Wednesday, November 15, 2017

VYOMBO VYA HABARI MAGHARIBI VYANYAMANZIA KIMYA JINAI ZA SAUDIA DHIDI YA WAYEMEN

Vyombo vya habari vya Magharibi vyanyamazia kimya jinai za Saudia dhidi ya Wayemen
Wabunge nchini Iran wamelaani vikali mauaji yanayotekelezwa na Saudi Arabia dhidi ya raia wa Yemen huku wakisema jinai hizo zimenyamaziwa kimya na vyombo vya habari vya magharibi.
Katika taarifa siku ya Jumatano, wabunge 191 wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran wamesema katika zama hizi ambazo, madola ya Magharibi, hasa Marekani, hudai kuwa watetezi wa haki za binadamu, tunashuhudia jinai za kuogofya zikitekelezwa na Saudi Arabia dhidi ya watu wanaodhulumiwa na wasio na ulinzi wa Yemen.
Wabunge wa Iran wametahadharisha kuwa Yemen inakabiliwa na maafa ya kibinadamu ambayo yamesababishwa na hujuma ya Saudia dhidi ya nchi hiyo sambamba na mzingiro wa anga, nchi kavu na bahari na hivyo kupelekea misaada ya dharura kama  dawa na chakuka kutowafikia Wayemen. Wabunge wa Iran wamesema Saudi Arabia na waitifaki wake, hasa Marekani, wanabeba dhima ya jinai dhidi ya watu wa Yemen.
Watoto ni waathirika wakuu wa jinai za Saudia nchini Yemen
Taarifa hiyo imeongeza kuwa: "Swali kubwa hapa ni kuwa, je, ni vipi Saudi Arabia inawaua watu wasio na hatia kila siku kwa kutumia silaha mbali mbali hatari huku wanaodai kutetea haki za binadamu wakiwa kimya, bali hata wakiunga mkono jinai hizo?"
Wiki iliyopita Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa alieleza wasiwasi wake kuhusu hatua ya Saudi Arabia na washirika wake ya kufunga kabisa mipaka ya Yemen kwa siku ya tano mfululizo na kusisitiza kuwa Yemen inakabiliwa na baa kubwa zaidi la njaa kuwahi kushuhudiwa duniani katika miongo ya hivi karibuni.
Saudi Arabia ikishirikiana na Marekani, Israel na nchi nyingine kadhaa za Kiarabu ilianzisha mashambulizi ya pande zote dhidi ya Yemen Machi mwaka 2015. Maelfu ya raia wasio na hatia wameuawa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi kutokana na mashambulizi hayo.

No comments:

Post a Comment