Monday, October 30, 2017

AMIR WA QATAR: IRAN NDIO NJIA PEKEE YA KUPITISHIA CHAKULA NA DAWA KATIKA KIPINDI CHA MZINGIRO

Amir wa Qatar: Iran ndio njia pekee ya kupitishia chakula na dawa katika kipindi cha mzingiro
Mfalme wa Qatar Sheikh Tamim bin Hamad Al Thani amesema Iran ndio njia pekee ya kupitishia chakula kwa ajili ya wananchi wa Qatar waliowekewa mzingiro; na akaongeza kwamba Saudi Arabia na nchi nyengine tatu za Kiarabu zinakula njama ya kuubadilisha utawala katika nchi yake.
Amir wa Qatar ameyasema hayo katika mahojiano na kanali ya televisheni ya CBS ya Marekani. Akijibu suali kuhusu dai kwamba Saudia na nchi nyengine tatu za Kiarabu zinaituhumu Doha kuwa ina urafiki wa kupita kiasi na Tehran, Sheikh Tamim Al Thani amesema: Iran ni jirani wa Qatar na serikali ya Doha ina uhusiano mpana wa kisiasa na Iran kuliko ilivyo na Saudia na waitifaki wake.
Mfalme wa Qatar amekumbusha matukio yaliyojiri miaka 21 nyuma na njama zilizofanywa kwa madhumuni ya kumpindua baba yake Shiekh Hamad bin Khalifa Al Thani na kuongeza kuwa: historia imeonyesha kuwa hapo kabla pia Saudi Arabia imefanya kila njia ili kuubadilisha utawala nchini Qatar.
Amir wa Qatar akimlaki Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif alipotembelea Qatar hivi karibuni
Kuhusiana na kuwepo ofisi za kundi la kigaidi la Taliban mjini Doha, Mfalme wa Qatar ameeleza kuwa: Marekani ilitutaka tuwapokee Taliban na kuliruhusu kundi hilo lifungue ofisi yake mjini Doha ili Marekani iweze kufanya mazungumzo nalo.
Mbali na kutangaza utayari wa kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na nchi nne zilizoiwekea vikwazo nchi yake ili kutatua mgogoro uliopo baina ya Doha na nchi hizo, Sheikh Tamim Al Thani amesema: Qatar inataka kumalizwa hitilafu zilizopo, lakini hakuna kitu chenye hadhi ya juu zaidi kuliko heshima na mamlaka ya kujitawala nchi hiyo.
Tangu tarehe 5 Juni mwaka huu, Saudi Arabia, Imarati (UAE), Bahrain na Misri zimevunja uhusiano wao wa kidiplomasia na Qatar kwa sababu ya misimamo ya Doha ambayo haiwiyani na sera za utawala wa Riyadh. Mbali na kuiwekea vikwazo, nchi hizo nne zimeifungia Qatar pia mipaka yao ya nchi kavu, baharini na angani.../

No comments:

Post a Comment