Sunday, November 19, 2017

DURU ZA ZANU-PF: CHAMA TAWALA ZIMBABWE KINAPANGA KUMTIMUA MUGABE

Duru za ZANU-PF: Chama tawala Zimbabwe kinapanga kumtimua Mugabe
Viongozi wa chama tawala nchini Zimbabwe cha ZANU-PF wanatazamiwa kupitisha uamuzi wa kumuondoa uongozini Rais wa nchi hiyo na kiongozi wa chama hicho Robert Gabriel Mugabe, ambaye amekuwa akiiongoza nchi hiyo tangu ilipopata uhuru wake miaka 37 iliyopita. Hayo ni kwa mujibu wa duru mbili kutoka ndani ya chama hicho.
Kikao cha dharura kamati kuu ya ZANU-PF kilitazamiwa kufanyika mapema leo kufikiria uamuzi wa kumuondoa kwenye uongozi Mugabe mwenye umri wa miaka 93, siku chache baada ya jeshi kutwaa madaraka kwa lengo la kile kilichotajwa kama kuwachukulia hatua "wahalifu" waliomzunguka kiongozi huyo.
Wakati huohuo, ikimnukuu kiongozi wa Kanisa Katoliki ambaye ni mpatanishi katika mazungumzo na Mugabe, televisheni ya taifa ya Zimbabwe imetangaza kuwa kiongozi huyo atakutana na makamanda wa jeshi hii leo.
Kamati kuu ya chama tawala Zanu-pf inatazamiwa kumrejesha tena kwenye wadhifa wake makamu mwenyekiti wa chama Emmerson Mnangagwa, ambaye kutimuliwa kwake kama Makamu wa Rais na makamu mwenyekiti wa chama hicho kulipelekea jeshi kuingilia kati na kutwaa madaraka ya nchi.
Mke wa Mugabe Grace, yeye anatazamiwa kuvuliwa uongozi wa tawi la wanawake la chama cha Zanu-pf.
Robert Mugabe akiwa na mkewe Grace
Hayo yanajiri huku Rais Mugabe akiendelea kukataa kung'atuka madarakani licha ya kushuhudia kwa macho yake kutokea nyumbani kwake alikowekwa kizuzini jinsi uungaji mkono aliokuwa nao kutoka kwenye chama, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi ukiyeyuka ndani ya muda wa chini ya siku tatu tu.
Mpwa wa kiongozi huyo Patrick Zhuwao amevieleza vyombo vya habari kuwa Mugabe na mkewe "wako tayari kufa kwa kile wanachokiona kuwa ndio sahihi" kuliko kuachia ngazi ili kuhalalisha kile alichokielezea kama mapinduzi ya kijeshi.
Hayo yanajiri huku makumi ya maelfu ya wananchi wakimiminika kwenye barabara za miji ya nchi hiyo hususan mji mkuu Harare kushinikiza kiongozi huyo ang'atuke madarakani sambamba na kusherehekea kile wanachokieleza kama mwisho wa enzi za miaka karibu 40 ya utawala wake…/

No comments:

Post a Comment