Wednesday, November 29, 2017

RAIS BUHARI: RAIA WA NIGERIA WAMEKUWA WAKIUZWA KAMA MBUZI NCHINI LIBYA

Rais Buhari: Raia wa Nigeria wamekuwa wakiuzwa kama mbuzi nchini Libya
Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria amesema kuwa, raia wote wa nchi hiyo ambao wamekwama huko Libya watarejeshwa nyumbani na kusaidiwa kurejelea maisha ya kawaida.
Akizungumzia video za karibuni ambazo zimekuwa zikiwaonesha Waafrika wakiuzwa kwenye mnada wa watumwa nchini Libya, Rais Buhari amesema inasikitisha sana kwamba "baadhi ya raia wa Nigeria wanauzwa kama mbuzi  kwa  dola kadhaa huko Libya".
Rais wa Nigeria ameonekana pia kushangaa iwapo raia wa Libya walijifunza lolote la maana tangu kuondolewa madarakani kwa Kanali Muammar Gaddafi mwaka 2011.
''Walichojifunza pekee ni kuwapiga watu risasi na kuua. Hawakujifunza kuwa mafundi wa umeme, mafundi wa mabomba au ufundi wowote ule," amesema.
Rais Muhamadu Buhari wa Nigeria
Hayo yanajiri katika hali ambayo, radiamali mbalimbali zimeendelea kutolewa kuhusiana na taarifa za kuweko biashara ya utumwa nchini Libya.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetoa mwito wa kuendeshwa vita dhidi ya magendo ya binadamu na biashara ya utumwa katika bara la Afrika.
Filippo Grandi, Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR amesema,  kuna haja ya kukabiliana na biashara ya utumwa na vitendo vingine vya ukiukaji wa haki za binadamu vinavyofanywa dhidi ya wahajiri wanaopitia Libya wakiwa na nia ya kuelekea barani Ulaya kutafuta maisha mazuri.
Itakumbukwa kuwa, hivi kkaribuuni, televisheni ya CNN ilirusha hewani mubashara mnada wa kuuza Waafrika huko nchini Libya ambapo kila mtu alikuwa akiuzwa kwa dola zisizopungua 400 za Kimarekani. 

No comments:

Post a Comment