Saturday, November 25, 2017

HASIRA ZA WATU WA BANGUI BAADA YA GARI LA MINUSCA KUMUUA MWANAFUNZI

Hasira za watu wa Bangui baada ya gari la MINUSCA kumuua mwanafunzi
Wananchi katika mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, Bangui wamebainisha ghadhabu zao baada ya mwanafunzi wa shule kupoteza maisha katika ajali iliyohusisha gari la askari wa Mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati MINUSCA.
Saa chache baada ya ajali hiyo, gari la Umoja wa Mataifa lililokuwa likipita Bangui lilishambuliwa na watu wenye hasira na kuchomwa moto hali iliyohatarisha maisha ya abiria waliokuwemo ambao walinusurika kuuawa.
Pia gari la zimamoto lililotumwa na MINUSCA lilishambuliwa na umati wa watu na kuharibiwa ambapo askari mmoja wa zimamoto alijeruhiwa. Matukio haya mawili kwa mujibu wa MINUSCA yalifuatiwa na mashambulizi mengine kadhaa dhidi ya magari ya mpango huo katika mji mzima wa Bangui.
MINUSCA inashirikiana na serikali, jeshi la polisi la nchi hiyo na wadau wengine kuhakikisha utulivu unarejea katika mji huo mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati.
MINUSCA imekaribisha taarifa ya serikali ya CAR baada ya tukio la ajali ya bahati mbaya  iliyokatisha maisha ya kijana mwanafunzi mjini Bangui.
MINUSCA imesikitishwa na kifo hicho na kuungana na serikali kutoa wito wa kudumisha utulivu miongoni mwa wananchi baada ya tukio hilo kuzusha maandamano ya ghasia mjini Bangui dhidi ya Umoja wa Mataifa.
Askari wa MINUSCA
Katika tukio hilo waziri wa habari na msemaji wa serikali ya CAR akaeleza kwamba MINUSCA ingependa kuwafahamisha kuwa gari lililomgonga na kumuua mwanafunzi huyo ni mali yake lakini lilikuwa likiendeshwa  na mwanajeshi wa jeshi la Jamhuri ya Afrika ya Kati (FACA).
Hayo yanajiri katika hali ambayo ukosoaji dhidi ya wanajeshi hao wa MINUSCA wapatao elfu 13  umeendelea kuongezeka kutokana na wananchi kutoridhishwa na utendaji wa vikosi hivyo katika kuwalinda raia wa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Askari hao wanalaumiwa kwa kutozuia mauaji ya Waislamu nchini humo.
Machafuko huko Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR) yalizuka mwaka 2013, baada ya waasi wa Seleka kumuondoa madarakani aliyekuwa rais wa nchi hiyo, François Bozizé. Baada ya rais Mwislamu, Michel Djotodia kuchukua mamlaka, waasi na magaidi wa Kikristo wenye misimamo ya kufurutu ada wa Anti-Balaka walianzisha mauaji ya kimbari dhidi ya jamii ya Waislamu, ambapo maelfu ya Waislamu waliuawa na wengine wengi kuwa wakimbizi.

No comments:

Post a Comment