Monday, January 29, 2018

SAEB ERAKAT: VITENDO VYA MAREKANI VINACHOCHEA MACHAFUKO MASHARIKI YA KATI

Saeb Erakat: Vitendo vya Marekani vinachochea machafuko Mashariki ya Kati
Katibu wa kamati ya utendaji ya Harakati ya Ukombozi wa Palestina (PLO) amesema kuwa, hatua na vitendo vya Marekani vimekuwa vikichochea vurugu na machafuko katika eneo la Mashariki ya kati.
Saeb Erakat, amesema bayana kwamba, hatua ya hivi karibuni ya Rais Donald Trump wa Marekani kuhusiana na Beitul-Muqaddas na wakimbizi wa Palestina ni ushahidi wa wazi wa kuchochea na kueneza machafuko na vurugu katika eneo la Mashariki ya Kati.
Afisa huyo mwandamizi wa Harakati ya Ukombozi wa Palestina (PLO) amebainisha kwamba, uamuzi wa Trump wa kuitambua Beitul Muqaddas kuwa eti ni mji mkuu wa utawala vamizi wa Israel na kutaka uanzishwe mchakato wa kuhamishiwa ubalozi wa Washington katika mji huo unaonyesha msimamo mkali, uenezaji vurugu na machafuko, umwagaji damu na chokochoko alizo nazo rais huyo wa Marekani.
Msikiti wa al-Aqswa, unaopatikana katika mji wa Beitul-Muqaddas Palestina

Saeb Erakat amesema, hatua hiyo ya Trump si chokochoko kwa Palestina tu bali kwa eneo zima la Mashariki ya Kati.
Katibu huyo wa kamati ya utendaji ya Harakati ya Ukombozi wa Palestina (PLO) amesisitiza kuwa, njia pekee ya kurejeshwa amani na utulivu katika eneo la Mashariki ya Kati ni kukomeshwa uvamizi wa Israel na kuimarishwa mamlaka ya kujitawala Palestina mji mkuu wake ukiwa Beitul-Muqaddas.

No comments:

Post a Comment