Saturday, November 4, 2017

MALENGO YA HATUA YA KIJESHI LA MAREKANI NCHINI SOMALIA

Malengo ya hatua za kijeshi za Marekani nchini Somalia
Kutokana na kushadidi mashambulizi ya kigaidi katika ardhi ya Somalia, ndege za kivita za Marekani kwa mara ya kwanza zimefanya mashambulizi dhidi ya ngome za makundi ya kigaidi katika nchi hiyo ya mashariki mwa Afrika.
Kundi la kigaidi la al Shabab ambalo limetangaza utiifu wake kwa viongozi wa kundi la al Qaida limekuwa likipigana na serikali ya Somalia kwa miaka kadhaa sasa. Kundi hilo liliteka miji kadhaa ya Somalia ikiwemo sehemu kubwa ya mji mkuu Mogadishu lakini Agosti mwaka 2011 lilifurushwa katika miji na maeneo mengi ya nchi hiyo kutokana na mashambulizi makubwa ya jeshi la Somalia likishirikiana na askari wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika. Hata hivyo kundi hilo la kigaidi bado linadhibiti miji kadhaa hususan maeneo ya vijijini ya Somalia. 

Wanamgambo wa kundi la al Shabab wenye makao yao Somalia 
Katika miezi ya hivi karibuni kundi hilo limebadili mbinu zake kwa kuzidisha mashambulizi ya kuvizia na kujilipua kwa mabomu badala ya kukabiliana moja kwa moja na vikosi vya jeshi la serikali ya Somalia na askari wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika. Mfano wa wazi wa ukweli huo ni shambulizi la wiki mbili zilizopita mjini Mogadishu ambalo limeua karibu watu mia nne. 
Kwa sasa Marekani, kama kawaida yake, imeparamia wimbi la kupambana na ugaidi na kundi la al Shabab na kuanza kuingilia moja kwa moja masuala ya ndani ya Somalia kwa kushambulia baadhi ya maeneo ya kundi hilo. Tunapotupia jicho sera na siasa za Marekani barani Afrika tunaona kuwa, japokuwa askari wa Marekani wamekuwepo kwa miaka mingi katika nchi mbalimbali za Afrika lakini nchi hiyo ilianzisha rasmi kambi na eneo lake la sita la kijeshi duniani mwaka 2007 kwa kuanzisha ofisi ya Komandi ya Jeshi ya Marekani Barani Afrika AFCOM kwa kifupi. Katika kipindi cha miaka kadhaa ya hivi karibuni Marekani imekuwa ikichunga na kufuatilia harakati zote za kijeshi barani Afrika na kufuatilia maslahi yake haramu katika nchi za bara hilo kwa kutumia njia na mbinu mbalimbali kama kutuma washauri wa masuala ya kijeshi na eti kutoa mafunzo kwa majeshi ya nchi za Kiafrika. Miongoni mwa malengo hayo yanayohudumia maslahi ya Marekani ni kufuatilia harakati za nchi wapinzani kama China na Russia huko Afrika, kufuatilia maslahi ya kiuchumi na kibiashara na kutumia maeneo ya kistratijia ya nchi za bara hilo kwa malengo ya kikoloni.  
Mchambuzi Nick Turse anasema: Kwa sasa Marekani ina vikosi vya jeshi katika nchi kadhaa za Afrika ambazo hazina tatizo lolote la makundi ya kigaidi kama lile la Daesh. Kwa msingi huo hatuwezi kusema kuwa operesheni zinazofanywa na wanajeshi hao wa Marekani ni sehemu ya mapambano dhidi ya ugaidi kama wanavyodai viongozi wa serikiali ya Washington".
Pamoja na hayo Marekani imezidisha kasi ya kutuma majeshi yake barani Afrika kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi kama inavyoshuhudiwa katika nchi kama Niger. Operesheni hizo zinaipa Marekani fursa ya kutimiza malengo yake ya kisiasa, kiuchumi na kijeshi.
Seneta Lindsay Graham wa Kamati ya Jeshi la Marekani anasema: Maana na hakika ya vita imo katika hali ya kubadilika na sasa tunashuhudia hatua zaidi barani Afrika.
Alaa kulli hal, ripoti mbalimbali zinaonesha kuwa, Washington ni miongoni mwa pande zilizoshiriki kuunda na kuanzisha makundi hatari ya kigaidi kama Daesh, Al Qaida na Twaliban. Hivyo basi mashambulizi ya sasa dhidi ya wapiganaji wa al Shabab ni ya kimaonyesho tu yanayofanyika kuwahadaa walimwengu au kwa shabaha ya kutimiza malengo ya kikoloni ya nyuma ya pazia.

Magaidi wa kundi la kitakfiri la Daesh 

No comments:

Post a Comment