Monday, November 27, 2017

UHURU KUAPISHWA LEO, KAMBI YA UPINZANI YASUSIA, YAITISHA MKUTANO JACARANDA

Uhuru kuapishwa leo, kambi ya upinzani yasusia, yaitisha mkutano Jacaranda
Mivutano ya kisiasa inaonekana kupamba moto zaidi leo nchini Kenya huku vyombo vya usalama vikilinda maeneo muhimu ya jiji la Nairobi kabla ya kuapishwa Rais Uhuru Kenyatta hii leo kwa ajili ya kipindi cha awamu ya pili.
Kenyatta ambaye alishinda uchaguzi wa marudio wa tarehe 26 Oktoba uliosusiwa na kambi ya upinzani, anaapishwa leo huku chama kikuu cha upinzani cha NASA kikiwataka wafuasi wake kususia sherehe hiyo na badala yake wakusanyike katika uwanja wa Jacaranda katika eneo la Embakasi mjini Nairobi kwa kile kinachosemekana ni kuomboleza mauaji ya wafuasi wa kinara wa kambi ya upinzani, Raila Odinga, waliouawa na maafisa wa polisi katika ghasia za uchaguzi wa rais.
Watu zaidi ya 70 waliuawa katika vurugu za kisiasa msimu huu wa uchaguzi, wengi wao wakiwa wameuawa kwa kupigwa risasi na polisi.
Polisi ya Kenya ikikabiliana na waandamanaji
Jumamosi iliyopita kamanda wa polisi mjini Nairobi, Japhet Koome alisema kuwa muungano wa upinzani wa NASA haujaitaarifu polisi kuhusu mkutano huo.
Koome alisisitiza kuwa jeshi la polisi litakabiliana na mtu yeyote atakayefanya mkutano bila ya kuliarifu jeshi hilo.
Rais Uhuru Kenyatta amewataka Wakenya kuungana na kufanya kazi pamoja baada ya ushindani wa kisiasa ili kulijenga taifa hilo.
Viongozi wa nchi kadhaa za kigeni wamealikwa katika sherehe ya kuapishwa Rais Uhuru Kenyatta.

No comments:

Post a Comment