Wednesday, November 8, 2017

MWANAMFALME: HAKI ZA BINADAMU ZINAKANYAGWA SANA SAUDIA

Mwanamfalme: Haki za binadamu zinakanyagwa sana Saudia
Khalid bin Farhan Al Saud, Mwanamfalme ambaye amejitenga na utawala wa Aal-Saud, amesema kuwa kabla ya kuomba hifadhi ya kisiasa nchini Ujerumani, kwa muda mrefu alikuwa akiishi kwa wasiwasi na mashaka mengi nchini Saudia.
Farhan Al Saud ambaye ni mpinzani wa utawala wa Saudia ameyasema hayo katika mahojiano na kanali moja ya televisheni ya Ujerumani ambapo amezungumzia kutokuwepo uhuru wa kujieleza na ukiukwaji haki za binadamu uliokithiri nchini humo. Amesema kuwa, baada ya kupinga utawala wa Aal-Saud na kuwasilisha malalamiko ya kuwepo uhuru wa kiraia, alikumbwa na mashinikizo na udhia mkubwa kiasi kwamba alilazimika kujiuzulu jeshini na kutoroka nchi.
Khalid bin Farhan Al Saud, Mwanamfalme wa Saudia
Mwanamfalme huyo wa utawala wa Aal-Saud sambamba na kusisitiza kuwa, haogopi kitu chochote amesema zaidi ya mapendekezo 50 yamewasilishwa kwake kutoka ubalozi wa Saudia nchini Ujerumani yakimtaka aandike taarifa ya kuomba msamaha kwa Mfalme Salman bin Abdulaziz Al Saud lakini amekataa kufanya hivyo. Khalid bin Farhan Al Saud ameashiria pia njama za viongozi wa Saudia za kumuwekea mashinikizo na hata ikiwezekana kumtia mbaroni kwa kumtumia dada yake anayeitwa 'Ibtisam' na anaeshikiliwa katika kifungo cha nyumbani nchini Saudia na kusema kuwa, watawala wa ukoo wa Aal-Saud kwa mara kadhaa walimtisha kwamba ikiwa hatoacha kufichua machafu ya utawala wa kifalme wa Saudia, watamuua dada yake.
Ukandamizaji wa askari wa Aal-Saud
Kwa mujibu wa takwimu na ripoti za ndani nchini Saudia, zaidi ya wanaharakati wa kisiasa na wanasheria elfu 30 wanashikiliwa katika jela mbalimbali za utawala huo wa Aal-Saud.

No comments:

Post a Comment