Sunday, October 8, 2017

MAELFU WAANDAMANAKUSHINIKIZA MUAFAKA CATALONIA

Malefu ya watu wameandamana Jumamosi katika miji mbalimbali ya Uhispania wakishinikiza kufanyika majadiliano kumaliza mgogoro wa jimbo la kaskazini-mashariki la Catalonia, linalotaka kujitenga.
Spanien Barcelona Demonstration in Weiß für Dialog (Getty Images/C. McGrath)
Wakiwa wamebeba mabango yenye ujumbe usemao "Hablamos?" na "Parlem?" - maneno ya Kikatalan na Kihispania yanayomaanisha "Tunaweza kuzungumza?" - waandamanaji hao walikusanyika majira ya saa sita mchana nje ya kumbi za miji ya Madrid na Barcelona, na pia katika miji ya Zaragoza, Seville na Bilbao.
"Ahsanteni kwa kuujaza uwanja wa Cibeles mjini Madrid na kumbi kadhaa za miji kote Uhispania. Sasa tuwaache wanasiasa wafanye kazi yao, hicho ndicho tunachowalipia mishahara," waliandika waandaji wa maandamano hayo kwenye ukurasa wao wa Facebook.
Hashtag ya #parlemhablemos ndiyo mada iliyohanikiza kwenye mtandao wa Tweeter. Kabla ya maandamano ya Jumamosi, ambako watu waliombwa kuvaa nguo nyeupe kuepusha kaulimbiu au nyimbo za vyama, waandaaji walisambaza ilani iliosoma: "Tunajua inawezekana kuishi pamoja. Uhispania ni bora kuliko watawala wake na imeonyesha hili mara nyingi."
"Tulikuwa na wasiwasi kuhusu mwelekeo wa kisiasa katika siku hizi zilizopita. Zilikuwa zinaelekea kwenye mkwamo," mmoja wa waandaji wa maandamano hayo Pablo Fernandez aliliambia shirika la habari la Ujerumani dpa.
Spanien Barcelona Demonstration für Dialog (Reuters/E. Gaillard) Watu wakishiriki maandamano kuunga mkono majadiliano katika uwanja mjini Barcelona, Uhispania Oktoba 7, 2017.
Mjini Madrid, kulikufanyika pia mkutano wa kupinga kujitenga katika eneo la Plaza de Colon, ulioandaliwa na wakfu wa kizalendo wa ulinzi wa taifa la Uhispania wa DENAES. Mkutano huo ulihudhiriwa na watu karibu 50,000," kwa mujibu wa duru rasmi. Watu walikuwa wakiimba nyimbo za "Idumu Uhispania," "Adumu Mfalme" na "Catalonia pia ni Uhispania."
Maandamano kuendelea Jumapili
Maandamano mengine makubwa ya kupinga uhuru wa Catalonia yamepangwa kufanyika siku ya Jumapili mjini Barcelona yakiitwa "Inatosha! Turudi kutumia akili." Maandamano hayo yaamepangwa kufungwa kwa hotuba ya mwandishi habari alieshinda tuzo ya amani ya Nobel na mwandishi vitabu Mario Vargas Llosa.
Oktoba 1, Catalonia iliitisha kura ya maoni kuamua juu ya uhuru wake ambapo asilimia 90 ya walioshiriki waliunga mkono kujitenga na Uhispania, ingawa uitikiaji wa kura hiyo ulikuwa ni asilimia 43 ya watu wanaostahili kupiga kura.
Tangu wakati huo, Uhispania imetumbukia katika mgogoro mkubwa zaidi wa kisiasa kuwahi kuikumba katika kipindi cha miongo kadhaa, huku serikali ya jimbo la Catalonia ikionekana kutangaza uamuzi wa upande mmoja wa uhuru licha ya hatua hiyo kupigwa marufuku na Mahakama ya Katiba ya Uhispania na serikali kuu mjini Madrid.
Spanien Madrid Demonstration gegen Unabbhähigkeit Kataloniens (Getty Images/AFP/J. Soriano) Mjini Madrid, waandamanaji wakipeperusha bendera za Uhispania wakati wa maandamano yalioitishwa na Wakfu wa DENAES wa ulinzi wa taifa la Uhispania, katika uwanja wa Colon, 07.10.2017.
Merkel, Juncker wazungumzia mgogoro huo
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na rais wa Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Jean-Claude Juncker waliujadili mzozo huo katika mazungumzo kwa njia ya simu siku ya Ijumaa.
Mashaka yatokananyo na mzozo huo yameyalaazimu makampuni kadhaa ya kibiashara na mabenki kuhamisha shughuli zake nje ya Catalonia na kuzipeleka katika maeneo mengine ya Uhispania katika siku za karibuni.
Kikao cha bunge la jimbo la Catalonia kilichokuwa kimepangwa kufanyika siku ya Jumatatu, na ambacho kilitarajiwa kuhusisha tangazo la upande mmoja la uhusu, kimefutwa baada ya kupigwa marufu na mahakama ya juu ya nchi hiyo.
Serikali ya Uhispania na polisi yake wamekosolewa vikali kutokana na ukandamizaji wa vurugu wa polisi siku ya kura, ambayo ilikuwa tayari imetangazwa kuwa haramu na mahakama ya katiba, na ilikuwa imepingwa vikali na serikali kuu mjini Madrid.

No comments:

Post a Comment