Saturday, September 23, 2017

KENYA YATAKA DUNIA ISAIDIE KIKOSI CHA AAMISOM KULINDA AMANI SOMALIA

Kenya yataka dunia isaidie kikosi cha AMISOM kulinda amani Somalia
Kenya imeitaka jamii ya kimataifa iongeze zaidi usaidizi wake kwa Kikosi cha Umoja wa Afrika cha Kulinda amani Somalia, AMISOM ili kiweze kushughulikia kwa kina vitisho vya usalama kabla ya kuanza kutekelezwa mpango wa kupunguza idadi ya askari wake.
Ombi hilo limo katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Balozi Amina Mohammed wakati akihutubia kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani siku ya Ijumaa.
Amesema ili kuimarisha mafanikio yaliyokwishapatikana, Kenya inaunga mkono azimio la Baraza la Usalama kuhusu msingi ya AMISOM. Aidha amesema zaidi ya yote kuna haja ya kuwepo msaada wa kuwezesha ujenzi mpya wa Somalia, kukiwemo kuwezesha serikali kutoa huduma za msingi.

Askari wa kulinda amani wa AMISOM 
Kwingineko katika hotuba yake, Balozi Amina amezungumzia pia mabadiliko ya tabianchi akisema kuwa pamoja na kusababisha mizozo ya rasilimali za maji na ardhi, yanagharimu asilimia 3 ya pato la ndani la taifa kila mwaka.
Hali kadhalika Waziri huyo wa Mambo ya Nje wa Kenya amezungumza kuhusu suala la wakimbizi kwa kutambua kuwa Kenya tangu miaka ya 60 imehifadhi wakimbizi kutoka nchi jirani ikiwemo Somalia, hatua ambayo imekuwa na changamoto nyingi zikiwemo za kiusalama.
Amesema ni kwa mantiki hiyo ndipo mwaka 2013 Kenya ilitia saini makubaliano ya pande tatu baina yake, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR na serikali ya Somalia kwa lengo la kuwezesha wakimbizi kurejea nyumbani kwa hiari.

Friday, September 22, 2017

KOREA KASKAZINI NA MAREKANI ZAENDELEZA VITA VYA MANENO

Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un amemuita Rais Donald Trump kuwa ni "ni mtu asiyeweza kufikiri sawasawa" na kusema atalipa gharama kutokana na kauli zake za vitisho anazotoa dhidi ya nchi hiyo.
Südkorea TV Bildschirm mit Donald Trump und Kim Jong Un (picture-alliance/AP Photo/Ahn Young-joon)
 Kwa mujibu wa shirika la habari la Korea Kaskazini Kim Jong Un amesema hii leo kuwa Trump ni mtu asiyestahili kuwa na hadhi ya kuwa na mamlaka aliyo nayo ya amiri jeshi mkuu wa nchi na kumuelezea Rais huyo wa Marekani kuwa ni mtu "mjanja na jambazi  anayechezea moto".
Matamshi hayo ya kiongozi wa Korea Kaskazini yanafuatia hotuba ya Rais Donald Trump aliyoitoa katika mkutano wa baraza kuu la Umoja wa Mataifa Jumanne wiki hii. Kim Jong Un amesema matamshi ya Trump yamemshawishi kuamini kuwa njia ambayo kiongozi huyo wa Korea Kaskazini aliyochagua kuifuata ni sahihi na kuwa ndiyo anapaswa kuifuata hadi mwisho na kuongeza kuwa alikuwa akifikiria kuchukua hatua kali.  Waziri wa mambo ya nje wa Korea Kaskazini ameripotiwa akitishia nchi hiyo kufanya jaribio la bomu la Hydrogen katika bahari ya pasifiki.
Trump atangaza vikwazo vipya dhidi ya Korea Kaskazini
Haya yanakuja mnamo wakati Rais Donald Trump akitangaza vikwazo vipya dhidi ya Korea Kasakazini vinavyolega kuidhibiti uwezo wa nchi hiyo katika kuendeleza mipango yake ya kuwa na uwezo wa kutengeneza silaha za nyukilia pamoja na makombora.  Rais Trump alitangaza vikwazo hivyo hapo jana wakati alipokuana na viongozi wa nchi washirika Japan na Korea Kusini ikiwa ni siku mbili baada ya kulihutubia baraza kuu la Umoja wa Mataifa na kutishia kuwa ataisambaratisha Korea Kaskazini iwapo itaendelea na vitendo vyake vya uchokozi.
Trump alisaini hapo jana amri nyingine ya utekelezaji inayolenga kuyapiga marufuku makampuni yaliyoko Marekani  yanayoshirikiana kibiashara na Korea Kaskazini.
Waziri anayehusika na masuala ya fedha wa Marekani Steven Mnuchin amesikika akisema kuwa taasisi za fedha tayari zimetaadharishwa kuwa zinapaswa kuchagua moja ama zinafanya biashara na Marekani au Korea Kaskazini.
Miami Steve Mnuchin US-Finanzminister (picture-alliance/AP Photo/L. Sladky) Waziri wa fedha wa Marekani Steven Mnuchn
Tayari Korea Kaskazini imeyapiga marufuku makampuni ya kigeni yanayoshirikiana na Korea Kaskazini katika mipango yake ya kijeshi lakini hatua ya sasa inatanua wigo wa vikwazo vilivyochukuliwa dhidi ya Korea Kaskazini ambavyo sasa vinagusa kuanzia teknolojia ya habari na mawasiliano, sekta ya uzalishaji ikiwa ni pamoja na viwanda vya nguo pamoja na uvuvi.
Hata hivyo nyakati zitaeleza iwapo vikwazo hivyo vya kuchumi vitamlazimisha kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un kurudi nyuma ingawa kiongozi huyo kijana anaonekana kuionyesha dunia kuwa hatishwi na matamshi makali ya Trump.
Sigmar Gabriel asisitiza juu ya ushirikiano kimataifa
USA Bundesaussenminister Sigmar Gabriel spricht vor der UN-Vollversammlung (Reuters/E. Munoz) Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmar Gabriel
Wakati huohuo waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Sigmar Gabriel katika hotuba yake kwenye baraza kuu la Umoja wa Mataifa ameonya juu ya kauli za  kutanguliza masilahi ya taifa akionesha dhahiri kutokukubaliana na kauli kama hiyo ambayo imetolewa mara kwa mara na Rais wa Marekani Donald Trump.
Akizungumza pasipo kumtaja Trump, Gabriel alisema kauli za kutanguliza utaifa kwanza ni kauli ambazo zitasababisha migongano kitaifa na mwishowe hakuna faida itakayopatikana.  Amesisitiza kuwa dunia inahitaji ushirikiano zaidi kimataifa na utaifa kidogo na siyo kinyume chake.
Aidha waziri huyo wa mambo ya nje wa Ujerumani alitoa mwito wa kuimarishwa kwa Umoja wa Mataifa akitolea mfano wa mafanikio ambayo Ujerumani imepata kupitia ushirikiano kimataifa na pia ushirikiano barani ulaya na kuongeza kuwa halikuwa suala la "Ujerumani kwanza" lililoifanya Ujerumani kuwa taifa lenye nguvu kiuchumi bali  ni Ulaya pamoja na kuwajibika kimataifa.

SERIKALI NIGERIA YAELEZA WASIWASI WAKE KUHUSU SILAHA ZA MAGENDO NCHINI HUMO

Serikali Nigeria yaeleza wasiwasi wake kuhusu silaha za magendo nchini humo
Serikali ya Nigerfia imetangaza kwamba, ina wasiwasi kuhusu silaha zinazoingizwa kwa wingi nchini humo kupitia njia za magendo.
Msemaji wa Idara ya Forodha ya Nigeria, Joseph Attah amesema kuwa matokeo ya awali ya uchunguzi uliofanyika katika uwanja huo yanaonesha kuwa, wahusika wa magendo ya silaha nchini Nigeria ni makundi ya mafia yaliyoko nchini Uturuki.
Attah ameongeza kuwa, tangu mwanzoni mwa mwaka huu silaha zaidi ya elfu tatu zimegunduliwa na kukamatwa katika bandari ya Lagos kutoka Uturuki. 
Hadi sasa ubalozi wa Uturuki nchini Nigeria haujasema lolote kuhusu tuhuma hizo za magendo ya silaha kutoka Uturuki kelekea Nigeria. 
Silaha za magendo zinaingizwa Nigeria kutoka Uturuki
Maafisa wa Idara ya Forodha ya Nigeria wanatazamiwa kufanya mazungumzo na wenzao wa serikali ya Uturuki akiwemo balozi wa nchi hiyo mjini Abuja kuhusu maudhui ya magendo ya silaha zinazoingizwa nchini humo kutoka Uturuki. 
Nigeria imekuwa ikisumbuliwa na machafuko makubwa hususan katika maeneo ya kaskasini mwa nchi hiyo.

UNICEF: ASILIMIA 60 YA WAKIMBIZI WA ROHINGYA NI WATOTO WADOGO


UNICEF: Asilimia 60 ya wakimbizi wa Rohingya ni watoto wadogo
Mfuko wa Watoto wa Umoja wa Mataifa (UNICEF) umetangaza kuwa, karibu asilimia 60 ya wakimbizi Waislamu wa jamii ya Rohingya waliokimbilia Bangladesh kutokana na mauaji na ukatili unaofanywa na Mabudha na jeshi la Myanmar, ni watoto wadogo.
UNICEF imetangaza kuwa, hadi sasa watoto 1400 wa Waislamu wa Rohingya wamesajiliwa baada ya kuvuka mpaka na kuingia Bangladesh wakiwa peke yao bila ya wazazi au wasimamizi wao. 
Taarifa ya UNICEF imesema kuwa, watoto hao wakimbizi wameshuhudia kwa macho mauaji ya wazazi na watu wa familia zao au kuchomwa moto makazi na nyumba zao. 
Taarifa hiyo imeongeza kuwa, kambi za wakimbizi za Waislamu wa Rohingya nchini Bangladesh zina hali mbaya sana na kwamba makumi ya maelfu ya wakimbizi hao wanaoshi katika maeneo yasiyo na usalama na yasiyofaa kwa ajili ya watoto.
Wakimbizi wa Rohingya, Myanmar
Maelfu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya wameuawa katika mashambulizi yanayoendelea kufanywa na Jeshi la Myanmar na Mabudha wenye misimamo ya kuchupa mipaka hususan katika jimbo la Rakhine.   
Wimbi jipya la mauaji ya Waislamu wa Rohingya katika jimbo hilo lililoko magharibi mwa Myanmar lilianza tarehe 25 Agosti mwaka huu. Takribani Waislamu laki nne kutoka Myanmar wamekimbilia nchi jirani ya Bangladesh na hali katika kambi za wakimbizi ni mbaya kutokana na kukosekana misaada ya kutosha.

AL: BOMU LA SAUDIA LILILOUA FAMILIA YA BUTHAINA LILITENGENEZWA MAREKANI

AI: Bomu la Saudia lililoua familia ya Buthaina lilitengenezwa Marekani
Wataalamu wa shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International wamesema kuwa, bomu lililoua raia 16 wa Yemen wakiwemo watu wote wa familia ya mtoto Buthaina aliyenusurika shambulizi hilo, lilitengenezwa nchini Marekani.
Uchunguzi uliofanywa na wataalamu wa silaha wa Amnesty International umebaini kuwa, bomu lililotumiwa na Saudia kuua raia hao lina sifa za mabomu ya Marekani yanayorushwa na ndege na kuongozwa kwa leza.
Ripoti hiyo imesisitiza kuwa, mashambulizi yanayofanywa na Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya Yemen yanaendelea kuwa sababu kuu ya mauaji ya raia hususan watoto wadogo nchini Yemen.
Buthaina akiwa hospitali
Matokeo hayo ya utafiti wa Amnesty International yametolewa baada ya Umoja wa Ulaya kuwasilisha muswada katika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa ukitaka kufanyike uchunguzi kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanyika nchini Yemen.
Shambulizi la ndege za Saudi Arabia lililofanyika tarehe 25 mwezi uliopita wa Agosti katika makazi ya raia mjini Sana'a liliua raia 16 wakiwemo wazazi wawili na mtoto Buthaina na ndugu zake watano. Alipoulizwa anataka kufanya nini, Buthaina mwenye umri wa miaka 5 ambaye amebakia peke yake kati ya watu wote wa familia yake, alisema anataka kurudi nyumbani na kucheza na ndugu zake….
Buthaina akijaribu kufungua jicho lake moja lililobakia zima
Picha zilizooneshwa na vyombo vya habari za mtoto huyo ndogo wa Yemen aliyebakia peke yake baada ya familia yake yote kuuawa na ndege za Saudi Arabia zimewasikitisha sana walimwengu.
Buthaina aliyejeruhiwa katika shambulizi hilo amepoteza jicho lake moja.

MWANASHERIA MKUU: KENYA HAIKO KWENYE HATARI YA MGOGORO WA KIKATIBA

Mwanasheria Mkuu: Kenya haiko kwenye hatari ya mgogoro wa kikatiba
Mwanasheria Mkuu wa Kenya amesema kuwa nchi hiyo haitakabiliwa na mgogoro wa kikatiba au wa kisiasa hata kama uchaguzi rais wa marudio uliopangwa kufanyika Oktoba 26, umesogezwa tarehe hadi baada ya mwishoni mwa Oktoba.
Githu Muigai ameongeza kuwa, serikali ya sasa itaendelea kuwepo madarakani kihalali kwa nguvu kamili ya kikatiba hadi uchaguzi mpya utakapokamilika na kiongozi mpya kuapishwa.
Mahakama ya Juu ya Kenya mwezi huu ilitengua ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi wa Agosti 8 ikiashiria kuwepo kasoro na kuiamuru Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka kuandaa uchaguzi mpya hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Oktoba. Uhuru Kenyatta atachuana kwa mara nyingine na hasimu wake kutoka muungano wa Nasa, Raila Odinga.
Mwanasheria Mkuu wa Kenya alikuwa akijibu matamshi ya wakili wa Odinga katika shauri lililopelekea kutenguliwa ushindi wa Kenyatta, Bwana James Orengo aliyesema kuwa muhula wa urais wa Kenyatta utafikia kikomo iwapo uchaguzi huo wa marudio hautafanyika hadi kufikia mwishoni mwa Oktoba na hivyo kuitumbukiza nchi katika mgogoro wa kikatiba.
Wakili James Orengo ambaye amepingana na kauli ya Mwanasheria Mkuu wa Kenya 
Naye kiongozi wa  muungano wa NASA nchini Kenya Raila Odinga amesema anaamini kuwa, muhula wa kuwa madarakani Uhuru Kenyatta utamalizika katika kipindi cha siku 60 baada ya Mahakama ya Kilele kutoa uamuzi wa kutengua matokeo ya uchaguzi wa rais tarehe Mosi Septemba. Odinga amesema hatashiriki uchaguzi iwapo baadhi ya masharti hayatatimizwa likiwemo la kutaka kuondolewa baadhi ya maafisa wa Tume Huru ya Uchaguzi

HATIBU WA SWALA YA IJUMAA TEHRAN: TRUMP NI MTU MWENYE AKILI FINYU, KIDHABI NA MPENDA VITA

Hatibu wa Swala ya Ijumaa Tehran: Trump ni mtu mwenye akili finyu, kidhabi na mpenda vita
Hatibu wa Swala ya Ijumaa ya leo mjini Tehran amesema kuwa hotuba iliyotolewa na Rais Donald Trump wa Marekani katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ni ya kipumbavu na kwamba Trump ni mtu mwenye akili finyu, kidhambi na mpenda vita.
Katika hutuba yake ya hivi karibuni kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Rais huyo wa Marekani aliituhumu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ambayo ni miongoni mwa mihimili na nguzo kuu za kupambana na magaidi katika eneo la Mashariki ya Kati, kuwa inaunga mkono ugaidi.
Katika hotuba zake za leo kwenye Swala ya Ijumaa, Hujjatul Islam Walmuslimin Kazem Seddiqi amesema matamshi yasiyo ya kidiplomasia ya Trump ni kielelezo cha hasira na kuchanganyikiwa. 
Donald Trump
Hatibu wa Swala ya Ijumaa ya Tehran ameashiria kufeli kwa njama za Marekani katika eneo la Mashariki ya Kati na kusema: Katika miezi ya hivi karibuni Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, wapiganaji wa Hizbullah na Russia wametoa kipigo kikali kwa magaidi wanaoungwa mkono na kusaidiwa na Marekani na washirika wake. 
Hujjatul Islam Walmuslimin Seddiqi ameongeza kuwa, Daesh, al Qaida, Taliban na magenge mengine kadhaa ya kigaidi ni watoto wa Marekani na Saudi Arabia na kusisitiza kuwa: Nchi hizo mbili zimetumia mamilioni ya fedha za watu wao kwa ajili ya kuanzisha makundi kama hayo ya kigaidi. Amesema, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ni mapinduzi ya watu waliodhulumiwa kote duniani na kuongeza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu daima itaendelea kuwasaidia watu wa Iraq na Syria katika vita vyao dhidi ya magaidi. 
Magaidi wa Daesh wakiwamiminia risasi raia wa Iraq
Hatibu wa Swala ya Ijumaa ya Tehran pia amewapa mkono wa pole Waislamu kote duniani kwa mnasaba wa kuwadia mwezi wa Muharram na kusisitzia kuwa, Imam Hussein bin Ali (as) aliuawa katika mwezi huu katika mapambano yake dhidi ya mfumo na utawala wa kidhalimu na kibeberu.   

KAMANDA SALAMI: KUINGIA VITANI NA IRAN HAKUTAKUWA NA MATOKEO GHAIRI YA KUSHINDWA

Kamanda Salami: Kuingia vitani na Iran hakutakuwa na matokeo ghairi ya kushindwa
Naibu Kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran (SEPAH) sambamba na kusisitiza kuwa kuingia vitani na Iran hakuwezi kuwa na natija nyinginge ghairi ya kushindwa amesema kuwa Wiki ya Kujilinda Kutakatifu imeleta izza ya usalama kwa taifa hili.
Brigedia Jenerali Hussein Salami ameyasema hayo leo katika mji wa Gorgab wa mkoa wa Isfahan, katikati mwa Iran na kuongeza kuwa, kujilinda kutakatifu ni alama ya umoja wa taifa la Iran mkabala wa uistikbari wa dunia. Akibainisha kwamba Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imerithi utamaduni wa tukio la Ashura amesema kuwa, kile kinacholifanya taifa hili kuendelea kusimama imara dhidi ya Marekani, utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na washirika wao ni uimara na ushujaa wa wanaume na wanawake wa Iran walikokurithi kutoka utamaduni wa Ashura na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu. 
Brigedia Jenerali Hussein Salami
Naibu Kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran (SEPAH) amesema kuwa katika kipindi cha miaka minane ya kujitetea kutakatifu Iran ya Kiislamu ikiwa peke yake iliweza kuonyesha adhama yake mbele ya mabeberu wa dunia na kwamba baraka za kujitolea muhanga wanamapambano wa vita hivyo, ndiko kulikoliletea taifa la Iran ushujaa na uimara. Aidha ameashiria matamshi yasiyo ya kidiplomasia ya Rais Donald Trump wa Marekani katika Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) na kuongeza kuwa, umefika wakati kwa serikali ya Washington kujiepusha na upuuzi wa namna hiyo.

KIM JONG-UN: TRUMP ANA MATATIZO YA AKILI, NITAMFANYA AJUTIE MATAMSHI YAKE YA VITISHO

Kim Jong-un: Trump ana matatizo ya kiakili, nitamfanya ajutie matamshi yake ya vitisho
Kim Jong-un, Kiongozi wa Korea Kaskazini amejibu matamshi ya vitisho ya Rais Donald Trump wa Marekani na kusema kuwa, rais huyo wa Marekani ana matatizo ya kiakili na kwamba atalipa gharama ya matamshi yake ya vitisho dhidi ya Pyongyang.
Katika sehemu nyingine, kiongozi huyo wa Korea Kaskazini sambamba na kuashiria matamshi ya hivi karibuni ya rais wa Marekani aliyetishia kuishambulia Pyongyang amesema kuwa, nitamfanya kiongozi huyo wa Marekani ajutie matamshi yake aliyoyatoa katika mkutano mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) kwa kuitishia Korea Kaskazini.
Mgogoro kati ya Korea Kaskazini na Marekani wazidi kuongezeka, huku walimwengu wakimkosoa Trump
Itakumbukwa kuwa Jumatatu iliyopita katika mkutano huo wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Trump alizishambulia nchi kadhaa za dunia na kutoa vitisho dhidi ya nchi hizo badala ya kuzungumzia amani na usalama. Akiizungumzia Korea Kaskazini Trump alisema, Marekani italazimika kuiangamiza kikamilifu nchi hiyo ya Asia, isipokuwa kama Pyongyang itakubali kurudi nyuma kuhusiana na miradi yake ya silaha za nyuklia. Kadhalika rais huyo wa Marekani ambaye hadi sasa ameendelea kukosolewa duniani kutokana na matamshi yake yasiyo ya mantiki, alimtaja Kim Jong-un kwa jina la 'Mtu wa Makombora' na kuongeza kuwa, kiongozi huyo wa Korea Kaskazini anafanya mambo yatakayopelekea yeye, mfumo na raia wa nchi yake kujiangamiza.
Moja ya makombora yanayoitia kiwewe Marekani na kumfanya Trump atokwe na matamshi ya ajabu
Kama hiyo haitoshi usiku wa Alkhamisi ya jana Trump alisaini dikrii mpya ambayo inaitaka Wizara ya Hazina ya Marekani kuwawekea vikwazo watu au taasisi za kigeni zinazoshirikiana kibiashara na Korea Kaskazini. Kabla ya hapo pia Korea Kaskazini iliwekewa vikwazo vipya na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutokana na kuyafanyia majaribio makombora yake ya balestiki na silaha za nyuklia. Pyongyang imekuwa ikisisitiza kuwa, itaendelea kujiimarisha kijeshi ili kukabiliana na chokochoko za Marekani na washirika wake dhidi yake.

KAMAND WA JESHI LA ISRAEL: NI VIZURI ISRAEL IENDELEE KUJIEPUSHA KUINGIA VITANI NA HIZBULLAH

Kamanda wa jeshi la Israel: Ni vizuri Israel iendelee kujiepusha kuingia vitani na Hizbullah
Mkuu wa Majeshi ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel amesema kuwa, ni kwa maslahi ya utawala huo ikiwa utaendelea kujitenga mbali na vita vyovyote na Harakati ya Kiislamu ya Hizbullah ya nchini Lebanon.
Gadi Eizenkot, aliyasema hayo jana Alkhamisi katika mahojiano na mtandao wa habari wa Kizayuni wa Walla na gazeti la utawala huo la Yedioth Ahronoth na kuongeza kuwa, harakati ya Hizbullah ndio adui mkubwa na hatari anayeitia wasi wasi mkubwa Israel, hasa kwa kuzingatia kuwa ina uwezo mkubwa wa kijeshi huku ikiwa na ngome kadhaa za kijeshi Lebanon na Syria kiasi cha kuifanya iwe jeshi kubwa.
Askari wa Israel wakilia mithili ya watoto baada ya kushindwa katika vita vya mwaka 2006 na Hizbullah
Amesisitiza kuwa, harakati hiyo ya muqawama imekuwa ikipambana nchini Syria kwa miaka kadhaa sasa huku ikiwa na vikosi kamili vya kivita sambamba na kutoa misaada ya kijeshi na intelejensia za kivita kwa jeshi la Syria. Ameongeza kuwa, hata kama jeshi la Israel lina nguvu, lakini linatakiwa liendelee kujizuia kuanzisha vita vyovyote na harakati hiyo ya Kiislamu. Mkuu wa Majeshi ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel sambamba na kujaribu kuwapa utulivu Wazayuni kwamba hivi sasa  eti ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu ( Israel) kuna usalama na kwamba, jeshi la Israel limejiandaa kukabiliana na aina yoyote ya changamoto na tishio dhidi yake, amesema kuwa, ni lazima utengamano uliopo kwa sasa uendelee kuwepo badala ya kuingia vitani na Hizbullah.
Wanamapambano wa muqawama wa Hizbullah
Itakumbukwa kuwa katika vita vya siku 33 vya mwaka 2006 kati ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na harakati ya muqawama ya Hizbullah, Israel ilipata hasara kubwa na kulazimika kurudi nyuma. Katika sehemu nyingine Gadi Eizenkot amesema kuwa uwepo wa serikali ya mamlaka ya ndani ya Palestina inaoongozwa na Mahmoud Abbas ni kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni kwa kuwa kuna mahusiano mazuri ya kiusalama kati ya Israel na serikali hiyo.

Saturday, September 16, 2017

CHAMA TAWALA BURUNDI KIMELALAMIKIA RIPOTI YA UN KUHUSU HAKI ZA BINADU

Chama tawala nchini Burundi kimelalamiria ripoti ya Umoja wa Mataifa iliyoitaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) ifanye uchunguzi kuhusu jinai zilizofanywa na viongozi wa Burundi dhidi ya raia wa nchi hiyo.
Chama tawala Burundi jana kilieleza kuwa ripoti ya Umoja wa Mataifa inayosema kuwa viongozi wa Burundi wamehusika katika kukiuka haki za raia wake kuwa ni ripoti ya kisiasa na yenye lengo la kutoa pigo kwa chama hicho tawala. 
Kuhusiana na suala hilo Evariste Ndayishimiye Katibu Mkuu wa chama tawala cha Burundi amezishambulia kwa maneno Umoja wa Mataifa na Umoja wa Ulaya  kufuatia ripoti hiyo yenye kukinzana dhidi ya viongozi wa Burundi na kuitaja Ulaya na nchi za magharibi kuwa ni mashetani wa Ulaya.
Evariste Ndayishimiye Katibu Mkuu wa chama tawala Burundi, CNDD-FDD  
Maafisa wa uchunguzi wa Umoja wa Mataifa tarehe Nne mwezi huu wa Septemba waliitaka mahakama ya ICC ichunguze jinai zilizofanywa na viongozi wa serikali ya Burundi dhidi ya raia wa nchi hiyo yakiwemo mauaji ya kunyonga nje ya mkondo wa sheria, utiaji mbaroni kiholela, mateso, ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia. Burundi ilitumbia katika mgogoro wa kisiasa tangu mwezi Aprili mwaka 2015 kufuatia hatua uya Rais Pierre Nkurtunziza wa nchi hiyo ya kuamua kugombea kiti cha urais kwa muhula wa tatu kitendo ambacho kimepingwa na wapinzani wa Burundi wakisema kuwa ni kinyume na katiba. 

UTURUKI YAILALAMIKIA UJERUMANI KUHUSU MKUTANO WA WAKURDI

Uturuki imemuita balozi wa Ujerumani nchini  humo jana Jumamosi(16.09.2017) kuhusiana na kile ilichosema ni mkutano wa wanamgambo wa Kikurdi  mjini Kolon, wizara  ya  mambo ya kigeni imesema.

Alewiten und Kurden demonstrieren in Köln gegen Erdogan (picture-alliance/AP Photo/M. Meissner)
Wizara ya  mambo  ya  kigeni imeeleza  hayo  katika  taarifa  inayoashiria kuchafuka  zaidi kwa  uhusiano  kati ya  mataifa  hayo washirika  wa  NATO.
"Tunashutumu  kufanyika  kwa  mkutano  katika  mji  wa  Kolon  nchini Ujerumani  wa kundi la  kigaidi  la PKK, na kuruhusu propaganda za  kigaidi.
Tumeeleza hisia  zetu  kwa  nguvu  kabisa  kwa  balozi  wa Ujerumani  mjini Ankara, ambae  aliitwa  katika  wizara  ya  mambo  ya  kigeni," taarifa  ilisema.
Kurdisch Hungerstreik Geschichte Abdullah Ocalan (Diego Cupolo)
Wakurdi katika tukio la utamaduni mjini Kolon
Taarifa  hiyo  ilionekana  kuzungumzia  kuhusu  maandamano  ya  Septemba 3 wakati  kiasi  ya  Wakurdi 25,000 waliandamana  mjini  Kolon  dhidi  ya  rais wa  Uturuki  Recep Tayyip Erdogan, baadhi  wakibeba  mabango  yenye picha  ya  Abdullah Ocalan, kiongozi  wa   chama  cha  Wafanyakazi  wa Kikurdi, PKK, ambacho  kimeorodheshwa  kama   kundi  la  kigaidi  na  Umoja wa  Ulaya  na  Marekani, na  kimepigwa  marufuku  nchini  Ujerumani.
Uturuki  imekuwa  ikiishutumu  Ujerumani  kwa  kutofanya  vya  kutosha kuzuwia  wanaharakati  wa  PKK.
Watu 14,000  walishiriki  katika  sherehe  za  kitamaduni  za  Wakurdi, ambazo  zilichukua kauli  mbiu  ya "Uhuru kwa  Ocalan, mamlaka  kwa Wakurdi," kituo cha  televisheni  cha  WDR kimeripoti.
Paris Kurden Demonstration gegen Erdogan (picture-alliance/AP Photo/Francois Mori)
Maandamano ya Wakurdi dhidi ya rais Erdogan
Kauli mbiu za PKK
Kauli  mbiu  hiyo  inamuhusisha  Abdullah Ocalan , kiongozi  aliyeko kifungoni  wa  chama  kilichopigwa  marufuku  cha  Wafanyakazi  wa  Kikurdi PKK, kundi  lililoorodheshwa  kuwa  ni  kundi  la  kigaidi  nchini  Uturuki  na Umoja  wa  Ulaya. Majeshi  ya  Uturuki  yamo  katika mzozo wa  muda  mrefu na kundi  la  PKK  upande  wa  kusini  mashariki  mwa  nchi  hiyo.
Wizara  ya  mambo  ya  kigeni  ya  Ujerumani  haikujibu  ombi  la  shirika  la habari  la  dpa  kutaka  kuzungumzia  hatua  iliyochukuliwa  na  Uturuki kumuita  balozi  wa  Ujerumani. Katika  taarifa  iliyotolewa  jana  Jumamosi , wizara  ya  mambo  ya  kigeni  ya  Uturuki  lisema  inashutumu  tukio  la  mjini Kolon, na  kudai kwamba  "propaganda  ya  ugaidi  ilifanyika  katika  tukio  hilo na  kundi  lenye  mahusiano  na  kundi  la   kigaidi  la  PKK nchini  Ujerumani, na  kwamba  picha  za  Ocalan zilioneshwa, kitu  ambacho  ni  kinyume  na sheria.
Gazeti  la  mjini  Kolon  la  Express limeripoti kwamba  kabla  ya maandamano  kuanza  polisi  mwanamke  mwenye  umri  wa  miaka  24 alipata  majeraha  kichwani  na  alilazimika  kupelekwa  hospitali. Polisi  pia walikamata  bendera na  kutoa onyo  rasmi kwa  washiriki , Express  lilisema.
Hii  ni  mara  ya  pili mwaka  huu ambapo  Uturuki  ilimwita  balozi  wa Ujerumani  nchini  humo  kuhusiana  na  maandamano  ya Wakurdi  nchini Ujerumani.
Deutschland Kurden demonstrieren in Köln (picture-alliance/dpa/M. Hitij)
Maandamano ya wakurdi mjini Kolon
Baada  ya  maandamano  ya  mamia  kwa  maelfu  ya  Wakurdi mjini Frankfurt  mwezi  Machi, polisi  ilifanya  uchunguzi. Walisema  katika  wakati huo  hawakuingilia  maandamano  hayo  ili kuepusha  kuchochea  ghasia.
Wakurdi  ni  asilimia  15  ya  idadi  ya  watu  nchini  Uturuki na mara  kadhaa hushutumu  kile  wanachokiona  kuwa  ni  ubaguzi unaofanywa  na  serikali. Chama  cha  PKK , ambacho  kimekuwa  kikipigana  na  serikali  ya  Uturuki kwa  zaidi  ya  miaka  30, kimeelezwa  kuwa  ni  kundi  la  kigaidi  nchini Ujerumani  tangu  mwaka  1993.

SPIKA WA BUNGE LA IRAN: UTATUZI WA SUALA LA UGAIDI UNAHITAJIA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, utatuzi wa suala la ugaidi unahitajia ushirikiano wa kimataifa.
Dakta Ali Larijani alisema hayo jana katika mkutano wake na waandishi wa habari akiwa pamoja na Siegfried Bracke, Spika wa Bunge la Ubelgiji ambapo alisisitiza juu ya kuweko ushirikiano kati ya Tehran na Brussels katika nyanja mbalimbali hususan katika migogoro ya Mashariki ya Kati ikiwemo ya Yemen na Myanmar.
Spika Larijani amesema kuwa, ana matumaini Mabunge ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Ubelgiji yatapanua zaidi wigo wa mazungumzo na ushirikiano hususan katika masuala ya haki za binadamu. Aidha amesema kwamba, ana matarajio safari ya Spika wa Bunge la Ubelgiji hapa Tehran itafungua zaidi milango ya ushirikiano wa kiuchumi na masuala mengine.
Dakta Ali Larijani, Spika wa Bunge la Iran
Kwa upande wake Siegfried Bracke Spika wa Bunge la Ubelgiji sambamba na kuashiria kwamba, nchi yake haikubaliani na siasa zote za Marekani amesisitiza kwamba, ofisi ya Umoja wa Ulaya inapaswa kufunguliwa haraka iwezekanavyo mjini Tehran.
Spika wa Bunge la Ubelgiji sambamba na kukaribisha kwa mikono miwili ustawishaji ushirikiano na Iran amesisitiza juu ya kuondolewa vizingiti vilivyoko katika uwanja huo.
Kadhalika Siegfried Bracke sanjari na kuashiria kwamba, viongozi wa Iran na Ubelgiji wanaona kuna umuhimu wa kustawishwa zaidi ushirikiano wa pande mbili katika vita dhidi ya ugaidi amesema kuwa, polisi wa pande mbili wamekuwa na mazungumzo ya ngazi za juu kabisa.

PAPA HAENDI DRC MPAKA UCHAGUZI UFANYIKE

Mwakilishi wa kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Francis, katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, anasema kiongozi huyo hatoizuru nchi hiyo hadi hapo uchaguzi uliocheleweshwa kwa muda mrefu utakapofanyika.

Vatikan Papst Franziskus hält Pfingsrede vor dem Petersdom (picture-alliance/dpa/S. Spaziani)
Mwezi Machi mwaka huu, Papa Francis alifuta ziara yake ya Kinshasa iliyokuwa ifanyike wakati wa majira ya joto kutokana na mzozo wa kisiasa, ingawa alikutana na Rais Joseph Kabila mjini Vatican mwaka uliopita.
Monsinyoo Luis Mariano Montemayor amenukuliwa jana akisema Papa Francis anasikitishwa na hali inayoendelea kati ya viongozi kisiasa na wananchi wake.
Kauli hiyo ameitoa baada ya kulizuru jimbo la Kasai lenye utajiri wa madini ya almasi, ambako mashirika ya chakula ya Umoja wa Mataifa yameonya kuwa mamilioni ya watu wanakabiliwa na njaa kutokana na mzozo huo.
Kanisa Katoliki lina ushawishi mkubwa katika nchi hiyo yenye watu milioni 70 ambako nusu yake wanaifata imani ya kanisa hilo na mwezi Desemba mwaka uliopita lilikuwa mpatanishi katika mazungumzo ya kitaifa kati ya serikali na vyama vya upinzani, ambayo yanatarajiwa kuifanya nchi hiyo kufanya uchaguzi wake kabla ya kumalizika kwa mwaka huu.

KOREA KASKAZINI YAZIDI KUIONYESHA DUNIA UBABE

Korea Kaskazini imefanya jaribio lingine la kombora lililopita kaskazini mwa Japan kabla ya kutua katika bahari ya Pacific, na kusababisha ukosoaji kutoka jumuiya ya kimataifa. Kombora hilo linaweza kufika hadi km 5000.

Nordkorea Diktator Kim Jong-un (Reuters/KCNA)
Waziri wa ulinzi wa Japan Istunori Onodera, aliwaambia waandishi habari kuwa umbali wa kombora hilo ungetosha kulifikisha katika kisiwa cha Marekani cha Guam kilichoko katika bahari ya Pacific, na kwamba ufatuaji huo ulilenga kujaribu ufanisi wa kombora hilo jipya na umbali linaloweza kuruka.
Maafisa wa ulinzi wa Japan wanaamini kombora hilo lina uwezo wa kufika umbali wa hadi kilomita 5,000.
Jaribio la Ijumaa limekuja chini ya wiki mbili tangu Korea Kaskazini ilipofanya jaribio lake la sita la kombora la nyuklia ambalo lilielezwa kuwa lenye nguvu zaidi, na siku moja baada ya serikali mjini Pyongyang kutoa vitisho dhidi ya Marekani na washirika wake, ikiwemo Japan.
Japan Verteidigungsminister Itsunori Onodera Reaktion auf Nordkorea Raketenabschuss (Getty Images/AFP/T. Kitamura)
Waziri wa ulinzi wa Japan Itsunori Onodera akizungumzia jaribio la karibuni zaidi la kombora la Korea Kaskazini, 15.09.2017.
Baraza la usalama laitisha kikao cha dharura
Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa liliitisha kikao cha dharura siku ya Ijumaa, kilichoombwa na Marekani na Japan.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelaani jaribio hilo, na katika taarifa aliyoitoa leo, ameutolea wito uongozi wa Korea Kaskazini kukoma kufanya majaribio mengine, kuheshimu maazimio ya Umoja wa Mataifa, na kutoa nafasi ya kuanzisha tena majadiliano ya dhati kuhusu uondoaji wa silaha zake za nyuklia.
Waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe, alisema serikali ya Tokyo haiwezi kuvumilia kitendo cha kuudhi kama hicho.
Naye rais wa Korea Kusini Moon Jae in alisema katika taarifa kuwa uchokozi unaojirudia wa Korea Kaskazini ni kitisho kikubwa kwa kwa rasi ya Korea, na kwa amani na usalama wa jumuiya ya kimataifa.
Katibu Mkuu wa jumuiya NATO Jens Stoltenberg alisema alilielezea jaribio hilo kama ukiukaji mwingine wa kizembe wa maazimio ya Umoja wa Mataifa unaohitaji kuitikiwa kimataifa.
China: Alieanzisha mzozo aumalize
Kwa upande wake, China, ambayo ni jirani mwenye uhusiano wa kiuchumi na Korea Kaskazini, ililaani jaribio hilo na kusema linakiuka maazimio ya Umoja wa Mataifa, lakini ilipinga madai kuwa yenyewe ndiyo inahusika na kushamiri kwa mzozo katika eneo hilo. Hua Chunying ni msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje ya China.
Nordkorea feuert erneut Rakete über Japan hinweg (Reuters/Kim Hong-Ji)
Raia wa Korea Kusini wakiangalia ripoti ya habari juu ya Korea Kaskazini kurusha kombora lililopita katika anga ya Japan.
"Suala la nyuklia la Korea Kaskazini ni la kiusalama zaidi na kiini chake ni tofauti kati ya Korea Kaskazini na Marekani. China siyo mlengwa katika suala hilo na haihusiki na kuongezeka kwa mgogoro huo," alisema Hua Chunying, msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje ya China na kuongeza kuwa, alieanzisha matatizo ndiye anaepaswa kuyamaliza.
Urusi pia ililaani jaribio hilo, huku msemaji wa ikulu ya Kremlin Dmitry Peskov akilitaja kama uchokozi utakaosababisha kuongezeka kwa mzozo katika rasi ya Korea. Urusi na China, ambazo zina uhusiano wa karibu na Korea Kaskazini, zote ni wanachama wa kudumu wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa.
Baraza liliiwekea Korea Kaskazini vikwazo vipya siku ya Jumatatu, kuhusiana mipango yake ya nyuklia na makombora, hii ikiwa ni juu y avikwazo vingine ilivyowekewa wiki tano zilizopita, ambavyo vilitarajiwa kupunguza karibu dola bilioni moja kutoka mapato ya dola bilioni tatu yatokanayo na mauzo ya nje.

KIWANGO CHA HATARI CHAPANDISHWA BAADA YA SHSMBULIO LONDON

Uingereza  imepandisha kiwango cha  kitisho cha mashambulizi ya  kigaidi, ikiwa  na  maana  kwamba shambulio jingine  linaweza kutokea wakati wowote.

London Anschlag auf Underground Ubahn (picture alliance/AP Photo)
Kundi linalojiita  "Dola la  Kiislamu" limesema  linahusika  na shambulio  hilo ambalo watu 29 wamejeruhiwa  katika  kituo cha treni kilichokuwa na watu wengi cha chini  ya  ardhi mjini London.
Polisi ya Uingereza imeanza kazi ya kumtafuta mtu aliyehusika na shambulio hilo jana kufuatia shambulio  la kigaidi katika kituo  cha  treni  mjini  London. Kitu  ambacho kilifichwa  ndani  ya ndoo  ya  plastiki pamoja  na  mfuko wa kununulia  vitu unaotumika  kwa kuwekwa  katika friji uliripuka ndani ya behewa  la  treni lililojaa  watu , na kuwajeruhi 29, wengi  wao  kwa  kuungua.
England Theresa May verlässt die Downing Street in London (REUTERS/T. Melville)
Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May
"Bila shaka, hiki  kilikuwa  kitu  ambacho  kilikusudiwa kusababisha  madhara  makubwa,"  waziri  mkuu Theresa May  alisema  baada  ya  kuitisha  mkutano  wa  kamati  ya serikali  ya  kuchukua  hatua  za  dharura inayojulikana kama COBRA.
Baadaye jana, May  alisema  kiwango  cha  hatari  kwa nchi  hiyo  kimepandishwa  kutoka  hali  mbaya  na kwenda  juu  zaidi hadi  hali  mbaya  sana, ambayo  ina maana  shambulio  linatarajiwa  wakati  wowote.
"Umma  utashuhudia  polisi  wengi  zaidi  katika  mfumo wa  usafiri  na  katika  mitaa  yetu  wakitoa  ulinzi wa  ziada ," May  amesema.
"Hii  ni  hatua  sahihi  na  inayoeleweka  ambayo  itatoa uhakikisho  wa  ziada  na  ulinzi wakati  mchakato  wa uchunguzi  ukiendelea."
London Explosion in Bahn der Underground (picture-alliance/AP Photo/V. Jones)
Kamishna msaidizi wa polisi mjini London Mark Rowley akizungumza na waandishi habari kuhusu shambulio mjini humo
Kundi linalojiita "Dola la Kiislamu"
Kundi linalojiita  Dola  la  Kiislamu  limedai  kundi linalojihusisha  na  kundi  hilo linahusika  na  shambulio hilo, kwa  mujibu wa  kitengo  cha  propaganda  cha  kundi hilo  cha  Amaq. Ofisa  anayehusika  na  kupambana  na ugaidi  nchini  Uingereza  amesema  kundi  la  IS  mara nyingi  hudai  kuhusika  na  mashambulio  ambayo hayajahusika  kabisa  na  kundi  hilo  na  kwamba  maafisa wanatafuta washukiwa  na  vitu  vinavyoweza kusababisha kupatikana kwao.
Watu walioshuhudia  wamesema  kwamba  majeraha yaliyasabishwa  na  mripuko  wenyewe, wakati  kwa wengine yalisababishwa  na  mkanyagano  uliofuatia wakati  abiria  wa  treni  wakijaribu kuharakisha  kutoka  nje ya  kituo  hicho ambacho  kwa  kawaida  kinatumiwa  na watu  wachache.
London Anschlag auf Underground Ubahn (picture-alliance/AP Photo/K. Wigglesworth)
Uchunguzi umeanza kubaini utambulisho wa mshambuliaji
Wengine  wanaeleza  kwamba  "mtafaruku ulitokea" wakati mamia  ya  watu  wakijaribu  kukimbia  moto.
"Nilikandamizwa  katika  ngazi. Watu  walikuwa wakiniangukia , watu walizimia, wakilia, kulikuwa  na watoto  wadogo waking'ang'ania  mgongoni  mwangu," Ryan Barnett  mwenye  umri  wa  miaka  25  aliliambia shirika  la  habari  la The Associated Press.
Polisi ya  Uingereza  imesema  mamia  ya  wapepelezi wanafanya  mahojiano ya  dharura  kutaka  kujua utambulisho  wa  mshambuliaji  na  wanasaidiwa  na kitengo  cha  ujasusi.

KUCHANGANYIKIWA SERIKALI YA TRUMP KUHUSIANA NA IRAN

Sambamba na kutangazwa majina mapya ya raia na mashirika ya Iran ambayo yameongezwa kwenye orodha ya vikwazo ya Marekani, serikali ya nchi hiyo kwa mara nyingine tena imeakhirisha vikwazo vya nyuklia dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa siku nyingine 120.
Hatua hiyo kwa upande mmoja inaongeza majina ya raia na mashirika ya Kiirani yatakayowekwa kwenye orodha iliyotajwa na wakati huohuo kuilazimisha Marekani kufungamana na ahadi ilizotoa kuhusu mapatano ya nyuklia kati ya Iran na nchi sita kubwa za dunia ikiwemo Marekani yenyewe, mazungumzo yanayojulikana kwa ufupisho wa JCPOA. Hata hivyo Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani imesisitiza kwamba hatua hiyo haipaswi kuchukuliwa kuwa ni alama ya serikali ya Rais Donald Trump wa nchi hiyo kubadili msimamo wake kuhusiana na mapatano hayo ya nyuklia. Katika miezi ya hivi karibuni serikali ya Trump imekuwa na msimamo unaogongana kuhusiana na mapatano hayo.
Nchi zilizotia saini mapatano ya nyuklia ya JCPOA
Viongozi wa serikali hiyo akiwemo Trump mwenyewe pamoja na Nikki Haley, mwakilishi wake wa kudumu katika Umoja wa Mataifa, licha ya kudai kuwa Iran imekiuka moyo wa mapatano ya JCPOA na hivyo kusisitiza udharura wa kuangaliwa upya mapatano hayo, lakini wakati huohuo serikali ya Washington imeamua kuakhirisha vikwazo vya nyuklia dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa siku 120. Suala hilo linathibitisha wazi kwamba miaka miwili baada ya kuanza kutekelezwa mapatano ya JCPOA kati ya Iran na kundi la 5+1 na wakati huohuo kuthibitishwa mara kadhaa kuwa Iran imetekeleza ahadi zake zote, Marekani bado imechanganyikiwa na kushindwa kabisa kutekeleza hata moja ya ahadi muhimu ilizotoa kuhusiana na mapatano hayo ya kimataifa.
Kuchanganyikiwa huko pia kunatokana na migongano ya kisiasa inayooneka wazi ndani ya Marekani. Kuna kundi la wanasiasa nchini Marekani ambalo linadai kwamba kutokana na kuwa matarajio ya nchi hiyo ya kuiona Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inabadili misimamo yake juu ya masuala kama vile makombora na siasa zake za kieneo hayajafikiwa, Washington inapasa kuendelea kupuuza mapatano ya JCPOA na hata kujitoa kwenye mapatano hayo bila kujali malalamiko na ukosoaji wa walimwengu.
Rais Trump, aliyechanganyikiwa kuhusiana na mapatano ya JCPOA
Hii ni pamoja na kuwa matamshi ya kutowajibika ya Trump katika kipindi cha kampeni zake za uchaguzi na baada ya kuingia ikulu ya White House yameiweka pagumu serikali yake kuhusiana na mapatano ya JCPOA. Pamoja na hayo, kundi jingine kubwa la wanasiasa na wataalamu wa Marekani linaamini kwamba ni vigumu kuendelea kutoa madai kuwa Iran imekiuka mapatano hayo au kutotekeleza ahadi zake katika hali ambayo Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia IAEA daima umekuwa ukitoa ripoti zinazothibitisha kwamba Iran imefungamana na kutekeleza kikamilifu ahadi zake zote kuhusu mapatano hayo ya kimataifa.
Makao makuu ya IAEA mjini Vienna, Austria
Hii ni pamoja na kuwa uungaji mkono mkubwa wa karibu pande zote za Ulaya, Russia, China na Umoja wa Mataifa kwa mapatano hayo unaendelea kuisukuma nchi hiyo katika ukingo wa kutengwa kisiasa kimataifa. Kwa msingi huo licha ya kundi hilo kuendelea kuituhumu Iran juu ya masuala yasiyohusiana na Mapatano ya JCPOA lakini linaitaka serikali ya Washington kuheshimu mapatano hayo. Kwa kuzingatia suala hilo, serikali hiyo imeamua kuakhirisha vikwazo vya nyuklia kwa kipindi kingine cha siku 120 ili kuliridhisha kundi la pili na wakati huohuo kuongeza majina ya raia na mashirika mapya ya Iran kwenye orodha ya vikwazo vyake vingine ili kuliridhisha kundi la kwanza; suala ambalo linabainisha wazi kuchanganyikiwa kwa Wamarekani kuhusiana na Iran.

HUFFINGTON POST: WAMAREKANI NI WABAGUZI

Matokeo ya uchunguzi wa taasisi mbili za kisayansi za Marekani yanaeleza kuwa, watu wengi wa nchi hiyo wana mielekeo ya kibaguzi licha ya kutoa madai ya kupinga fikra ya kuwatambua wazungu kuwa ndio wanadamu walio juu na bora kuliko wengine.
Gazeti la Huffington Post linalochapishwa nchini Marekani limeripoti kuwa, matokeo ya uchunguzi wa maoni uliofanywa kwa pamoja na taasisi ya Ipswich na Chuo Kikuu cha Virginia yameonesha kuwa, ingawa idadi ya waungaji mkono wa manazi mamboleo na fikra kwamba wazungu wako juu na ni bora zaidi kuliko wanadamu wengine, lakini baadhi ya fikra na mitazamo ya kibaguzi na ya kufurutu mipaka inaungwa mkono kwa wingi nchini humo. 
Uchunguzi huo wa maoni ulifanyika kuanzia tarehe 21 Agosti hadi tarehe 5 Septemba, yaani wiki kadhaa tu baada ya mapigano ya wabaguzi wa rangi katika jimbo la Virginia.
Maandamano ya kupinga ubaguzi nchini Marekani
Matokeo ya uchunguzi huo pia yameonesha kuwa, asilimia 8 ya washiriki wamesema kuwa, wanaiunga mkono harakati ya kitaifa ya wazaungu wabaguzi na kwamba asilimia 39 kati yao wanaamini kuwa, wazungu wanashambuliwa nchini Marekani!
Uchunguzi huo umebaini kuwa, mtu mmoja kati ya kila Wamarekani sita anaamini kwamba, ndoa zinapaswa kufanyika baina ya watu wa mbari moja na si kwa mfano kati ya Wamarekani weusi na wazungu.  
Kyle Kondick Mkurugenzi wa Mahusiano ya Kisiasa wa Chuo Kikuu cha Virginia anasema matokeo ya uchunguzi huo yanaonesha kuwa, jamii ya Marekani ina mitazamo inayokubali ubaguzi wa rangi.    

IRAN; MOJAYA MADOLA MANNE YANAYOONGOZA KATIKA TEKNOLOJIA YA SATALAITI DUNIANI

Nguvu na uwezo wa kielimu sambamba na nguvu za kiulinzi na makombora ni miongoni mwa mambo muhimu yanayojenga nguvu na uwezo wa taifa lolote katika zama hizi; na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, kwa upande wake imepiga hatua nzuri katika uga wa nguvu na uwezo wa kielimu na kisayansi hususan katika teknolojia ya satalaiti.
Mshauri wa Kamanda Mkuu wa Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alitangaza siku ya Alkhamisi kuwa: Iran ni moja ya nchi nne duniani zinazoongoza katika nyanja zote za teknolojia ya satalaiti. Brigedia Jenerali Mohammad Hassan Nami amesema Iran inao utaalamu na uwezo mkubwa katika nyuga za teknolojia ya satalaiti ikiwemo vituo vya kurushia, mitambo ya kubebea angani, satalaiti zenyewe pamoja na vituo vya upokeaji na uongozaji.
Brigedia Jenerali Mohammad Hassan Nami
Mafanikio katika uga wa kutuma satalaiti angani sambamba na uwezo wa kuunda makombora ya aina mbalimbali yenye uwezo na malengo tofauti yameifanya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iwe na nguvu na uwezo katika nyanja za aina kwa aina. Kutengeza satalaiti na kuituma anga za mbali kwa kutumia maroketi ya kubebea satalaiti ni upeo wa juu kabisa wa utunishaji nguvu na misuli ya uwezo wa nchi yoyote ile katika uga wa teknolojia ya anga za mbali. Katika uwanja huo, Iran imetuma angani satalaiti mbalimbali kwa kutumia maroketi ya kubebea satalaiti; na hivi sasa ni miongoni mwa nchi nne zinazoongoza katika uga huo duniani ikiwa pia imo kwenye mikakati ya kutuma wanadamu katika anga za juu. Akizungumzia suala hilo, Fat-hollah Ummi, Mkuu wa kituo cha utafiti wa anga za mbali cha Wizara ya Sayansi, Utafiti na Teknolojia ya Iran alitangaza wiki iliyopita kwamba: "marubani wanne wenye uzoefu mkubwa hivi sasa wanapatiwa mafunzo makubwa na magumu ili hatimaye wawili miongoni mwao wachaguliwe kwa ajili ya kutumwa kuelekea anga za mbali".
Satalaiti ya Omid iliyotumwa na Iran katika anga za mbali
Kabla ya hapo, mnamo mwaka 2013, wanasayansi wa anga za juu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran walifanikiwa kutuma anga za mbali kima wawili waliopewa majina ya Aftab na Fargam; na kwa mujibu wa Fat-hollah Ummi hadi sasa kima hao wawili wangali hai; na wataalamu wa Kiirani wanafanya utafiti kuhusu athari za safari za anga za mbali kwa mtoto aliyezaliwa na kima hao.
Kwa kutegemea uwezo na utaalamu wake wa ndani na juhudi za waatalamu wake, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeweza kuwa moja ya mataifa yenye uwezo wa juu katika nyuga mbalimbali za teknolojia ya satalaiti. Kutokana na mafanikio makubwa iliyopata, kila pale inapotuma satalaiti kwa mafanikio kuelekea anga za mbali, maadui zake wakiongozwa na Marekani hushindwa kuvumilia jambo hilo. Kwa kutoa mfano, mnamo tarehe 27 Julai mwaka huu, Iran ilifanikiwa kurusha kwa mafanikio roketi la kubebea satalaiti la Simorgh katika kituo cha taifa cha anga za mbali cha Imam Khomeini (MA) kilichopo hapa mjini Tehran. Siku moja tu baada ya mafanikio hayo, yaani tarehe 28 Julai, Wizara ya Hazina ya Marekani ilitumia kisingizio cha kufanyiwa jaribio roketi la Simorgh ambalo lilihusu masuala ya utafiti tu na kisayansi, kuzijumuisha taasisi sita za Iran kwenye orodha ya vikwazo vyake dhidi ya taifa hili. Katika hatua nyengine inayofanana na hiyo, Alkhamisi ya tarehe 14 ya mwezi huu wa Septemba wizara hiyo iliongeza majina ya watu na mashirika mengine kadhaa ya Kiirani yanayohusika na masuala ya makombora kwenye orodha ya vikwazo dhidi ya Iran. Hatua hiyo ya serikali ya Washington inakinzana na sheria za kimataifa na hata makubaliano ya nyuklia na azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Akizungumza siku tatu zilizopita pembeni ya mkutano wake na Katibu Mkuu wa Shirikia la Ushirkiano wa anga za mbali la Asia na Oceania (APSCO), Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia za Mawasiliano wa Iran Mohammad Javad Azari Jahrami alisema: "Sekta ya anga za mbali haikuashiriwa kwa namna yoyote ile kwenye makubaliano ya nyuklia ya JCPOA, na hata katika azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama pia sekta ya satalaiti ya Iran haijawekewa mpaka wowote".
Rais Hassan Rouhani alipokagua uundaji wa roketi la Simorgh
Shughuli za satalaiti na utumaji wake kuelekea anga za mbali kwa malengo ya utafiti ni jambo la dharura na la kawaida kwa nchi yoyote ile. Kwa sababu hiyo, bila kujali hatua za kutapatapa zinazochukuliwa na Marekani, Iran ingali inaendelea kupiga hatua na kusonga mbele katika uga huo ambapo hivi sasa inajiandaa kutuma anga za mbali satalaiti nyengine mpya iliyopewa jina la "Satalaiti ya Urafiki". Kuwa na nguvu na uwezo katika sekta mbalimbali kumeifanya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iwe dola athirifu na lenye sauti katika eneo na ulimwenguni kwa jumla, ambapo licha ya kuandamwa na mashinikizo ya kisiasa na kiuchumi hivi sasa imekuwa moja ya madola yanayoongoza katika uga wa utaalamu wa makombora na satalaiti duniani.../