Thursday, October 19, 2017

LARIJANI: VITENDO VYA CHUKI VYA WAMAREKANI NI DUKUDUKU LA MABUNGE YOTE

Larijani: Vitendo vya chuki vya Wamarekani ni dukuduku la mabunge yote
Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) amezungumzia mazungumzo yake ya hivi karibuni na maspika wa mabunge ya nchi zilizoshiriki katika mkutano wa Umoja wa Mabunge Duniani mjini Saint Petersburg, Russia na kusema kuwa, maspika wa mabunge yote yaliyoshiriki kwenye mkutano huo wana wasiwasi na dukuduku na vitendo vya kiuadui vya Wamarekani.
Shirika la habari la IRIB limemnukuu Ali Larijani akisema hayo leo na kuongeza kuwa, katika matamshi yake ya hivi karibuni, rais wa Marekani, Donald Trump ameonesha sura halisi ya nchi yake lakini tab'an amelaumiwa na dunia nzima.
Amesema, maneno yasiyo na msingi yaliyotolewa na rais wa Marekani yanaonesha namna alivyoshindwa kuwakinaisha watu, hivyo, badala ya kutumia lugha ya mantiki, ameropoka mambo yasiyo na msingi.
Dk Ali Larijani akihutubia mkutano wa Umoja wa Mabunge Duniani mjini Saint Petersburg, Russia

Itakumbukwa kuwa, tarehe 13 mwezi huu wa Oktoba, rais wa Mareekani alitoa tuhuma zisizo na msingi dhidi ya Iran na alisema pia kuwa, hatounga mkono ripoti nane zilizotolewa na Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki IAEA zinazothibitisha kuwa Iran imeheshimu kikamilifu makubaliano ya nyuklia ya JCPOA.
Akiwa mjini Saint Petersburg, Dk Ali Larijani, Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu alionana na maspika wenzake kadhaa kama vile wa Iraq, Mexico, Vietnam na Uturuki na kujadiliana nao masuala mbalimbali ya pande mbili na masuala tata ya eneo hili.
Mkutano wa siku tano waa Umoja wa Mabunge Duniani ambao ulishirikisha ujumbe mbalimbali wa mabunge kutoka zaidi ya nchi 150 ulianza siku ya Jumamosi mjini Saint Petersburg, Russia chini ya kaulimbiu "Kueneza Utamaduni na Amani Kupitia Mijadala ya Kidini na Kikaumu."

No comments:

Post a Comment