Thursday, February 16, 2017

KUNDI LA G20 LAKUTANA KUJADILI MISUKOSUKO YA DUNIA

Mawaziri wa kigeni wa nchi 20 zinazoongoza kiviwanda na kiuchumi wanakutana mjini Bonn Ujerumani, kuijadili njia za kuepukana na mizozo siku za mbele, huku kukiwa na wasiwasi juu ya muelekeo wa sera ya nje ya Marekani.
Deutschland G 20 Außenministertreffen in Bonn (picture-alliance/dpa/R. Vennenbernd)
Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani, Sigmar Gabriel, ambaye ndiye mwenyeji wa mazungumzo hayo ya siku mbili, amesema kwamba  kuchaguliwa Rais Donald Trump kunapaswa kuwa sawa na king'ora cha kuiamsha Ulaya, kukabiliana na changamoto zijazo. Waziri Gabriel aliliambia gazeti la kila siku la Ujerumani, Frankfuerter Allgemeine Zeitung, kwamba Umoja wa Ulaya unahitaji mageuzi, ikiwa unataka kweli kuwa na umuhimu mbele ya madola yenye nguvu kama Marekani, Urusi na China.
Sigmar Gabriel Bundesaußenminister (picture-alliance/dpa/A. Shcherbak) Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani, Sigmar Gabriel
Alisema tumekuwa tukiamini kwa muda mrefu, kwamba mwenendo wetu wa kuishi unalindwa vilivyo na Wamarekani, akimaanisha ushawishi wa Marekani kiutamaduni, diplomasia na kijeshi katika ulimwengu wa Magharibi baada ya vita vya pili vya dunia. Gabriel alisema wakati umewadia kwa Waulaya kusimamia maadili yao na ikihitajika hata kwa njia ya kijeshi, bila ya kutegemea msaada wa Marekani. Kwa kufanya hivyo kutasaidia kuondokana na shaka shaka zinazoongezeka kuhusu Ulaya, jambo ambalo limesababisha kufufuka kwa siasa za kizalendo barani Ulaya katika miaka ya hivi karibuni.
Mazungumzo miongoni mwa  kundi hilo la G20 la mataifa ya kiviwanda na yanayokuwa kiuchumi, yatatuwama katika kile kinachoitwa malengo 17 ya maendeleo endelevu yaliokubaliwa na Jumuiya ya Kimataifa yawe yamefikiwa ifikapo 2030. Lakini mazungumzo ya pembeni yalianza mapema asubuhi kabla ya kufunguliwa mkutano huo leo mchana. 
Deutschland G 20 Außenministertreffen in Bonn - Rex Tillerson (picture alliance/dpa/B. Smialowski) Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani, Rex Tillerson
Kwa upande wa waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani, Rex Tillerson, ambaye ujumbe wake umepiga kambi nje ya jiji la Bonn itakuwa ni nafasi yake ya kwanza kukutana na mawaziri kadhaa wa mambo ya nchi za nje, akiwemo, Sergei Lavrov, wa Urusi ambaye alipangiwa kukutana naye baadae leo. Tayari Tillerson alikutana kwa mara ya kwanza na mawaziri wenzake wa Saudi Arabia, Uingereza, Oman na Umoja wa Falme za Kiarabu. Mbali na mizozo duniani na njia ya kukabiliana nayo, masuala mengine katika ajenda ni kuanzia jinsi ya kulisaidia bara la Afrika, changamoto za mabadiliko ya tabianchi hadi vita nchini Syria wakati huu wa misukosuko katika maeneo mbalimbali duniani.
Mkutano huu wa Bonn, utakuwa  sawa na maandalizi ya mkutano wa viongozi wakuu wa taifa na serikali wa kundi hilo la G20, watakaokutana  katika mji wa bandari wa kaskazini mwa Ujerumani - Hamburg, mwezi Julai.

No comments:

Post a Comment