Saturday, September 23, 2017

KENYA YATAKA DUNIA ISAIDIE KIKOSI CHA AAMISOM KULINDA AMANI SOMALIA

Kenya yataka dunia isaidie kikosi cha AMISOM kulinda amani Somalia
Kenya imeitaka jamii ya kimataifa iongeze zaidi usaidizi wake kwa Kikosi cha Umoja wa Afrika cha Kulinda amani Somalia, AMISOM ili kiweze kushughulikia kwa kina vitisho vya usalama kabla ya kuanza kutekelezwa mpango wa kupunguza idadi ya askari wake.
Ombi hilo limo katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Balozi Amina Mohammed wakati akihutubia kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani siku ya Ijumaa.
Amesema ili kuimarisha mafanikio yaliyokwishapatikana, Kenya inaunga mkono azimio la Baraza la Usalama kuhusu msingi ya AMISOM. Aidha amesema zaidi ya yote kuna haja ya kuwepo msaada wa kuwezesha ujenzi mpya wa Somalia, kukiwemo kuwezesha serikali kutoa huduma za msingi.

Askari wa kulinda amani wa AMISOM 
Kwingineko katika hotuba yake, Balozi Amina amezungumzia pia mabadiliko ya tabianchi akisema kuwa pamoja na kusababisha mizozo ya rasilimali za maji na ardhi, yanagharimu asilimia 3 ya pato la ndani la taifa kila mwaka.
Hali kadhalika Waziri huyo wa Mambo ya Nje wa Kenya amezungumza kuhusu suala la wakimbizi kwa kutambua kuwa Kenya tangu miaka ya 60 imehifadhi wakimbizi kutoka nchi jirani ikiwemo Somalia, hatua ambayo imekuwa na changamoto nyingi zikiwemo za kiusalama.
Amesema ni kwa mantiki hiyo ndipo mwaka 2013 Kenya ilitia saini makubaliano ya pande tatu baina yake, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR na serikali ya Somalia kwa lengo la kuwezesha wakimbizi kurejea nyumbani kwa hiari.

No comments:

Post a Comment