Wednesday, November 22, 2017

MNANGAGWA AREJEA ZIMBABWE, KUPISHWAIJUMAA KUMRITHI MUGABE

Mnangagwa arejea Zimbabwe, kuapishwa Ijumaa kumrithi Mugabe
Makamu wa Rais wa Zimbabwe aliyepigwa kalamu nyekundu hivi karibuni na Rais Robert Mugabe aliyetangaza kujiuzulu hapo jana amerejea nchini akitokea Afrika Kusini.
Emmerson Mnangagwa alifutwa kazi wiki mbili zilizopita na kukimbia nchi akihofia usalama wake. Mwanasiasa huyo alipigwa kalamu kutokana na kile wadadisi wa mambo walikitaja kuwa ni hatua ya Mugabe mweye umri wa miaka 93 kumsafishia njia mkewe Grace Mugabe, arithi kiti chake.
Wananchi wa Zimbabwe mjini Harare wamebeba mabango yenye picha za Mnangagwa zilizoambatana na jumbe zisemazo: Karibu nyumbani shujaa wetu; Uliahidi utarejea na kweli umerejea, karibu sana. Baadhi ya picha za mwanasiasa huyo zilikuwa na jina lake la utani la "Mamba".
Jacob Mudenda, Spika wa Bunge la nchi hiyo amesema maandalizi ya kumuapishwa Mnangagwa Ijumaa ijayo ili kuchukua nafasi ya Mugabe yanaelekea kukamilika.
Mugabe na Mnangagwa katika sherehe ya taifa huko nyuma
Akiongea baada ya kukutana na Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini kabla ya kuondoka nchini humo mapema leo, Mnangagwa amesema: "Taifa hili halipaswi tena kushikwa mateka na mtu mmoja, ambaye yuko tayari kufia ofisini kwa gharama yoyote ile."
Hapo jana Jumanne, Mugabe katika barua yake kwa Spika wa Bunge, alisema amejiuzulu kwa khiari yake mwenyewe ili kupisha mapokezano ya uongozi kwa njia ya amani, baada ya kuiongoza nchi hiyo ya kusini mwa Afrika kwa miaka 37.
Baada ya Spika wa Bunge la Zimbabwe kutoa tangazo la kujiuzulu kwa Mugabe, wananchi wa taifa hilo walijitokeza mabarabarani kwa shangwe, nderemo na vifijo kusherehekea habari hizo.

No comments:

Post a Comment