Mataifa Inayohusika na Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu imesema kuwa maelfu ya watu wameathirika na mafuriko hayo, wamepoteza makazi na miundo mbinu kuharibiwa huko Puntland.   
Kimbunga cha kitropiki cha Sagar kilivyoiathiri Somaliland

Saturday, May 19, 2018

WATUWATATU TU WAMENUSURIKA KATIKA AJALI YA NDEGE ILIYOKUWA IMEBEBA WATU 110 NCHINI CUBA

Watu watatu tu wameripotiwa kunusurika katika ajali ya ndege iliyochakaa aina ya Boeing 737 ambayo ilianguka hapo jana muda mfupi baada ya kuruka katika uwanja wa ndege wa Havana nchini Cuba huku wachunguzi wakijaribu kubaini chanzo cha ajali hiyo kupitia mabaki ya ndege hiyo.
Kwa mujibu wa televisheni ya taifa ya Cuba hali ya hewa ilikuwa ya mawingu na mvua ilikuwa inanyesha wakati ndege hiyo ambayo imeshatumika kwa muda wa miaka 39 ilipoanguka ikiwa katika safari za ndani kuelekea mji wa Holguin mashariki mwa nchi hiyo.
Rais Miguel Diaz-Canel wa Cuba amesema tume maalumu imeundwa kuchunguza chanzo cha ajali hiyo.
Rais Miguel Diaz-Canel wa Cuba (katikati ya askari na raia) alipokagua tukio la ajali
Ndege hiyo ilikuwa imebeba abiria 104, akthari yao wakiwa ni Wacuba pamoja na wahudumu sita.
Abiria wanne walionusurika walipelekwa hospitali ya Havana, ambapo hadi kufikia jana usiku watatu miongoni mwao walikuwa wangali hai.
Ajali hiyo ya jana ya ndege imetajwa kuwa mbaya zaidi kuwahi kutokea nchini Cuba katika kipindi cha miongo mitatu iliyopita na ya tatu kwa ukubwa kutokea duniani tangu mwaka 2010.../

RAIS RTUMP WA MAREKANI AWATUSI TENA WAHIJIRI KWA KUWAITA KUWA NI WANYAMA

Rais Donald Trump wa Marekani kwa mara nyingine ametoa matamshi mabaya yenye kuwavunjia heshima wahajiri au wahamiaji nchini humo kwa kuwataja kuwa ni wanyama.
Matamshi hayo ya Trump si ya kwanza ya aina yake kwani miezi kadhaa iliyopita katika kikao chake na wajumbe wa vyama vya Democrat na Republican katika Ikulu ya White House aliashiria kuhusu wahajiri kutoka Haiti, El Salvador na baadhi ya nchi za Afrika na kuzitaja kuwa sawa na shimo la kinyesi.
Matamshi hayo ya mara kwa mara ya Trump ya kuwavunjia heshima wahamiaji hasa wenye asili ya Afrika yamekosolewa na wajumbe wa chama cha upinzani cha Democrat ambao wanasema ni ishara ya wazi kuwa mtawala huyo ni mbaguzi wa rangi.
Ikulu ya White House ilijaribiu kuonyuesha kuwa matamshi hayo yalitokana na hisia za kitaifa za rais huyo, lakini baada ya kuendelea malalamikio kuhusu matamshi hayo ya kishenzi ya Trump, rais huyo akiwa katika mkutano na Katibu Mkuu wa Shirika la Kijeshi la Nato, katika kujaribu kutetea matusi yake kuhusu wahajiri wanaoingia nchini humo kinyume cha sheria, amesema wakati alipowahutubu kwa kuwaita kuwa ni 'Wanyama' siku ya Jumatano, alikusudia genge la wahalifu linalojulikana kama  'MS 13'.
Matamshi hayo ya Trump kuhusu wahajiri ambayo aliyatoa wakati wa mkutano wake na wakuu wa jimbo la California, yamekosolewa vikali na wajumbe wa Bunge la Kongresi.
Mtu mwenye asili ya Afrika akikandamizwa nchini Marekani
Aghalabu ya wajumbe wa Kongresi wanaamini kuwa matamshi hayo yasiyokubalika hata kidogo ya Trump, yanaonyesha wazi kuwa hawajibiki na ni mchochezi.
Matamshi hayo ya Trump ya kuwavunjia heshima na kuwadhalilisha wahajiri yameandamana na hatua za kivitendo za kuwatenganisha watoto wahajiri na wazazi wao.
Hali kadhalika Trump amewawekea Waislamu vizingiti kuingia Marekani sambamba na hatua zingine nyingi za kibaguzi. Hatua hizo za Trump zinalenga kuwashinikiza wahajiri na wahamiaji ili kuwazuia wasiingie Marekani.
Matamshi ya kibaguzi ya rais wa Marekani ni chanzo cha wasiwasi na hofu katika jamii ya Marekani hasa miongoni mwa wasomi nchini humo ambao wanaamini kuwa matamshi hayo yasiyofaa hata kidogo yataharibu itibari iliyobakia ya nchi hiyo duniani.
Rupert Colville, Msemaji wa Ofisi ya Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa anasema matamshi ya Trump ni ya kushtua na ya kuaibisha.
Ikulu ya White House na hata Donald Trump mwenyewe wamejaribu kukanusha matamshi hayo ya kibaguzi, lakini ukweli usioweza kupingika ni huu kuwa, ubaguzi wa rangi ni sehemu ya utambulisho wa wazi wa utawala wa Rais Trump na Ikulu ya White House.

Tuesday, April 17, 2018

MAHAKIMU ZAIDI YA 250 WAFUTWA KAZI JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA CONGO

Mahakimu zaidi ya 250 wafutwa kazi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imewafuta kazi zaidi ya mahakimu 250 kwa sababu mbalimbali ikiwemo ya ufisadi.
Waziri wa Sheria Alexis Thambwe Mwamba amesema kuwa, mahakimu hao wamefutwa kazi kwa sababu za ufisadi na wengine kutokuwa na elimu ya taaluma hiyo.
Waziri thambwe amebainisha kuwa, hatua hii imechukuliwa ili kuwazuia watu waliokuwa wakiingia katika idara ya mahakama wakiwa na lengo la kujipatia fedha badala ya kuwatumikia raia wa nchi hiyo.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, idadi kamili ya mahakimu waliofutwa kazi na serikali ni 256 na kwamba, sababu kuu ni majaji hao kujihusisha na vitendo vya kupokea rushwa, kutokuwa na elimu ya taaluma hiyo na kundi la tatu limestaafishwa.
Alexis Thambwe Mwamba, Waziri wa Sheria wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Hii sio mara ya kwanza kwa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Kinshasa kuwachukulia hatua maafisa wa juu wa idara ya Mahakama. Mwaka 2009, Rais Joseph Kabila aliwafuta kazi majaji 96 baada ya kubainika kuwa walikuwa wakijihusha na vitendo vya ufisadi.
Hatua hiyo ya kufutwa kazi majaji hao inakuja kukiwa kumesalia miezi 7 kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu katika nchi hiyo inayokabiliwa na changamoto kubwa ya usalama. 
Uchaguzi huo uliokuwa ufanyike mwishoni mwa mwaka jana ulisogezwa mbele na sasa unatarajiwa kufanyika Desemba 23, mwaka huu ili kumpata mrithi wa Rais Joseph Kabila, ambaye muhula wake wa uongozi ulimalizika Desemba 20, 2016.

Friday, April 13, 2018

MAGAIDI WA BOKO HARAM WAMEWATEKA WATOTO ZAIDI YA 1,000 TOKEA 2013

Magaidi wa Boko Haram wamewateka watoto zaidi ya 1,000 tokea 2013
Magaidi wakufurishaji wa kundi la Boko Haram nchini Nigeria wamewateka watoto zaidi ya 1,000 tokea mwaka 2013.
Hayo yamedokezwa katika ripoti mpya ya Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Watoto, UNICEF ambayo imetolewa kwa munasaba wa kutekwa wasichana 276 wa shule katika mji wa Chibok kaskazini mashariki mwa Nigeria. Wasichana hao walitekwa na magaidi wa kundi hilo la Kiwahhabi la Boko Haram.
Mkuu wa UNICEF nchini Nigeria Mohamed Malick Fall amesema watoto katika eneo la kaskazini mashariki mwa Nigeria wanaendelea kukabiliwa na mashambulizi ambayo yanashtua sana. UNICEF imesajili kesi zaidi ya 1,000 za watoto kutekwa nyara lakini imesema idadi hiyo huenda ikawa kubwa zaidi. Aidha shirika hilo la Umoja wa Mataifa limesema limemhoji msichana aliyewahi kutekwa na Boko Haram ambaye sasa ana umri wa miaka 17 ambaye amesema alinajisiwa na wapiganaji wa kundi hilo. Anasema alipata mimba baada ya tukio hilo la kusikitisha na sasa anakabiliwa na matatizo mengi katika kambi ya wakimbizi huku akikejeliwa kuwa  yeye ni 'mke wa wapiganaji wa Boko Haram'.
Katika usiku wa Aprili 14 kuamkia 15, magaidi wa Boko Haram waliwateka nyara wasichana 276 ambao wengi wameshaachiliwa lakini 100 bado hawajulikani waliko na kuna wasi wasi kuwa baadhi wameshafariki huku baadhi wakiwa wameamua kubakia huko walikotekwa nyara.
UNICEF inasema tokea uanze uasi wa magaidi wa Boko Haram nchini Nigeria, hadi sasa waalimu zaidi ya 2,295 wameuawa na shule 1,400 kubomolewa.
Neno Boko Haram kwa ya lugha ya Kihausa lina maana ya 'elimu kutoka nchi za Magharibi ni haramu'. Zaidi ya watu elfu 20 wamepoteza maisha nchini Nigeria tokea kundi la Boko Haram lianzishe uasi mwaka 2009 huku wengine zaidi ya milioni mbili wakilazimika kukimbia makazi yao kutokana na ugaidi wa Boko Haram ambao sasa umeenea katika nchi jirani kama vile Cameroon, Niger na Chad.
Boko Haram ni kundi lenye misimamo ya kufurutu mipaka nchini Nigeria ambalo kutokana na kuwa na ufahamu mbaya na potofu kuhusiana na Uislamu, limeitumbukiza nchi hiyo katika dimbwi la machafuko na mauaji sambamba na kuzusha hitilafu za kidini na kikabila nchini humo.

DRC YASUSIA MKUTANO WA UMOJA WA MATAIFA WA KUKUSANYA FEDHA ZA KUWASAIDIA RAIA WA NCHI HIYO

 DRC yasusia mkutano wa Umoja wa Mataifa wa kukusanya fedha za kuwasaidia raia wa nchi hiyo
Mkutano maalumu uliotishwa na Umoja wa Mataifa umeanza leo mjini Geneva Uswisi kwa kuchangisha fedha za kukabiliana na janga la kibinaadamu katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo huku serikali ya Kinshasa ikiususia mkutano huo.
Mashirika ya misaada yanasema kuwa, zaidi ya watu milioni 5 wamelazimika kuyakimbia makazi yao katika Jamhuri ya Kidemokrasia yya Congo kwa sababu ya mapigano katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo.
Aidha mkutano huo  wa wafadhili umeanza leo huku takwimu za Umoja wa Mataifa zikionesha kwamba, watu milioni 13 wanahitaji msaada huku thuluthi moja kati yao wakiwa  ni wakimbizi wa ndani  ambao wanahitaji msaada wa dharura wa kibinadamu mwaka huu.
Wafadhili hao wa kimataifa wanatafuta  kiasi cha dola bilioni 1.7 kuwasaidia watu hao wanaohitaji dawa, chakula na makazi mazuri.
Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Hata hivyo, serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imesusia mkutano huo, ikiyashutumu mashirika ya kiraia kwa kutoa takwimu za uongo na kulichafulia jina taifa hilo.
Uamuzi huo wa serikali ya Kinshasa wa kususia mkutano huo umekosolewa, huku baadhi ya wakosoaji wakisema kwamba, serikali yya Kinshasa ingeshiriki tu katika mkutano huo ili kuwashajiisha wafadhili watoe misaada kwani wanaoumia ni raia.
Hayo yanajiri katika hali ya ambayo, hivi karibuni Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa  lilionya kuwa, hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imeendelea kuwa mbaya na imefikia hatua ya kuwa janga kwenye baadhi ya maeneo ya nchi hiyo, huku mamilioni ya watu wakikabiliwa na njaa.

AYATULLAH AKHTARI: MAWAHABI WANAPIGWA NA WANAZUONI NA MATAIFA YA KIISLAMU

Ayatullah Akhtari: Mawahabi wanapingwa na wanazuoni na mataifa ya Kiislamu
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimatataifa ya Ahlul-Beit (AS) amesisitiza kuwa, utawala wa Aal Saud hauna nafasi yoyote si ya kielimu wala uungaji mkono wa wananchi na kwamba, akthari ya wanazuoni wa Kiislamu wanawapinga Mawahabi wa Saudi Arabia.
Ayatullah Muhammad Hassan Akhtari amesema hayo akiwa nchini Syria na kubainisha kwamba, Maulama waliowengi wa Kiislamu na mataifa ya Kiislamu wanachukia Uwahabi ulioletwa na Aal Saud.
Ayatullah Akhtari ameongeza kuwa, aidiolojia ya uchupaji mipaka ya Uwahabi ambayo inaenezwa na kuungwa mkono na Saudi Arabia imepelekea kutokea magaidi ambao wamekuwa wakifanya mashambulio ya kigaidi katika maeneo mbalimbali ulimwenguni.
Katibu Mkuu wa Jumuiya yay Kimataifa ya Ahlul-Beit (AS) amesema Saudia inataka kulinda nafasi yake kupitia kuzusha hitilafu na mifarakano pamoja na kutekeleza mauaji dhidi ya raia wasio na hatia.
Uwahabi
Aidha ameashiria juhudi za utawala wa Saudi Arabia za kutaka kuwa na uhusiano wa kawaida na utawala haramu wa Israel na kusema kuwa, hatua hiyo ya utawala wa Riyadh inalenga kuulinda na kuuhifadhi utawala huo, hata hivyo jambo hilo linalaaniwa na Waislamu ulimwenguni.
Kadhalika Katibu Mkuu wa Jumuiya yay Kimataifa ya Ahlul-Beit (AS) amesema kuwa, Saudia imeamua kuuunga mkono utawala dhalimu wa Israel ili kuifurahisha Marekani.
Ayatullah Akhtari ameashiria pia kwamba, watawala wa Saudia wamebomoa athari nyingi za Kiislamu katika miji mitakatifu ya Makka na Madina na kuongeza kwamba, wanachofuatilia Aal Saud ni kuzusha fitina na mifarakano miongoni mwa Waislamu.

Thursday, April 12, 2018

WANARIADHA 13 WA AFRIKA ' WATOWEKA' AUSTRALIA

Wanariadha 13 wa Afrika 'watoweka' Australia
Wanariadha 13 wa Afrika walioenda kushiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola nchini Australia wametoweka katika mazingira ya kutatanisha.
David Grevemberg, Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirikisho la Michezo ya Jumuiya ya Madola amewaambia waandishi wa habari leo Alkhamisi mjini Gold Coast kunakofanyika mashindano hayo kuwa: "Wanariadha wengine watano raia wa Rwanda, Uganda na Sierra Leone wametoweka na kwenda kusikojulikana."
Ameongeza kuwa, hii ni baada ya wanariadha wengine wanane kutoka Cameroon kutoweka hapo awali, na sasa idadi hiyo ya wanaichezo wa Kiafrika waliotoweka katika mazingira ya kutatanisha nchini humo imefikia 13.
Serikali ya Australia imetoa viza kwa wanamichezo wanaoshiriki katika michezo hiyo, kuendelea kuwa nchini humo hadi tarehe 15 mwezi Mei. 
Wakimbizi kutoka nchi mbalimbali duniani huko Australia
Peter Dutton, Waziri wa Masuala ya Ndani ya Australia ameonya kuwa, mwanariadha yeyote atakayebaki nchini humo kinyume cha sheria baada ya muda wake wa viza kumalizika, atafurushwa nchini humo kwa nguvu.
Ni vyema kukumbusha hapa kuwa, mwaka 2000 wakati wa mashindano mengine ya Jumuiya ya Madola jijini Sydney, wanaridha zaidi ya 100 waliendelea kuishi katika jiji hilo hata baada ya kumalizika kwa michezo hiyo.

KREMLIN YAJIBU TWITTER YA TRUMP: MAKOMBORA EREVU YANAPASWA KUELEKEZWA KWA MAGAIDI, SI KWA SERIKALI HALALI

Kremlin yajibu Twitter ya Trump: Makombora erevu yanapaswa kuelekezwa kwa magaidi, si kwa serikali halali
Msemaji wa Ikulu ya Rais wa Russia, Kremlin amesema Moscow Russia haishiriki katika udiplomasia wa Twitter.
Dimitri Peskov ameyasema hayo akijibu ujumbe ulioandikwa na Rais Donald Trump wa Marekani katika mtandao wa kijamii wa Twitter ambaye ameitahadharisha Russia kwamba isubiri makombora ya Marekani huko Syria.  
Peskov amesema kuwa, Russia inaunga mkono hatua madhubuti na inaamini kuwa ni muhimu kujiepusha na hatua yoyote inayoweza kuchafua zaidi hali iliyopo hivi sasa.
Mapema leo Rais Donald Trump wa Marekani aliimbia Russia kupitia mtandao wa Twitter kwamba ijitayarishe kwa mashambulizi ya makombora "mazuri, mapya na erevu" huko Syria. Marekani inadai serikali ya Syria imetumia silaha za gesi ya sumu katika eneo la Douma huko Ghuta Mashariki, suala linalokadhibishwa na Syria na Russia. 
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya kigeni ya Russia, Maria Zakharova pia amejibu matamshi hayo akisema: Mashambulizi erevu yanapaswa kuelekezwa kwa magaidi ni si kwa serikali halali ya Syria.
Image Caption
Russia pia imesema kuwa itayatungua makombora yote ya Marekani yatakayopigwa kueleka Syria na kwamba itapiga mahala yatakakotokea.

Monday, April 9, 2018

ARAB LEAGUE YALAANI JINAI ZA KARIBUNI ZA UTAWALA WA KIZAYUMI DHIDI YA WAPALESTINA

Arab League yalaani jinai za karibuni za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League) amelaani jinai za wanajeshi wa utawala wa Kizayuni dhidi ya raia wa Palestina.
Ahmad Abul Ghait amelaani jinai za utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Ghaza na kulitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutekeleza majukumu yake katika kuwalinda raia wa Palestina mbele ya jinai za utawala wa Israel. 
Ahmad Abul Gheit, Katibu Mkuu wa Arab League
Mahmoud Afifi, msemaji wa Katibu Mkuu wa Arab League pia jana alitahadharisha kuhusu kuendelea jinai hizo za utawala wa Kizayuni huko Ghaza na kueleza kuwa hali ya mambo katika eneo hilo inahitajia uingiliaji wa jamii ya kimataifa. Afifi alisisitiza kuwa wale wote waliohusika na jinai dhidi ya raia wa Palestina huko Ghaza inapasa wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria. 
Maelfu ya Wapalestina tarehe 30 mwezi uliopita wa Machi walifanya maandamano ya amani katika maadhimisho ya mwaka wa 42 wa "Siku ya Ardhi" kuelekea katika mpaka wa Ghaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu; ambapo waandamanaji hao walikabiliwa na hujuma na mashambulizi ya utawala wa Israel. Katika siku hiyo ya maandamano hayo ya amani chini ya anuani ya "Haki ya Kurejea", Wapalestina 17 waliuliwa shahidi na wengine zaidi ya 1400 walijeruhiwa. Tangu siku hiyo hadi sasa, Wapalestina wasiopungua 29 wameshauliwa shahidi kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa Israel na wengine zaidi ya 3000 wamejeruhiwa. Nchi nyingi na vile vile taasisi za kimataifa zimelaani jinai hizo za Wazayuni.

HATIMAYE SPIKA WA BUNGE LA SOMALIA AJIUZURU

Hatimaye Spika wa Bunge la Somalia ajiuzulu
Spika wa Bunge la Federali la Somalia, Mohamed Sheikh Osman Jawari, hatimaye amejiuzulu baada ya nchi hiyo ye Pembe ya Afrika kushuhudia taharuki na mgogoro mkubwa wa kisiasa kwa wiki kadhaa.
Dahir Amin Jesow, mmoja wa wabunge ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa, "Asubuhi ya leo tulikuwa tunajiandaa kujadili hoja ya kumuondoa madarakani Spika, mara ghafla Naibu Spika akaja na barua ya kujiuzulu Spika huyo na kuisoma mbele yetu. Tumepongeza hatua hiyo ya kujiuzulu ambayo inakubalika kikatiba, na tunatumai huu ndio mwisho wa mzozo wa kisiasa nchini." 
Wiki iliyopita, Rais Mohammed Abdullahi Farmajo wa Somalia alisimamisha kikao kingine cha Bunge kilichokusudia kujadili hoja hiyo ya kumuengua madarakani Spika wa bunge hilo.
Somalia imeshuhudia malumbano makali baina ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo Hassan Ali Khaire pamoja na kundi la wabunge wanaomuunga mkono kwa upande mmoja, na Spika wa Bunge la nchi hiyo ya Pembe ya Afrika kwa upande mwingine.
Image Caption
Mgogoro huo ulianza mapema mwezi jana, baada ya wabunge zaidi ya 100 wanaoegemea upande wa Waziri Mkuu, kuwasilisha hoja bungeni ya kutaka kuenguliwa madarakani Spika wa bunge, kwa madai kuwa amekuwa kizingiti kwenye shughuli za bunge hilo. 
Mohamed Osman Jawari, Spika wa Bunge la Somalia anatuhumiwa na wabunge kuwa anatumia vibaya madaraka yake na kuzuia kufanyiwa marekebisho katiba ya nchi hiyo. 

Sunday, April 8, 2018

RASMI ALIYEKUWA RAIS WA BRAZIL AJISALIMISHA TAYARI KUTUMUIKIA KIFUNGO

Rais wa zamani wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva amewasili katika jela la Curibita kuanza kutumikia kifungo cha miaka 12 jela.
Hatua hiyo ya kujisalimisha kwa polisi ameichukua baada ya mahakama siku ya Ijumaa kumhukumu kwa mashitaka ya ufisadi. Matangazo ya moja kwa moja ya vituo vya televisheni vya Brazil yameonesha akiwasili kwa helikopta katika makao makuu ya polisi katika mji wa Curibita ulioko kusini mwa Brazil.
Mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 72 aliondoka Sao Paoli akiwa amezingirwa na walinzi kwenye jengo la muungano wa wafuaji vyuma mjini humo. Alipenya katikati ya wafuasi wake waliokuwa wanamzuia asiondoke na kuingia katika gari la polisi. Anasisitiza kuwa mashitaka dhidi yake yalichochewa kisiasa. Lula alikutwa na hatia ya kupokea rushwa kutoka kwenye kampuni kubwa ya ujenzi, ili iweze kupata mikataba ya serikali.

UN: MYANMAR HAIPO TAYARI KUWAPOKEA WAKIMBIZI WAROHINGYA

UN: Myanmar haipo tayari kuwapokea wakimbizi Warohingya

Umoja wa Mataifa umesema Myanmar haipo tayari kuwapokea malaki ya wakimbizi Waislamu wa Rohingya wanaoishi kambini katika nchi jirani ya Bangladesh.

Ursula Mueller, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Kibinadamu ameyasema hayo baada ya kufanya ziara ya siku sita nchini Myanmar na kubainisha kuwa, mazingira yalivyo hivi sasa nchini humo hayaruhusu kurejea nyumbani wakimbizi wa Rohingya.

Amesema, "Kutokokana na kile nilichokishuhudia binafsi, hali mbaya ya kiafya, ukosefu wa dhamana ya usalama na kuendelea kufurushwa kwa wakimbizi wengine kutoka mkoani Rakhine ni miongoni mwa mambo yanayoonyesha kuwa Myanmar haijajiandaa kuwapokea Warohingya hao walioko Bangladesh.

Wakimbizi Waislamu wa Rohingya

Mwezi uliopita, Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa ilitahadharisha kuhusiana na kuendelea mauaji ya kizazi yanayofanywa na serikali ya Myanmar dhidi ya Waislamu wa jamii ya Rohingya magharibi mwa nchi hiyo, huku wakimbizi hao wakisisitiza watarejea nchini Myanmar kwa masharti mawili; mosi, wadhaminiwe usalama wao na pili wapewe uraia.

Mauaji hayo ya umati dhidi ya Waislamu nchini Myanmar tangu mwezi Agosti mwaka jana katika mkoa wa Rakhine magharibi mwa nchi, yamepelekea zaidi ya Waislamu laki saba kukimbilia hifadhi katika nchi jirani ya Bangladesh.

Thursday, April 5, 2018

JESHI LA YEMEN LASHAMBULIA TENA KWA KOMBORA SHIRIKA LA MAFUTA LA SAUDIA ARAMCO

Jeshi la Yemen lashambulia tena kwa kombora Shirika la Mafuta la Saudia Aramco
Kwa mara nyingine, jeshi la Yemen kwa kushirikiana na Harakati ya Kiislamu ya Answarullah, limeshambulia kwa kombora ghala la kuhifadhia mafuta la Shirika kubwa la Mafuta nchini Saudia Aramco katika mji wa Jizan, kusini magharibi mwa nchi hiyo.
Taarifa iliyotolewa na jeshi la Yemen imesema kuwa, kombora lililotumika kushambulia ghala hilo la mafuta ni aina ya Badr-1 na kwamba lilifyatuliwa jana usiku. Wakati huo huo duru za serikali ya Saudia zimedai kwamba, ngao ya kuzuia makombora ya nchi hiyo lilifyatua kombora na kuliharibu kombora hilo la jeshi la Yemen kabla ya kufika eneo lengwa.
Kombora la Badr-1 la Answarullah
Hili ni shambulio la pili la kombora la balestiki kufanywa na jeshi la Yemen na Harakati ya Answarullah dhidi ya shirika la mafuta la Saudia katika kipindi cha wiki moja. Alkhamisi iliyopita pia, jeshi la Yemen lililishambulia kwa kombora la balestiki shirika kubwa la uzalishaji mafuta la Saudia ambapo wakati viongozi wa Riyadh wakidai pia kwamba kombora hilo lilizuiliwa, baadhi ya duru zilisema kuwa, kombora hilo lilifika eneo lengwa. Kadhalika viongozi wa Saudia walidai kwamba tarehe 25 mwezi jana, jumla ya makombora saba yalivurumishwa kutoka nchini Yemen ambapo matatu kati yake yalianguka katika mji wa Riyadh.
Hujuma za Saudia dhidi ya maeneo ya raia nchini Yemen
Mashambulizi ya makombora ya harakati ya Answarullah na jeshi la Yemen yanajiri huku hujuma za Saudia kwa kushirikiana na nchi kadhaa za Kiarabu na Magharibi dhidi ya Yemen zikiwa zimeingia mwaka wa nne. Aidha uwezo wa makombora ya harakati hiyo unashuhudiwa huku Yemen ikiwa imewekewa mzingiro wa kila upande na nchi wavamizi.