Wednesday, September 13, 2017

POLISI KENYA YATUMIA GESI YA KUTOA MACHOZI BAADA YA WANAWAKE KUVAMIWA MUKUTANONI

Polisi nchini Kenya katika mji wa Kisumu magharibi mwa nchi hiyo leo wamenyunyiza angani gesi ya kutoa macho na kufyatua risasi ili kuwatawanya vijana wa kiume waliovamia hoteli moja na kuanza kuwapiga wanawake waliokuwa wakihudhuria mkutano wa uchaguzi mjini humo.
Tarehe Nane mwezi Agosti mwaka huu Kenya ilifanya chaguzi za Rais, bunge na serikali za mitaa, hata hivyo wiki tatu baadaye mahakama ya juu ya nchi hiyo ilitengua matokeo ya uchaguzi wa rais ikiashiria kuwepo kasoro na dosari katika mfumo wa utoaji matokeo. Uchaguzi wa marudio umepangwa kufanyika Oktoba 17 mwaka huu.
Jumuiya ya Wanawake wa Kikristo ya Kenya leo Jumatano ilikuwa ikifanya mkutano wake kuhusu marudio ya uchaguzi huo tajwa mara ikivamiwa na kundi la vijana wa kiume walioingia hotelini mahali mkutano huo ulipokuwa ukifanyikika. Hayo yameelezwa na Joseph Keitany kutoka polisi ya kaunti ya Kisumu. Mji wa Kisumu unafahamika kama ngome ya kiongozi wa upinzani Kenya Raila Odinga.
Raila Odinga, Kiongozi wa upinzani Kenya (NASA)  
Vijana hao wavamizi wameiba komyuta mpakato na fedha za wanawake waliokuwa mkutanoni. Vijana hao wavamizi wamedai kuwa wanawake hao walikuwa wakinunua vitambulisho vya kupigia kura. Washiriki wa mkutano huo kwa upande wao wamekanusha madai hayo na kusema kuwa waliitisha mkutano wao ili kutafuta njia ya kushajiisha upigaji kura wa amani. Ripoti zinaeleza kuwa wanawake kadhaa walijeruhiwa katika hujuma na uvamizi uliofanywa na vijana hao.../

No comments:

Post a Comment