Tuesday, October 3, 2017

WATU 17 WAUAWA KATIKA SHEREHE ZA KUJITANGAZIA UHURU CAMEROON

Watu 17 wauawa katika sherehe za kujitangazia uhuru Cameroon
Kwa akali watu 17 wameuawa na wengine wengi kujeruhiwa na askari wa jeshi la Cameroon, wakati wa maandamano ya kushinikiza kujitenga maeneo ambayo wakazi wake wanazungumza Kiingereza, katikati mwa nchi.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limesema watu hao wameuawa na maafisa usalama wa nchi hiyo katika machafuko na maandamano kwenye majimbo mawili yanayotaka kujtenga na serikali kuu ya Yaunde.
Amnesty imesema raia wawili wa Nigeria ni miongoni mwa watu waliouawa katika ghasia hizo baina ya waandamanaji na askari wa Cameroon.
Awali, shirika la habari la AFP liliripoti kuwa, miongoni mwa wanaharakati waliouawa katika maandamano ya Jumapili ni wafungwa watano waliokuwa wakijaribu kutoroka jela.
Maandamano ya kutaka 'kujitenga' nchini Cameroon
Raia wachache wa Cameroon wanaozungumza lugha ya Kiingereza wamekuwa wakifanya maandamano ya mara kwa mara tangu Novemba mwaka jana wakilalamikia kutengwa na serikali ya nchi hiyo.
Wafanyakazi wengi wa umma katika maeneo hayo pia wamekuwa wakifanya mgomo kulalamikia kile wanachokitaja kama ubaguzi, ambapo wanasema raia wa Cameroon wanaozungumza Kifaransa ndio wanaopewa nafasi za ajira.

No comments:

Post a Comment