Wednesday, November 22, 2017

BAADA YA MUGABE KUJIUZULU, UMOJA WA MATAIFA WAWATAKA WAZIMBABWE KUDUMISHA UTULIVU

Baada ya Mugabe kujiuzulu, Umoja wa Mataifa wawataka Wazimbabwe kudumisha utulivu
Umoja wa Mataifa umewataka wananchi wa Zimbabwe kudumisha amani na utulivu katika kipindi hiki baada ya Rais Robert Mugabe kutangaza kujiuzulu hapo jana.
Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amewataka wananchi wa nchi hiyo kudumisha amani na utulivu katika kipindi hiki inachopitia nchi yao baada ya kiongozi wa nchi hiyo kujiuzulu.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amezitaka tawala zote kuheshimu matakwa ya wananchi. Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe hatimaye jana alisalimu amri na kukubali kujiuzulu kufuatia mashinikizo ya kila upande ya kumtaka aachie madaraka. 
Jacob Mubenda, Spika wa Bunge la Zimbabwe alitangaza jana kwamba, amepokea barua ya kujiuzulu kutoka kwa kiongozi huyo mkongwe mwenye umri wa miaka 93.
Robert Mugabe amejiuzulu baada ya kuiongoza Zimbabwe kwa miaka 37
Katika barua hiyo ya kujiuzulu, Mugabe alisema anajiuzulu kwa hiari, ili kupisha mapokezano ya uongozi kwa njia ya amani, baada ya kuiongoza nchi hiyo ya kusini mwa Afrika kwa karibu miongo minne.
Baada ya Spika wa Bunge la Zimbabwe kutoa tangazo la kujiuzulu kwa Mugabe, wananchi wa taifa hilo walijitokeza mabarabarani kwa shangwe, nderemo na vifijo kusherehekea habari hiyo.
Jeshi la Zimbabwe Jumatano lilitangaza Jumatano iliyopita kwamba, Mugabe na familia yake wapo katika kifungo cha nyumbani na kisha kumuondoa uongozini. Jeshi la Zimbabwe lilichukua hatua hiyo kama radiamali kwa hatua ya siku kadhaa zilizopita iliyochukuliwa na Mugabe ya kumuuzulu aliyekuwa Makamu wake Emmerson Mnangagwa ili aweze kumrithisha nafasi hiyo mkewe  Bi Grace Mugabe.

No comments:

Post a Comment