Wednesday, November 15, 2017

SISITIZO LA UN LA ULAZIMA WA KUFUNGULIWA BANDARI YA AL HUDAYDAH NCHINI YEMEN

Sisitizo la UN la ulazima wa kufunguliwa bandari ya al Hudaydah nchini Yemen
Umoja wa Mataifa umepinga sharti lililotolewa na muungano vamizi wa nchi za Kiarabu unaofanya mauaji na umwagaji mkubwa wa damu nchini Yemen ambao umekataa kufungua bandari ya al Huydadah hadi pale matakwa yao ya kiuadui yatakapokubaliwa.
Kwa kweli hivi sasa hakuna watu wa nchi yoyote duniani walio na hali ngumu zaidi kushinda Wayemen. Hakuna mgogoro wowote ulioko duniani ambao hauko pia huko Yemen. Mashambulio ya kikatili ya Bani Saud ni ya kila siku nchini humo. Hakuna matumaini yoyote ya maisha nchini Yemen. Mabomu ya Aal Saud yanachukua roho za Wayemen kila siku huku njaa na magonjwa yakipigana vikumbo katika kuchukua roho za raia wasio na ulinzi wa nchi hiyo. Hali ni mbaya kiasi kwamba hata hakuna takwimu za kina za watu wanaokufa na kujeruhiwa kila leo katika nchi hiyo ya Kiislamu, lakini hata kama tutakubaliana na hizo hizo takwimu zinazotolewa na Umoja wa Mataifa basi tutaona ni kiasi gani Saudi Arabia na wenzake wanafanya ukatili wa kutisha katika nchi hiyo ya Kiarabu. Kwa mujibu wa takwimu hizo, zaidi ya watu elfu nane wameshauawa na makumi ya maelfu ya wengine wamejeruhiwa. Wahanga wa ukatili huo ni wa rika tofauti, kuanzia viajuza hadi vitoto vichanga, wanawake kwa wanaume. Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekundu limesema kuwa, kwa siku watu elfu saba wanaambukizwa ugonjwa wa kipindupindu na kila siku mamia ya raia wa nchi hiyo wanapoteza maisha. Njaa ni nduli wa tatu anayechukua roho za watu huko Yemen pembeni mwa vita na maradhi.
Hakuna waliosalimika na jinai za Saudi Arabia nchini Yemen
Mazingira ya hivi sasa yanasambaza harufu ya kifo kila sekunde nchini Yemen. Mgogoro wa nchi hiyo unakuwa mkubwa sekunde baada ya sekunde kutokana na nchi hiyo maskini kuzingirwa kila upande na kushambuliwa kila siku kwa kila aina ya silaha hata zilizopigwa marufuku. Hivi sasa njia zote za kuwafikishia misaada wananchi wa nchi hiyo zimefungwa. Hadi hivi sasa kumekuwa kukitolewa tahadhari za kutokea maafa makubwa ya kibinadamu ambayo yatakuwa makubwa zaidi duniani katika miongo kadhaa iliyopita. Lakini pamoja na hayo, na kutokana na uungaji mkono wa kila upande wa Marekani, serikali ya Saudia imekuwa ikipuuza tahadhari zote zinazotolewa. Mark Lukok, ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya misaada ya kibinadamu. Alisema wiki iliyopita kwamba kama misaada ya binadamu haitafikishwa kwa wananchi wa Yemen haraka iwezekanavyo, basi ukame ambao haujawahi kutokea katika miongo kadhaa ya hivi karibuni duniani, utatokea nchini humo.
Bila ya shaka ni kwa sababu hiyo ndio maana Umoja wa Mataifa umeitaka Saudi Arabia kufungua haraka bandari ya al Hudaydah huko Yemen. Hata hivyo utawala wa kidikteta wa Bani Saud umekataa bali umezidi kung'ang'ania msimamo wake wa kuifunga kabisa bandari hiyo ambayo ndiyo njia pekee ya kuwafikishia misaada wananchi wa Yemen. Saudi Arabia inadai kuwa bandari hiyo ilikuwa inatumika kufanya magendo ya silaha nchini Yemen, lakini imeshindwa kutoa ushahidi wa kuthibitisha madai hayo. Wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, kitendo cha Saudi Arabia cha kuifunga bandari hiyo ni ushahidi tosha kwamba ukatili wa wavamizi wa Yemen umeshindwa katika medani za vita na sasa wameamua kumalizia hasira zao kwa wananchi wa kawaida.
Licha ya ukatili mkubwa wanaofanyiwa, lakini wananchi wa Yemen bado wako ngangari, na wamesema katu hawatokubaliana na uvamizi wa nchi yao
Wachambuzi hao wanasema, hatua hiyo ya Saudia ni kujaribu kuishinikiza harakati ya Answarullah na waitifaki wake ili wakubali mapatano, baada ya kushindwa njama zote za maadui hao za kuidhibiti San'a, mji mkuu wa Yemen. Amma swali linalojitokeza habari ni kwamba, Umoja wa Mataifa ni mkweli kiasi gani katika mwito wake kwa Saudia wa kuitaka ifungue bandari ya al Hudaydah huko Yemen? Inabidi tusubiri na kuona ni kiasi gani umoja huo utaweza kuushinikiza ukoo wa Aal Saud katika suala hilo ndipo tutakapoweza kujua ukweli wa Umoja wa Mataifa katika mwito wake huo.

No comments:

Post a Comment