Friday, March 30, 2018

POLISI TANZANIA: HATUJABAINI SILAHA ILIYOTUMIKA KUMUUA AKWILIN, LEMA ASHANGAA

Polisi Tanzania:  Hatujabaini silaha iliyotumika kumuua Akwilina, Lema ashangaa
Kamanda wa jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania, Lazaro Mambosasa, amesema kuwa hadi sasa bado jeshi hilo linaendelea na uchunguzi kuhusu tukio la kuuawa kwa kupigwa risasi mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwilini.
Hata hivyo Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema ameshangazwa na taarifa hiyo iliyotolewa na Kamanda wa kanda maalumu ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa kuhusu kutojulikana silaha iliyotumika kumuua Akwilina na kuandika katika ukurasa wake wa Twitter kwamba: “Nimeitafakari kauli ya Mambosasa inayohusu tukio la Akwilini kuhusu silaha iliyotumika, bila shaka kuna dhambi kubwa inapangwa nawasihi Wana CHADEMA kuwa makini wakati huu kwani si ajabu ukasikia kuwa Ile silaha iliyotumika kumuua Akwilini imekutwa nyumbani kwa Kiongozi wa CHADEMA” -Lema

Kamanda wa jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa alisema jana Ijumaa mbele ya waandishi wa habari bado hawajabaini ni silaha gani ilitumika katika tukio la mauaji ya Akwilina Akwini, ambaye kifo chake kimezusha malalamiko makubwa ya asasi mbalimbali na kiraia nchini Tanzania.
Akwilina Akwilini, mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT)
“Bado tunaendelea na upelelezi wa tukio hili. Hatujajua ile silaha iliyotumika hadi kumpata Akwilina kwa sababu askari walikuwa wengi siku ile na hakukuwa na ushahidi ni yupi aliyetenda kosa hilo.“ Amesema Mambosasa. Hii ni katika hali ambayo, tarehe 18 Februari mwaka huu Kamanda Lazaro Mambosasa alinukuliwa akisema kuwa, jeshi la polisi linawashikilia askari wake sita na silaha zao kwa ajili ya uchunguzi zaidi kuhusiana na tukio hilo.
Polisi wakituliza ghasia nchini Tanzania
Akwilina Akwilini, aliuawa kwa kupigwa risasi tarehe 16 Februari mwaka huu, wakati polisi walipokuwa wakiwatawanya wafuasi wa chama cha upinzani cha Demokrasia na Maendelea (CHADEMA) waliokuwa wanaamdamana kuelekea ofisi za mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kushinikiza mawakala wao kupatiwa barua za viapo vyao kwa ajili ya kusimamia uchaguzi mdogo uliopita wa jimbo hilo.

AL SISI ATANGAZWA MSHINDI WA KITI CHA URAIS WA MISRI

Al Sisi atangazwa mshindi wa kiti cha Rais wa Misri
Rais Abdul Fattah al-Sisi wa Misri ametangazwa mshindi wa uchaguzi tata wa rais uliofanyika Jumatatu iliyopita, kwa kuzoa asilimia 92 ya kura zote zilizopigwa.
Uchaguzi wa Rais wa Misri uliofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 26 Machi, ulimalizika juzi tarehe 28. Katika uchaguzi huo al Sisi alichuana na Moussa Mostafa Moussa wa chama cha al Ghad ambaye ametajwa na vyombo vya habari kuwa hakuwa mpinzani wa al Sisi bali alichomekwa kwenye kinyang'anyiro hicho kuhalalisha zoezi hilo.
Mambo mawili yametajwa kuwa sababu kuu za ushindi wa Abdul Fattah al Sisi hata kabla ya uchaguzi huo kufanyika.
Kwanza ni kukandamizwa kambi kuu ya upinzani katika kipindi chote cha uongozi wa miaka minne iliyopita ya utawala wa al Sisi. Kijadi, mpinzani mkuu wa kiongozi wa sasa wa Misri alipaswa kuwa mgombea yeyote wa harakati ya Ikhwanul Muslimin. Katika kipindi chote cha miongo kadhaa iliyopita watawala wa Misri wamefanya kila wawezalo kuhakikisha kwamba, harakati hiyo inakandamizwa, viongozi wake wanaoswekwa jela na wafuasi wao wanahukumiwa vifungo au hata adhabu ya kifo. Baada ya kuondolewa madarakani dikteta wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak katika mapinduzi ya wananchi ya mwaka 2011, harakati hiyo ilipata anga ya pumua kidogo na mgombea wake akashinda uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia uliofanyika nchini humo. Hata hivyo serikali ya Muhammad Mursi haikuishi zaidi ya mwaka mmoja. Serikali hiyo ya kwanza kuchaguliwa na wananchi kwa njia za kidemokrasia, iliondolewa madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Jenerali Abdul Fattah al Sisi. 
Sami Hafez Anan
Sababu kuu ya pili ya ushindi wa al Sisi ni kubinywa na hata kukamatwa wapinzani mashuhuri wa kiongozi huyo kabla kidogo ya zoezi la uchabuzi wa rais. Serikali ya Cairo iliwazuia wagombea mashuhuri kama Ahmad Shafiq, Sami Hafez Anan, Abdel Munim Abul Futuh kujitosa katika kinyang'anyiro hicho kwa kutumia visingizio mbalimbali. Hata Moussa Mustafa Moussa aliyechuana na al Sisi katika uchaguzi huo anajulikana kuwa muungaji mkono wa Abdul Fattah al Sisi.
Uchaguzi wa rais uliofanyika Misri ulifanyika kwa kuwa hakukuwa na budi kufanyika, na al Sisi alilazimika kuitisha zoezi hilo. Mchambuzi wa masuala ya siasa Hassan Shukri anasema: Uchaguzi wa rais uliofanyika Misri haukuwa ushindani baina ya wagombea wawili bali lilikuwa zoezi la kuhalalisha utawala wa al Sisi. Hata hivyo siasa za ngumi ya chuma zinazotekelezwa na al Sisi akisaidiwa na jeshi tangu miaka minne iliyopita, kutotimizwa ahadi zilizotolewa na kiongozi huyo kwa wananchi na kupuuzwa au kukanyagwa demokrasia na uhuru vimeshusha chini zaidi imani ya Wamisri kwa kiongozi huyo." 
Jenerali Abdul Fattah al Sisi
Ni kwa kutilia maanani sababu hizo mbili ndiyo maana Abdul Fattah al Sisi akaingia kwenye klabu ya viongozi wa nchi za Kiarabu wanaoshinda chaguzi za rais kwa kupata eti asimia zaidi ya 90 ya kura zilizopigwa! Pamoja na hayo wanaharakati wa masuala ya kisiasa na kijamii wanatarajia kuwa, jenerali huyo mstaafu hatafanya marekebisho ya katiba yanatakayomruhusu kubakia madarakani baada ya kumalizika muhula wake wa vipindi viwili kama wafanyavyo baadhi ya viongozi wa nchi za Kiafrika na Kiarabu.

TUNDU LISSU : KINACHOWAPATA VIONGOZI WA UPINZANI TANZANIA, NI NJIA YA KUELEKEA IKULU

  
Tundu Lissu: Kinachowapata viongozi wa upinzani Tanzania, ni njia ya kuelekea Ikulu       
Mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) nchini Tanzania, Tundu Lissu amesema kuwa, kile kinachowapata viongozi wa chama kikuu cha upinzani cha Demokrasia na Maendelea (CHADEMA), ni maandalizi ya upinzani huo kuingia madarakani.
Tundu Lissu ameyasema hayo ikiwa ni baada ya viongozi sita wa chama hicho ambao ni Mwenyekiti Taifa wa chama Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Vincent Mashinji, Manaibu Katibu Mkuu, John Mnyika (Bara) na Salum Mwalimu (Zanzibar), Mweka Hazina wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Esther Matiko na mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, kushtakiwa kwa makosa manane na kisha kunyimwa dhamana.
Viongozi wa Chadema wakiwa kwenye gari la polisi baada ya kutiwa mbaroni
Kadhalika Lissu ambaye kwa sasa yuko nchini Ubelgiji kwa ajili ya matibabu, amefafanua kuwa, kilichowapata viongozi hao wa upinzani nchini Tanzania hakiwezi kuzima taa ya madai kwa ajili ya demokrasia ya kweli nchini humo. Viongozi hao wa chama cha Demokrasia na Maendelea (CHADEMA), walipelekwa jela siku ya Jumanne baada ya kupandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka manane yakiwamo ya kufanya maandamano yaliyosababisha kifo cha Mwanafunzi wa Chuo cha NIT, Akwilina Akwiline, uasi, kuhamasisha chuki kati ya wanajamii na kuchochea ghasia nchini Tanzania.
Rais John Pombe Magufuli wa Tanzania
Hayo yanajiri katika hali ambayo siku chache zilizopita, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliviambia vyombo vya habari kwa kuzituhumu asasi za serikali ya Dar es Salaam ikiwemo polisi kwamba, zilikuwa zinapanga mkakati wa kuwafungulia kesi ya mauaji na uhaini baadhi ya viongozi wa chama chake. Kwa mujibu wa Mbowe, lengo la kutekelezwa mkakati huo ni kuhakikisha kuwa viongozi hao wanawekwa mahabusu kwa muda mrefu ili kufifisha na kuua kabisa upinzani nchini.

WAPALESTINA 8 WAUAWA SHAHIDI NA JESHI LA ISRAEL KATIKA MAANDAMANO YA SIKU YA ARDHI

Wapalestina 8 wauawa shahidi na jeshi la Israel katika maandamano ya Siku ya Ardhi
Kwa akali Wapalestina wanane wameuawa shahidi na wanajeshi katili wa Israel katika maandamano ya Siku ya Ardhi, ya kulaani hatua ya utawala huo ghasibu ya kupora ardhi zao, yaliyofanyika leo karibu na uzio wa kibaguzi wa Israel katika Ukanda wa Gaza.
Wizara ya Afya ya Palestina imesema mbali na Wapalestina wanane kuuawa shahidi kwa kumiminiwa risasi na wanajeshi katili wa Israel, wengine zaidi ya 550 wamejeruhiwa vibaya.
Kituo cha Kutetea Haki za Wapalestina cha Adalah kimelaani vikali mauaji hayo, na kueleza kusikitishwa kwake na kitendo cha jeshi la Israel kutumia risasi hai, vifaru na maroketi dhidi ya waandamanaji ambao hawana ulinzi. 
Kituo hicho kimesema mauaji hayo dhidi ya Wapalestina waliokuwa wakiandamana kutetea ardhi zao zilizoporwa ni kinyume cha sheria za kimataifa.
Siku ya Ardhi huadhimishwa Machi 30 kila mwaka
Maelfu ya Wapalestina wamejitokeza kushiriki maandamano hayo, licha ya idadi kubwa ya wanajeshi wa Israel waliojizatiti kwa silaha nzito kuuzingira uzio huo wa Gaza, na licha ya utawala huo haramu kutumia fatua za Saudi Arabia kuwashawishi Wapalestina hao kutoshiriki maandamano hayo.
Itakumbukwa kuwa, siku kama ya leo miaka 42 iliyopita, maandamano ya kwanza ya "Yaumul Ardh" au Siku ya Ardhi yalifanyika huko katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, kulaani hatua ya utawala wa Kizayuni ya kupora ardhi za raia wa Kiarabu wa Palestina.
Waarabu sita wa Israel ambao hawakuwa wamejizatiti kwa silaha waliuawa na askari wa Kizayuni katika maandamano hayo yaliyofanyika Machi 30 mwaka 1976.

UTAFITI: WAKONGOMANI 8 KATI YA 10 HAWAMUUNGI MKONO RAIS KABILA WA DRC

Utafiti: Wakongomani 8 kati ya 10 hawamuungi mkono Rais Kabila wa DRC
Utafiti mpya wa maoni umeonyesha kuwa, kwa kila raia kumi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wanane hawamungi mkono Rais Joseph Kabila wa nchi hiyo.
Utafiti huo uliofanywa mwezi jana na shirika la utafiti la Congo Research Group CRG likishirikiana na Kituo cha Utafiri wa Maoni cha BERCI katika Chuo Kikuu cha New York unaonyesha wazi kuwa, akthari ya Wakongomani wamechoshwa na uongozi wa miaka 17 wa Rais Kabila na wangetaka kumuona akiachia ngazi.
Joseph Kabila alikataa kuachia madaraka baada ya kumalizika muhula wake wa utawala kikatiba mwaka 2016, na mpaka sasa hajajitokeza hadharani kusema iwapo ataachia ngazi baada ya uchaguzi wa rais unaotazamiwa kufanyika Disemba 23 mwaka huu au la.
Moise Katumbi, mwanasiasa mjasiriamali wa DRC
Kwa mujibu wa utafiti huo wa maoni uliowashirikisha Wakongamani elfu moja katika mikoa yote 26 ya nchi hiyo, asilimia 95 ya waliohojiwa wanasema wako tayari kushiriki uchaguzi rais wa mwezi Disemba; ambapo asilimia 26 wanasema wangelimchagua Moise Katumbi, kiongozi wa upinzani aliyeko uhamishoni, huku asilimia 13 wakisema wangelimchagua mwanasiasa mwingine wa upinzani Felix Tshisekedi kurithi mikoba ya Kabila.
Utafiti mwingine wa maoni uliofanywa mwaka mmoja uliopita na CRG na BERCI ulionyesha kuwa, asilimia 38 ya wapiga kura nchini humo wako tayari kumpigia kura Katumbi, na yumkini kiwango hicho kimeshuka ikilinganishwa na utafiti wa mwaka huu, kutokana na mwanasiasa huyo tajiri kutokuweko nchini kwa miaka miwili sasa

Sunday, March 25, 2018

RAIS WA IRAN LEO ANAELEKEA TURKMENISTAN NA JAMUHURI YA AZERBAIJAN

Rais wa Iran leo anaelekea Turkmenistan na Jamhuri ya Azerbaijan
Rais Hassan Rouhani wa Iran leo anaanza safari ya siku mbili ya kuzitembelea nchi jirani za Turkmenistan na Jamhuri ya Azerbaijan kwa lengo la kujadiliana na viongozi wa nchi hizo uhusiano wa pande mbili na matukio ya hivi karibuni ya kieneo.
Akiongoza ujumbe wa ngazi za juu, Rais Rouhani ataelekea Ashgabat, mji mkuu wa Turkmenistan katika duru ya kwanza ya safari yake kufuatia mwaliko wa rais mwenzake wa nchi hiyo Gurbanguly Berdimuhamedow.
Kwa mujibu wa Parviz Ismaili,  mkuu wa kitengo cha habari katika Ofisi ya Rais wa Iran, katika safari hiyo nchi hizo mbili zitatiliana saini mikataba kadhaa ya ushirikiano hasa katika sekta za biashara. Marais Aliyev wa Jamhuri ya Azerbaijan (kushoto) na Rouhani wa Iran katika mkutano wao mjini Tehran mwaka jana
Aidha akiwa Turkmenistan, Rais Rouhani atatembelea mji wa kale wa Merv siku ya Jumatano. Baada ya hapo Rouhani ataelekea Baku, mji mkuu wa Jamhuri ya Azerbaijan ambapo atafanya mazungumzo na rais wa nchi hiyo Ilham Aliyev. Inatazamiwa pia katika safari hiyo nchi mbili zitatiliana saini mikataba kadhaa ya ushirkiano wa kiuchumi.

WASI WASI WAMAREKANI KUHUSIANA NA VITA VYA KIBIASHARA KATI YA NCHI YAO NA CHINA

Wasi wasi wa Wamarekani kuhusiana na vita vya kibiashara kati ya nchi yao na China
Suala la Rais Donald Trump wa Marekani kutia saini dikrii ya kupandishwa ushuru wa forodha wa biadhaa za China, limeibua tofauti kubwa za kibiashara kati ya Marekani na China.
Kufuatia hatua hiyo, raia hususan wakulima wa Marekani wamekumbwa na wasi wasi mkubwa juu ya hatua zinazoweza kutekelezwa na China katika uga wa kibiashara. Wasi wasi huo umeibuka baada ya radiamali ya China ya kutangaza kwamba Beijing haitorudi nyuma katika mwenendo huo. Kwa kuzingatia hali mbaya ya uchumi wa Marekani kwa sasa hususan katika sekta ya kilimo, weledi wengi wanaamini kwamba, uzalishali ndio njia pekee inayoweza kuiokoa nchi hiyo kutokana na hali mbaya.
Marais wa China na Marekani
Hata hivyo kwa kutiwa saini dikrii hiyo na kadhalika hatua mkabala za Wachina katika uwanja huo, kunaifanya njia ya wokovu kufungwa na hivyo kuisababishia matatizo zaidi ya kiuchumi jamii ya Marekani. Kufuatia hali hiyo, Cui Tiankai, balozi wa China mjini Washington sambamba na kuonyesha kutofurahishwa na maamuzi ya serikali ya Marekani kuhusiana na kadhia hiyo amesema kuwa, kamwe China haikupendelea kuingia katika vita vya kibiashara na Marekani, lakini akatahadharisha kwamba, iwapo Beijing italazimika kuingia katika uwanja huo, basi haitorudi tena nyuma. Radiamali hiyo kali ya China, imeisababishia wasi wasi mkubwa jamii ya kiuchumi ya Marekani kiasi cha kuyafanya masoko ya hisa nchini humo kuporomoka.
Mgogoro kati ya Marekani na China
Timu ya Rais Donald Trump wa Marekani inaamini kwamba, kuzidishwa ushuru wa forodha kwa bidhaa za China kwa kiasi fulani kutapelekea kushuka kwa nakisi ya kibiashara ya Marekani ambapo licha ya kuwa huenda suala hilo likawa na madhara kwa sekta tofauti za kiuchumi nchini, lakini kwa muda mrefu litakuwa na maslahi kwa uchumi na jamii nzima ya Marekani. Peter Navarro, mshauri mkuu wa rais katika masuala ya biashara na viwanda, anasema kuwa, kupungua nakisi ya kibiashara, ni jambo linalotishia usalama wa taifa na kuifanya nchi hiyo kutegemea madeni na uwekezaji wa kigeni. Weledi wa mambo wanaamini kwamba, kutekelezwa dikrii hiyo mpya ya Rais Donald Trump wa Marekani kwa mashirika makubwa kama vile Boeing na Apple, kutakuwa na madhara makubwa sambamba na kupelekea makumi ya maelfu ya watu kupoteza fursa zao za kazi ndani ya nchi hiyo. Kadhalika iwapo China itachukua hatua ya kulipiza kisasi, basi sekta ya kilimo ya Marekani hususan uzalishaji wa mazao ya Soya, nao utaathirika zaidi huku makumi ya maelfu ya watu pia wakipoteza ajira. 
Mvutano ukiendelea
Jim Byrum, mtaalamu wa masuala ya kisiasa nchini Marekani, anasema: "Hivi sasa tunashuhudia mgogoro mkubwa. Ninachukia hata kutamka neno 'vita vya kibiashara,'  hata hivyo inaonekana kuwa sisi tayari tumesukumwa kuelekea upande huo." Mwisho wa kunukuu. Inaonekana kuwa, vita vya kibiashara kati ya Marekani na China vinakaribia kutokea. Ni wazi kuwa kupungua uzalishaji ni moja ya matokeo ya siasa ambazo zitasababisha kuongezeka kiwango cha watu wasio na ajira nchini Marekani. Kwa hakika wasi wasi wa mashirika na wakulima wa Marekani ni jambo lililo mahala pake, kwani hatua mkabala ya Wachina itazisababishia madhara makubwa sekta tofauti za kiuchumi nchini Marekani.

SERIKALI YA NIGERIA INAFANYA MAZUNGUMZO NA BOKO HARAMU YA UWEZEKANO WA KUSITISHA MAPIGANO

Serikali ya Nigeria inafanya mazungumzo na Boko Haram ya uwezekano wa kusitisha mapigano
Waziri wa Habari wa Nigeria amesema serikali inafanya mazungumzo na kundi la kigaidi na kitakfiri la Boko Haram kuhusu uwezekano wa kusitisha mapigano, lengo kuu likiwa ni kuhitimisha kikamilifu uadui na uhasama baina ya pande mbili.
Hii ni mara ya kwanza baada ya miaka kadhaa kwa serikali ya Abuja kutangaza kuwa inafanya mazungumzo na Boko Haram kuhusu usitishaji mapigano yaliyosababishwa na uasi uliopelekea kuuawa maelfu ya watu tangu mwaka 2009.
"Wengi wakiwa hawajui, kwa muda sasa tumekuwa tukifanya mazungumzo mapana ya kuhitimisha uhasama na waasi" amesema Lai Mohammed, Waziri wa Habari wa Nigeria kupitia taarifa aliyotoa kuzungumzia pia kilichofanyika hadi kupelekea kuachiwa huru zaidi ya wanafunzi wa kike 100 na kundi la kigaidi la Boko Haram wiki iliyopita.
Wasichana hao walitekwa nyara Februari 19 katika mji wa Dapchi kaskazini mashariki mwa Nigeria. Utekaji nyara huo wa wanafunzi wapatao 110 ulikuwa wa idadi kubwa zaidi tangu wanafunzi wa kike wapatao 270 walipotekwa nyara na kundi la kitakfiri la Boko Haram katika mji wa Chibok ulioko kaskazini mashariki pia mwa Nigeria mwaka 2014.
Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria akiwa na wanafunzi wa mji wa Dapchi baada ya kuachiwa huru na kuonana nao mjini Abuja
Siku ya Jumatano iliyopita, wanamgambo wa kundi la kigaidi la Boko Haram waliwashangaza wakaazi wa mji wa Dapchi walipoingia na magari mjini humo na kuwaachia huru wasichana hao ambao walisema, wenzao watano walifariki walipokuwa wakishikiliwa na kundi hilo na mmoja mwengine bado hajaachiwa huru.
Kwa mujibu wa Waziri wa Habari wa Nigeria, makubaliano yaliyofikiwa ya kusitisha mapigano kwa muda wa wiki moja kuanzia Machi 19 ndiyo yaliyowezesha Boko Haram kuwaachia huru wasichana hao.../

Thursday, March 22, 2018

KENYA NI MWENYEJI WA WIKI YA KUPAMBANA NA UBAGUZI WA RANGI WA ISRAEL

Kenya ni mwenyeji wa Wiki ya Kupambana na Ubaguzi wa Rangi wa Israel
Duru ya 14 ya 'Wiki ya Kupambana na Ubaguzi wa Rangi wa Israel' inafanyika katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi ikijumuisha maonyesho ya filamu, mijadala na matamasha ya kiutamaduni.
Shughuli hiyo ilianza tarehe 12 Machi na itaendelea kwa siku kadhaa zijazo kwa lengo la kuelimisha jamii kuhusu mfumo wa ubaguzi wa rangi (apartheid) katika utawala haramu wa Israel unaowalenga Wapalestina wanaopigania ukombozi wa ardhi zao.
Filamu kadhaa zinaonyesha kuhusu ubaguzi wa rangi Israel kwa lengo la kuwafahamisha wapenda haki nchini Kenya kuhusu utambulisho wa kibaguzi wa utawala haramu wa Israel. Hafla hizo zimehudhuriwa na watu wa matabaka mbali mbali ya jamii. Mijumuiko ya 'Wiki ya Kupambana na Ubaguzi wa Rangi wa Israel' nchini Kenya imeandaliwa na Harakati ya Mshikamano wa Kenya na Palestina kwa ushirikiano na Tume ya Haki za Binadamu Kenya, Kituo cha Uadilifu wa Kijamii cha Mathare, Kituo cha Utafiti cha Mau Mau, jumuiya za kijamii za Fahamu, Awaaz na Kituo cha Kulinda na Kutetea Haki kati ya taasisi zinginezo.
Kwa ujumla 'Wiki ya Kupambana na Ubaguzi wa Rangi wa Israel' (Israeli Apartheid Week) hulenga kuwahimiza walimwengu kuunga mkono harakati ya kuusisia kwa kila namna utawala haramu wa Israel. Mwaka huu ''Wiki ya Kupambana na Ubaguzi wa Rangi wa Israel'  ilianza Februari 19 na itaendelea hadi tarehe 17 Aprili' katika miji mbali mbali duniani.

SALAMU ZA PONGEZI ZA TRUMP KWA PUTIN HASIRA ZA WAPINZANI WA RUSSIA NDANI YA UTAWALA WA MAREKANI

Salamu za pongezi za Trump kwa Putin na hasira za wapinzani wa Russia ndani ya utawala wa Marekani
Salamu za pongezi alizotoa rais wa Marekani kwa rais wa Russia kwa ushindi aliopata wa kuchaguliwa tena kuwa rais wa nchi hiyo katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni zimewakasirisha baadhi ya maseneta nchini Marekani.
Seneta wa chama cha Republican John MacCain amemtuhumu Rais Vladmir Putin wa Russia kuwa ni dikteta na kusema kwamba: kwa kumpa salamu za pongezi Vladmir Putin,Trump amewatusi wananchi wote wa Russia ambao wamenyimwa haki ya kupiga kura katika uchaguzi huru na wa haki ili kuamua kuhusu mustakabali wa nchi yao, ikiwemo idadi kubwa ya wazalendo wa Russia; watu ambao wamehimili hatari nyingi ili kuweza kutumia haki yao ya kulalamika na kupambana na utawala wa Putin.
Seneta John McCain (kulia) na Rais Vladmir Putin wa Russia
Madai hayo yanatolewa katika hali ambayo katika uchaguzi wa rais wa Russia uliofanyika hivi karibuni vyama na mirengo tofauti ya kisiasa ikiwemo ya wapinzani wakubwa wa Kremlin ilishiriki kwenye uchaguzi huo kuchuana na rais Putin. Hata hivyo kiongozi huyo ameweza kuvutia kura na mapenzi ya aghalabu ya Warussia kutokana na utendajikazi wake wa miaka 17 hususan mafanikio aliyopata ya kuitatua migogoro ya kisiasa, kiuchumi na kiusalama iliyotokana na kuvunjika Shirikisho la Kisovieti la Urusi ya zamani na kufufua tena nguvu na satua ya nchi hiyo katika uga wa kimataifa. Hali hiyo imetafsiriwa na kuelezewa na mirengo inayoipinga Russia katika nchi za Magharibi na hasa Marekani kuwa ni udikteta na hila za kutaka kuyatia mkono matokeo ya uchaguzi wa rais wa Russia uliofanyika hivi karibuni. Mrengo huo unaitumia kila fursa ikiwemo ya utoaji salamu za pongezi rais wa Marekani kwa rais wa Russia ili kuvuruga uhusiano wa Washington na Moscow, ilhali kuwasiliana kwa njia ya simu marais wa nchi mbili na kupongezana kwa kushinda katika uchaguzi ni jambo la kawaida na lililozoeleka. Takribani mwaka mmoja na nusu uliopita Putin alimtumia salamu za pongezi Trump aliposhinda uchaguzi wa rais wa Marekani uliofanyika mwaka 2016; na hivi sasa baada ya kupita siku mbili tangu kufanyika uchaguzi wa rais wa Russia, Trump naye amefanya vivyo hivyo kupitia mazungumzo aliyofanya kwa njia ya simu na Vladmir Putin. Lakini yeye amekwenda hata mbali zaidi kwa kueleza matumaini aliyonayo ya kupatikana fursa haraka iwezekanavyo ya kukutana na kufanya mazungumzo na rais wa Russia.
Trump (kulia) na Putin wameshakutana zaidi ya mara moja kwa mazungumzo
Mrengo unaoipinga Russia nchini Marekani una hofu baada ya kuona kwamba, licha ya propaganda kali za kueneza sumu dhidi ya Kremlin kwa kutumia visingizio mbalimbali kama kuingilia Russia uchaguzi wa rais wa Marekani sambamba na tuhuma mpya dhidi ya Moscow za kumpa sumu jasusi wa pande mbili wa Uingereza, Trump angali anafanya kila njia ili kuona uhusiano wa nchi yake na Russia unaboreka.
Tangu wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais mwaka 2016 hadi sasa, rais wa sasa wa Marekani amesisitiza mara kadhaa kwamba bila ya kushirikiana na Russia baadhi ya mizozo mikubwa ya kimataifa hususan mgogoro wa vita vya Syria hautoweza kutatuka. Ni kwa sababu hiyo Trump angali anashikilia msimamo wake wa kuendelea kuwa na mawasiliano binafsi na rais wa Russia, kitendo ambacho kwa mtazamo wa baadhi ya watu kama John McCain, mkuu wa kamati ya huduma za vikosi vya ulinzi vya Marekani katika Seneti ya nchi hiyo, ni dhambi isiyosameheka.

Monday, March 5, 2018

MFUASI WA MUGABE AUNDA CHAMA KIPYA CHA SIASA ZIMBABWE KUCHUANA RAIS MNANGAGWA KATIKA UCHAGUZI

Mfuasi wa Mugabe aunda chama kipya cha siasa Zimbabwe kuchuana na rais Mnangagwa katika uchaguzi
Ambrose Mutinhiri, jenerali mstaafu wa jeshi la Zimbabwe na mfuasi wa aliyekuwa rais wa nchi hiyo Robert Mugabe ameunda chama kipya cha siasa kinachojulikana kama Harakati Mpya ya Kizalendo (NFP) kuchuana na rais Emmerson Mnangagwa katika uchaguzi mkuu ujao.
Mutinhiri, ambaye ni veterani wa vita vya uhuru wa Zimbabwe katika miaka ya 1970 alijitoa kwenye chama tawala cha ZANU-PF na kujiuzulu kiti chake cha ubunge siku ya Ijumaa iliyopita na kukutana na Mugabe siku ya Jumapili kumtaarifu juu ya kinachoendelea.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotoa hapo jana, NFP imetangaza kuwa  chama hicho kimeundwa na wananchama wa ZANU-PF na Wazimbabwe waliokasirishwa na utaratibu usio wa kikatiba na wa udhalilishaji uliotumika kumuondoa kihalifu uongozini rais Mugabe na wale kiliowataja kama wahalifu halisi walioiharibu bila ya aibu demokrasia inayochipua ya Zimbabwe.
Rais Emmerson Mnangagwa (kushoto) na Robert Mugabe (kulia)
Hayo yanajiri katika hali ambayo duru za karibu na rais wa zamani wa Zimbabwe zimeripoti kuwa Mugabe ana uchungu wa kuondolewa kwenye kiti cha urais alichokalia kwa miaka 37 na kwamba ametangaza uungaji mkono wake kwa chama kipya cha New Patriotic Front (NFP).
Mnamo mwezi Januari mwaka huu rais Emmerson Mnangagwa alitangaza kuwa uchaguzi ujao wa Rais, Bunge na serikali za mitaa nchini Zimbabwe utafanyika katika mazingira huru na ya haki.../

KUONGEZEKA BAJETI YA KIJESHI YA CHINA KATIKA MWAKA 2018

Kuongezeka bajeti ya kijeshi ya China katika mwaka 2018
Serikali ya China imetangaza kuongeza bajeti yake ya kijeshi katika mwaka huu wa 2018.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, bajeti ya kijeshi ya China katika mwaka huu wa 2018 itaongezea kwa asilimia 8.10. Bajeti ya kijeshi ya nchi hiyo imetangazwa kuwa  dola  bilioni 175. Duru za kijeshi nchini China zinasema kuwa bajeti ya kijeshi ya nchi hiyo bado ni ndogo ikilinganishwa na bajeti ya Marekani ya dola bilioni 700. Pamoja na hayo, hatua ya China ya kuongeza bajeti yake ya kijeshi inahesabiwa kuwa ni aina fulani ya radiamali ya nchi hiyo kwa mipango ya kijeshi ya kichokozi ya Marekani katika eneo la mashariki mwa Asia; ambayo imeshika kasi katika kipindi hiki cha mwaka mmoja wa hivi karibuni wa utawala wa Rais Donald Trump wa nchi hiyo.
Rais Donald Trump wa Marekani 
Katika stratejia yake mpya ya usalama wa taifa iliyoitangazwa hivi karibuni, Marekani inahisi kuwa China  ni nchi tishio zaidi dhidi yake na inasisitiza kuhitimishwa nguvu hiyo ya China. Moja ya siasa za kistratejia za Marekani mkabala na China ni kuona kunafanyika jitihada za kuishawishi Beijing izidishe bajeti yake ya kijeshi sambamba na kuiingiza katika mashindano ya kijeshi kati yake na Marekani na waitifaki wake katika eneo kama vile Japan na Korea ya Kusini. Siasa ambazo zinatajwa na viongozi wa China kuwa ni siasa za fikra za vita baridi za Washington; na kuamini kuwa Marekani inafanya kila iwezalo ili kuifanya China kuwa na mustakbali kama ule wa Umoja wa Kisovieti. Ndio maana China haipendelei kuingia katika mashindano ya kijeshi na Marekani licha  ya kuzidisha bajeti yake ya kijeshi. 
Nikita Danuk Naibu Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Kistratejia ya Russia anasema kuwa: Rais Donald Trump hataki kuharibu misingi ya  ushirikiano kati ya Washington na Beijing. Amejikita zaidi na kuzingatia kubadili ajenda ya siasa za nje za kila siku za Marekani. Nchi hii itaamiliana kwa tahadhari na China na kujaribu kupunguza taathira za China katika eneo. 
Moja ya manowari za China
Pamoja na hayo yote, China inatambua vyema kuwa mipango ya kiuchumi ya Marekani ikiwemo ile ya kuongeza tozo ya ushuru kwa bidhaa zinazoingia nchini humo kutoka China na kuvibana vitega uchumi vya nchi hiyo inaweza kuisababisha madhara nchi hiyo. Ndio maana China nayo hivi karibuni ikaamua kuendeleza mipango yake ya ustawi wa kijeshi yaani kuimarisha uwezo wake wa kujilinda mkabala na  Marekani. Wakati huo huo China inaamini kuwa vita vikuu zaidi vya kulazimishwa dhidi yake kutoka kwa Rais Donald Trump ni vita vya kibiashara na mara kwa mara  imetahadharisha kuhusu madhara ya vita hivyo. 
Majeshi ya China yakifanya maneva kwenye maji ya kusini mwa nchi hiyo
Kwa vyovyote vile  Marekani inafahamu vyema kuwa China ni nchi pekee yenye ushawishi chanya mkabala na nafasi ya kimataifa ya Washington katika maeneo mbalimbali duniani. Suala hilo ndilo lililoifanya Marekani itekeleze siasa za pande zote katika nyanja za kijeshi na kiuchumi dhidi ya Beijing na katika upande wa pili pia serikali ya China inafanya kila iwezalo ili kudhibiti hali ya mgogoro na siasa hizo za Trump; siasa ambazo kwa mtazamo wa Beijing zimefanikiwa na zinaweza kuipelekea kuimarisha amani na usalama katika eneo la mashariki mwa Asia kwa kushirikiana nchi za eneo hilo.

Sunday, March 4, 2018

UN YASIMAMISH SHUGHULI ZAKE NIGERIA BAADA YA WAHUDUMU WAKE KUUAWA

UN yasimamisha shughuli zake Nigeria baada ya wahudumu wake kuuawa
Umoja wa Mataifa umetangaza habari ya kusitisha shughuli zake za utoaji huduma na misaada ya kibinadamu kaskazini mashariki mwa Nigeria kutokana na kuuawa wafanyakazi wake katika mashambulizi ya hivi karibuni ya magaidi wa Boko Haram.
Taarifa ya Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa imesema kuwa, wahudumu 40 wa UN walikuwa katika mji wa Rann ambao una kambi ya wakimbizi wa ndani wapatao 55 elfu ulipovamiwa Alkhamisi usiku na wapiganaji wa Boko Haram.
Amesema kufuatia hujuma hiyo, Umoja wa Mataifa umesimamisha kwa muda utoaji wa huduma za kibinadamu katika mji huo ulioko kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Wapiganaji wa kundi la kigaidi la Boko Haram
Siku ya Ijumaa, shirika la madaktari wasio na mipaka lilitangaza habari ya kusimamisha shughuli zake zote kaskazini mwa Nigeria baada ya genge la wakufurishaji la Boko Haram kuushambulia mji wa Rann katika jimbo la Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Katika shambulizi lililofanywa na genge hilo Alkhamisi usiku, watu 11 wakiwemo wafanyakazi watatu wa kutoa misaada waliuawa huku wengine watatu wakihofiwa kutekwa nyara baada ya hujuma hiyo.
Mashambulizi ya magaidi wa Boko Haram nchini Nigeria na katika nchi jirani za Chad, Niger, na Cameroon yameshapelekea zaidi ya watu 20 elfu kuuawa na milioni mbili na laki sita wengine kuwa wakimbizi.

Friday, March 2, 2018

AL-SHABAAB YAUA ASKARI 5 WA KENYA KAUNTI YA MANDERA

Al-Shabaab yaua askari polisi 5 wa Kenya kaunti ya Mandera
Askari polisi watano wa Kenya wameuawa na wengine watatu kujeruhiwa baada ya wanachama wa kundi la kigaidi na kitakfiri la al-Shabaab kushambulia kambi mbili za maafisa usalama katika mji wa Fino katika kaunti ya Mandera.
Naibu Kamishna wa kaunti ndogo ya Laafey huko kaskazini mwa Kenya, Eric Oronyi amesema shambulizi hilo limefanyika usiku wa kuamkia leo, ambapo wanamgambo hao wamevamia kituo cha polisi wa kawaida na wa utawala katika mji wa Fino.
Amesema wavamizi hao kati ya 70 hadi 100 mbali na kutekeleza mauaji hayo, kadhalika wameng'oa mlingoti wa shirika moja la simu za rununu na kulemaza mawasiliano.
Magaidi hao wamekuwa wakishambulia mabasi ya uchukuzi wa umma kaunti ya Mandera na kuua
Mwezi uliopita, maafisa wengine watano wa polisi ya Kenya waliuawa baada ya wanachama wa al-Shabaab kushambulia msafara wa magari ya maafisa usalama katika barabara ya Elwak-Kotulo katika kaunti hiyo hiyo ya Mandera.
Kundi la kigaidi la al-Shabaab lenye makao yake Somalia mara kwa mara hutekeleza mashambulizi ndani ya ardhi ya Kenya kuishinikiza serikali ya nchi hiyo iondoe wanajeshi wake wanaohudumu katika Kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Afrika Somalia, AMISOM