Sunday, January 28, 2018

MPINZANI WA EL SISI KATIKA UCHAGUZI UJAO MISRI ATUPWA KATIKA JELA YA KIJESHI

Mpinzani wa el Sisi katika uchaguzi ujao wa Misri atupwa katika jela ya kijeshi
Wakili wa mkuu wa zamani wa jeshi la Misri ambaye ametangaza kuchuana na Rais Abdul Fattah el Sisi katika uchaguzi ujao wa rais nchini humo amesema kuwa, mteja wake emepelekwa katika jela ya kijeshi.
Habari hiyo imetangazwa leo na gazeti la Ra'y al Yaum na kumnukuu Naser Amin, wakili wa Sami Hafez Anan, mkuu wa zamani wa jeshi la Misri akiandika katika ukurasa wake wa Facebook wamba ameruhusiwa kwenda kuonana na Anan katika jela ya kijeshi.
Rais Abdul Fattah el Sisi wa Misri

Komandi Kuu ya vikosi vya ulinzi vya Misri, Jumanne ilivyopita ilitoa tamko na kumlaumu Anan kwa kutangaza kushiriki katika uchaguzi wa rais wa nchi hiyo. Aidha komandi hiyo ilimtuhumu Anan kuwa amevunja sheria na kutoa maneno ya kichochezi dhidi ya vikosi vya ulinzi vya Misri.
Tuhuma nyingine alizobebeshwa Sami Hafez Anan baada ya kutangaza kuwa atachuana na Rais Abdul Fattah el Sisi katika uchaguzi ujao ni pamoja na madai ya kughushi nyara na vyeti rasmi.
Tayari Ahmad Shafiq, waziri mkuu wa zamani wa Misri ametangaza kujitoa katika kinyang'anyiro hicho.
Khaled Ali, mwanasiasa mwingine aliyetangaza kuchuana na el Sisi naye ameshatangaza kujitoa katika kinyang'anyiro hicho. Kwa hali hiyo, hivi sasa Rais wa Misri Abdul Fattah el Sisi amebakia peke yake katika uchaguzi huo bila ya mpinzani yeyote.
Uchaguzi wa Rais wa Misri unatarajiwa kufanyika kati ya tarehe 26 na 28 Machi mwaka huu wa 2018

No comments:

Post a Comment