Sunday, October 8, 2017

KUKATAA TENA MAREKANI KUTIA SAINI MKATABA WA KUPIGA MARUFUKU SILAHA ZA NYUKLIA

Kukataa tena Marekani kutia saini mkataba wa kupiga marufuku silaha za nyuklia
Kwa mara nyingine tena, Marekani imekataa kutia saini makubaliano ya kupiga marufuku silaha za nyuklia ikisisitiza kuwa Washington haina mpango kabisa wa kujiunga na makubaliano hayo yanayoungwa mkono wa washindi wa tunzo ya Nobel.
Muda mchache tu baada ya kutangazwa washindi wa tunzo ya amani ya Nobel mwaka 2017, msemaji wa Ikulu ya Marekani (White House) alisema, hakuna mabadiliko yoyote katika msimamo wa Marekani wa kukataa kujiunga na makubaliano ya kupiga marufuku silaha za nyuklia. Alisema, Marekani inaamini kuwa makubaliano hayo hayawezi kuleta amani duniani na si tu hayawezi kupelekea kuangamizwa silaha za atomiki, lakini pia hayana uwezo wa kutia nguvu usalama wa nchi za dunia.
ICAN kampeni ya kimataifa ya kuangamiza silaha za nyuklia

Itakumbukwa kuwa, tunzo ya amani ya Nobel mwaka 2017 iliyotolewa siku ya Ijumaa, imekwenda kwa Kampeni ya Kimataifa ya Kuangamiza Silaha za Nyuklia (ICAN). Kampuni hiyo imetoa mchango mkubwa katika kutiwa saini makubaliano hayo na nchi 122 mwezi Julai mwaka huu. Hata hivyo makubaliano hayo ni ya kimaonyesho zaidi kulikoni kuwa ya uhakika. Sababu yake ni kwamba nchi nane zenye silaha za nyuklia yaani Marekani, Russia, Uingereza, Ufaransa, China, India, Pakistan na Korea Kaskazini pamoja na utawala wa Kizayuni wa Israel, zimekataa kutia saini makubaliano hayo.
Taarifa zinasema kuwa Marekani inamiliki vichwa elfu nne vya nyuklia hivi sasa. Wamarekani wanadai kuwa, lengo lao la kujilimbikizia silaha za nyuklia za mauaji ya umati, ni kujilinda mbele ya nchi nyingine zenye silaha hizo za maangamizi ya halaiki. Hata hivyo madai hayo hayana ukweli kwani Marekani ndiyo nchi pekee duniani ambayo imewahi kutumia silaha za nyuklia katika historia nzima ya mwanadamu. Katika Vita vya Pili vya Dunia, Marekani ilishambulia kwa nyuklia miji ya Hiroshima na Nagasaki nchni Japan kwa madai ya kuwalazimisha viongozi wa nchi hiyo wasalimu amri. Ukatili huo wa Marekani umewafanya kuwa wahanga maelfu kwa maelfu ya viumbe wakiwemo wanadamu. Ripoti zinaonesha kuwa hivi sasa Marekani inamiliki bomu lijulikanalo kwa jina la B61 na sasa hivi inalifanyia marekebisho bomu hilo kwa gharama zilizosawa na dola bilioni kumi. Bi Dianne Feinstein, seneta wa Marekani kutoka chama cha Democrats anaamini kuwa, silaha za kiistratijia zilizoko katika maghala ya silaha nchini Marekani ni nyingi mno ikilinganishwa na mahitaji ya nchi hiyo na waitifaki wake. 

Wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, Marekani haiwezi kabisa kujiunga na mikataba na makubaliano ya kuangamiza silaha za nyuklia duniani, bali kitu pekee kinachotegemewa kutoka kwa dola hilo la kibeberu ni kushadidisha majaribio yake ya nyuklia, jambo ambalo linazichochea nchi nyingine duniani kujilimbikizia silaha za kisasa zaidi za nyuklia na za maangamizi ya umati. Fauka ya hayo, rais wa Marekani, Donald Trump alisema waziwazi wakati wa kampeni za uchaguzi kwamba hatosita kufanya mashambulizi ya nyuklia akilazimika kufanya hivyo.
Hivi sasa jeshi la Marekani imejikita zaidi katika kutengeneza mabomu madogo madogo yenye athari hafifu kidogo ya nyuklia na kuyafanyia majaribio katika nchi mbalimbali za dunia kama za Mashariki ya Kati. Pamoja na kukhafifishwa huko, lakini mabomu hayo bado yanafanya uharibifu mkubwa. Sasa hivi si tu juhudi za kuangamiza silaha za nyuklia hazijafanikiwa, lakini baya zaidi ni kwamba madola ya kibeberu kama vile Marekani yanazidi kujilimbikizia silaha hizo angamizi na kuzifanya kuwa za hatari zaidi. Nukta ya kuzingatiwa hapa ni kwamba iwapo silaha hizo zitaingia mikononi mwa watu wasioaminika au magenge ya kigaidi, hakuna mtu yeyote anayeweza kutabiri ukubwa wa hatari na madhara yanayoweza kusababishwa na jambo hilo duniani. 

No comments:

Post a Comment