Tuesday, October 3, 2017

TOFAUTI KATI Y TRUMP NA REX W. TILLERSON KUHUSIANA NA KOREA KASKAZINI

Kwa mara nyingine suala la namna ya Washington inavyotakiwa kukabiliana na Korea Kaskazini, limeibua tofauti kati ya Rais Donald Trump na Waziri wake wa Mambo ya Nje Rex W. Tillerson.
Muda mfupi baada ya Tillerson kuzungumza mjini Beijing, China kuhusiana na uwepo wa mtandao wa mawasiliano ya moja kwa moja na serikali ya Korea Kaskazini, Rais Donald Trump amesema kuwa, kufanya mazungumzo na Pyongyang ni kupoteza wakati. Katika ukurasa wake wa Twitter, Trump alimueleza Waziri wake wa Mambo ya Nje kwa kuandika kuwa: "Nimeshamwambia Rex Tillerson, Waziri wetu mzuri sana wa Mambo ya Nje kwamba anapoteza muda wake kwa kujaribu kuzungumza na Mtu Mdogo wa Makombora". Mwisho wa kunukuu.
Rais Trump kushoto na Kim Jong-Un, Kiongozi wa Korea Kaskazini
Katika wiki za hivi karibuni na katika miamala isiyo ya kimantiki wala kidiplomasia, Trump alimtaja Kim Jong-Un, Kiongozi wa Korea Kaskazini kuwa 'Mtu wa Makombora.' Matamshi hayo aliyatoa katika hali ambayo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani alikuwa amefanya safari nchini China ambapo kwa mara ya kwanza alikiri kuwepo mawasiliano kati ya serikali ya Marekani na Pyongyang. Akiongea na waandishi wa habari, Tillerson alisema kuwa Washington inatumia mawasiliano hayo kwa ajili ya kufahamu misimamo ya Korea Kaskazini  kwa minajili ya kutatua mgogoro wa sasa wa eneo la Peninsula ya Korea. Kuongezeka mzozo wa eneo la Korea, kumeenda sambamba na kuibuka tofauti za ndani katika serikali ya Washington kuhusiana na kadhia hiyo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Rex W. Tillerson
Hata hivyo ifahamike kuwa, tofauti kati ya marais wa Marekani na mawaziri wao, ni jambo la kawaida. Pamoja na hayo hakujawahi kushuhudiwa tofauti kubwa kama za sasa kiasi cha kumfanya Rais Donald Trump aamue kuandika katika ukurasa wake wa Twitter akiieleza dunia kuhusiana na uwepo wa tofauti kati yake na waziri wake huyo wa masuala ya kigeni. Matamshi na maoni rasmi ya Trump kupitia mtandao wa Twitter yanaonyesha kwamba rais huyo wa Marekani ameazimia kuanzisha vita haribifu vya silaha za nyuklia katika eneo la mashariki mwa Asia na ni kwa ajili hiyo ndio ameepusha aina yoyote ya mazungumzo yenye lengo la kuzuia kutokea vita hivyo. Hii ni katika hali ambayo duru za kidiplomasia na hata za kijeshi nchini humo, kwa akali zimeweka wazi misimamo yao rasmi katika kufuatilia njia za  amani za utatuzi wa mgogoro wa eneo la Peninsula ya Korea.
Trump, rais wa Marekani
Kundi hilo linaamini kuwa, rais wa sasa wa Marekani ambaye hana aina yoyote ya uzoefu wa kisiasa na kiusalama, anakusudia kuitumbukiza nchi hiyo katika vita vya nyuklia na Korea Kaskazini, vita ambavyo vitasambaa hadi Japan, Korea Kusini, China na Russia. Ni kwa msingi huo ndio maana weledi hao wanafanya juhudi za kufungua milango ya mazungumzo ya amani na Pyongyang. Hata hivyo ili kujaribu kujionyesha kuwa naye ni mwanasiasa, Trump na katika kujaribu kuvutia uungaji mkono wa Wamarekani na hata wa baadhi ya washirika wake nje ya nchi, anaendelea kupiga ngoma ya vita dhidi ya Korea Kaskazini sambamba na kusisitiza kuwa mazungumzo na Pyongyang ni jambo lisilokuwa na faida yoyote. Ala kulli hal, misimamo hasi ya Rais Donald Trump dhidi ya Korea Kaskazini ndiyo imeifanya nchi hiyo ya Asia kujiimarisha zaidi kwa silaha za nyuklia na makombora ya balestiki suala ambalo kwa upande mwingine linaendelea kumtia hasira rais huyo wa Marekani.

No comments:

Post a Comment