Wednesday, November 29, 2017

KAMANDA WA BOKO HARAM ATIWA MBARONI, WENZAKE 4 WAUAWA, MATEKA 212 WAKOMBOLEWA

Kamanda wa Boko Haram atiwa mbaroni, wenzake 4 wauawa, mateka 212 wakombolewa
Jeshi la Nigeria limetangaza kuwa, limewakomboa raia wengine 212 waliokuwa wakishikiliwa mateka na wanachama wa kundi la kigaidi la Boko Haram katika msitu wa Sambisa.
Msemaji wa jeshi la Nigeria, Sani Usman amesema kuwa, jeshi la nchi hiyo limefanikiwa pia kumtia mbaroni mmoja wa makamanda wa Boko Haram, Amman Judee na kuwaua wapiganaji wanne wa kundi hilo la kigaidi.
Amesema kuwa, kamanda huyo wa Boko Haram aliyetiwa mbaroni anaendelea kusailiwa. Kwa mujibu wa jeshi la Nigeria, watu 212 waliokombolewa kutoka mikononi mwa wapiganaji wa Boko Haram ni kundi la pili kukombolewa na jeshi la nchi hiyo katika kipindi cha chini ya wiki moja.
Siku ya Jumamosi jeshi la Nigeria liliwakomboa raia wengine 30 waliokuwa wakishikiliwa na wanamgambo wa Boko Haram ambapo lilifanikiwa pia kuwauwa wanachama 11 wa kundi hilo la kigaidi katika kijiji cha Bama huko Borno kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Wanamgambo wa kundi la kigaidi la Boko Haram
Baadhi ya duru zinaripoti kwamba, jeshi la Nigeria limepata mafanikio makubwa katika siku za hivi karibuni katika vita na operesheni zake dhidi ya wanamgambo wa Boko Haram.
Mashambulizi ya genge la kigaidi la Boko Haram yalianza mwaka 2009 kaskazini na kaskazini mashariki mwa Nigeria na hadi hivi sasa zaidi ya watu 20 elfu wameshauwa kutokana na machafuko yaliyosababishwa na kundi hilo.
Kundi la Boko Haram limekuwa likifanya jinai za kila namna ikiwa ni pamoja na kuteka nyara watu pamoja na wasichana na kuwapiga mnada kama bidhaa. 

No comments:

Post a Comment