Wednesday, October 18, 2017

POLISI TANZANIA WAUA WATUHUMIWA WATANO WA UJAMBAZI NA KUKAMATA MAGURUNETI SABA

Polisi Tanzania waua watuhumiwa watano wa ujambazi na kukamata maguruneti saba
Polisi jijini Dar es Salaam Tanzania imetangaza habari ya kukamatafa maguruneti saba na kusema inaamini kwamba yangelitumiwa na watu wahalifu nchini humo.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi kanda ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, jeshi hilo la polisi pia limefanikiwa kuua watuhumiwa watano wa uhalifu katika matukio mawili tofauti na kwamba katika operesheni hizo mbali na kukamata maguruneti hayo, limefanikiwa kukamata bunduki aina ya SMG iliyofutwa namba, magazini yenye risasi 16, maganda 10 ya risasi za SMG pamoja na pikipiki ambazo polisi wanasema zilikuwa zinatumiwa na wahalifu hao kufanyia uhalifu.
Jeshi hilo limebainisha kwamba, silaha hizo zimekamatwa na askari waliokuwa doria majira ya usiku eneo la Msongola wilayani Ilala jijini Dar es Salaam, ambapo awali polisi hao walikuwa wakiwafuatilia washukiwa hao wa uhalifu waliokuwa wamepanda pikipiki moja wakiwa watatu.
Aidha Kamanda wa Polisi, Lazaro Mambosasa amesema kuwa, baada ya watuhumiwa hao watatu kubaini kuwa walikuwa wakifuatiliwa na polisi waliamua kuongeza mwendo na kuingia barabara ya vumbi ambako walifyatua risasi.
Kamanda Mambosasa amesema, askari waliwazidi nguvu watuhumiwa hao na kuwapiga risasi na kuanguka chini pamoja na pikipiki hiyo. Katika tukio jingine, polisi wa Tanzania wameua watu wawili baada ya kuwatuhumu kufanya ujambazi eneo la Mbagala Zakheim ambako walipokea taarifa kutoka kwa wananchi kuwa watu hao walipanga kuvamia maduka ya Tigo-Pesa na M-Pesa katika eneo hilo.

No comments:

Post a Comment