Saturday, November 25, 2017

IRAN YALAANI VIKALI HUJUMA YA KIGAIDI MSIKITINI MISRI

Iran yalaani vikali  hujuma ya kigaidi msikitini Misri
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani vikali hujuma ya kigaidi wakati wa Sala ya Ijumaa msikitini katika mkoa wa Sinai Kaskazini nchini Misri.
Katika taarifa kupitia ukurasa wake wa Twitter, Waziri wa Mambo ya Nje ya Iran Mohammad  Jawad Zarif amesema ugaidi hauheshimu thamani za Kiungu na kibinadamu.
Zarif ameongeza kuwa: "Kwa mara nyingine ugaidi umetoa pigo kwa taifa azizi la Misri na kwa mara nyingine kuthibitisha kuwa hautafautishi mahali hata ndani ya msikiti na maeneo mengine ya ibada."
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amelaani vikali hujuma hiyo ya kigaidi na kumuomba Mwenyezi Mungu awarehemu mashahidi na kuwapa majeruhi nafuu ya haraka.
Mohammad Javad Zarif
Jana Waislamu wasiopungua 235 wameuawa na wengine zaidi ya 110 kujeruhiwa katika shambulizi la magaidi wakufurishaji dhidi ya msikiti mmoja wa Twariqa katika Peninsula ya Sinai nchini Misri.
Duru za polisi nchini humo zimesema genge la kigaidi limeushambulia Msikiti wa al-Rawdhah ulioko katika mji wa Bir al-Abd, yapata kilomita 40 kutoka mji wa Al-Arish, makao makuu ya mkoa wa Sinai Kaskazini. 
Rais Abdulfattah al-Sisi wa Misri sanjari na kulaani hujuma hiyo, ameitisha mkutano wa dharura na vyombo vya usalama huku akitangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa, kufuatia ukatili huo wa magaidi.

No comments:

Post a Comment