Saturday, November 4, 2017

MAPIGANO YAENDELEA KASKAZINI MWA JAMHURI YA AFRIKA YA KATI

Mapigano yaendelea kaskazini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati
Jumuiya ya Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) imeripoti kuwa mapigano makali yangali yanaendelea katika mkoa wa Ouham kaskazini mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Taarifa iliyotolewa na jumuiya hiyo ya kimataifa ya tiba, mbali na kueleza wasiwasi uliopo kutokana na kuendelea mapigano yaliyochanganyika na vitendo vya ukatili kwenye maeneo mabalimbali ya mkoa wa Ouham imeongeza kuwa watu wasiopungua wawili waliuawa na wengine 21 walijeruhiwa katika mapigano yaliyotokea wiki iliyopita baina ya makundi mawili hasimu.
Kwa mujibu wa duru zenye mfungamano na Umoja wa Mataifa mapigano hayo yalihusisha kundi la waasi wa Kikristo la Anti-Balaka na wanamgambo wa kundi la wabeba silaha liitwalo Harakati ya Kizalendo kwa ajili ya Jamhuri ya Afrika ya Kati (MPC) ambalo limeundwa na baadhi ya waasi wa zamani wa harakati ya Seleka.
Jamhuri ya Afrika ya Kati imekuwa ikishuhudia mapigano na machafuko tangu aliyekuwa rais wa nchi hiyo François Bozizé alipoondolewa madarakani Machi 24, mwaka 2013 na harakati hiyo.
Rais Faustin-Archange Touadéra
Licha ya kufanyika uchaguzi wa rais mnamo mwezi Machi mwaka uliopita wa 2016 uliomleta madarakani rais wa sasa Faustin-Archange Touadéra, hata hivyo serikali ya Bangui inayoongozwa na kiongozi huyo hadi sasa imeshindwa kurejesha amani na uthabiti nchini humo.
Wakati Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alipofanya safari nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati katikati ya mwezi uliopita wa Oktoba aliashiria kuwa anakusudia kutoa wito wa kuongezwa askari wa ziada 9,000 katika operesheni za kulinda amani nchini humo hasa kwa ajili ya kuwalinda raia.../

No comments:

Post a Comment