Sunday, November 19, 2017

WIMBI LA KAMATAKAMATA SAUDIA KWA MADAI YA UFISADI LAENDELEA, SASA NI VIONGOZI WA KIJESHI

Wimbi la kamatakamata Saudia kwa madai ya ufisadi laendelea, sasa ni viongozi wa kijeshi
Katika muendelezo wa wimbi jipya la kamatakamata ambalo halijawahi kushuhudiwa nchini Saudia kwa madai ya kufanyika mageuzi na kupambana na ufisadi viongozi wa ngazi ya juu wa kijeshi wametiwa nguvuni nchini humo.
Hayo ni kwa mujibu wa baadhi ya magazeti mashuhuri ya Uingereza ambayo yametangaza kwamba, katika hali ambayo Mohammad Bin Salman Al Saud anadai kufanya marekebisho nchini Saudia, uhalisia wa mambo ni kwamba mrithi huyo wa kiti cha ufalme anapambana na wapinzani wake tu.
Mohammad Bin Salman Al Saud akiwa na Rais Donald Trump wa Marekani
Chanzo kimoja ndani ya ukoo wa kifalme wa Aal-Saud ambacho hakikutaka kutaja jina lake kimefichua kwamba, hadi sasa viongozi 14 wa ngazi ya juu wa gadi ya taifa na Wizara ya Ulinzi ya Saudia ambao wamestaafu, wametiwa nguvuni kwa tuhuma za kushiriki katika kutia saini mikataba ya kifedha inayotia shaka. Kukamatwa viongozi hao wa kijeshi kumeifanya idadi ya watu waliokamatwa katika wiki za hivi karibuni ndani ya taifa hilo, kupindukia 200 ambapo kati yao ni mawaziri wanne na wanamfalme 11 akiwemo Mrithi wa Kiti cha Ufalme wa zamani wa nchi hiyo.
Jinai za Saudi Arabi nchini Yemen
Baadhi ya maafisa wa jeshi wamefichua kwamba kutiwa mbaroni kwa makamanda hao wa kijeshi kumetokana na kushindwa kwao katika vita dhidi ya Yemen. Gazeti la Wall Street Journal limeandika kwamba, Mohammad Bin Salman Al Saud ambaye ameanzisha kile kinachotajwa kuwa ni kupambana na ufisadi wa kiuchumi nchini humo, mbali na kuwatia mbaroni mamia ya shakhsia wakubwa wakiwamo wanamfalme na matajiri wakubwa wa nchi hiyo, pia amefunga maelfu ya akaunti za watu hao. Baadhi ya vyanzo vya habari vimeandika kwamba, Bin Salman ametoa sharti la kuingizwa karibu asilimia 70 ya utajiri wao serikalini kama njia ya wao kuachiliwa huru.

No comments:

Post a Comment