Friday, September 22, 2017

KIM JONG-UN: TRUMP ANA MATATIZO YA AKILI, NITAMFANYA AJUTIE MATAMSHI YAKE YA VITISHO

Kim Jong-un: Trump ana matatizo ya kiakili, nitamfanya ajutie matamshi yake ya vitisho
Kim Jong-un, Kiongozi wa Korea Kaskazini amejibu matamshi ya vitisho ya Rais Donald Trump wa Marekani na kusema kuwa, rais huyo wa Marekani ana matatizo ya kiakili na kwamba atalipa gharama ya matamshi yake ya vitisho dhidi ya Pyongyang.
Katika sehemu nyingine, kiongozi huyo wa Korea Kaskazini sambamba na kuashiria matamshi ya hivi karibuni ya rais wa Marekani aliyetishia kuishambulia Pyongyang amesema kuwa, nitamfanya kiongozi huyo wa Marekani ajutie matamshi yake aliyoyatoa katika mkutano mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) kwa kuitishia Korea Kaskazini.
Mgogoro kati ya Korea Kaskazini na Marekani wazidi kuongezeka, huku walimwengu wakimkosoa Trump
Itakumbukwa kuwa Jumatatu iliyopita katika mkutano huo wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Trump alizishambulia nchi kadhaa za dunia na kutoa vitisho dhidi ya nchi hizo badala ya kuzungumzia amani na usalama. Akiizungumzia Korea Kaskazini Trump alisema, Marekani italazimika kuiangamiza kikamilifu nchi hiyo ya Asia, isipokuwa kama Pyongyang itakubali kurudi nyuma kuhusiana na miradi yake ya silaha za nyuklia. Kadhalika rais huyo wa Marekani ambaye hadi sasa ameendelea kukosolewa duniani kutokana na matamshi yake yasiyo ya mantiki, alimtaja Kim Jong-un kwa jina la 'Mtu wa Makombora' na kuongeza kuwa, kiongozi huyo wa Korea Kaskazini anafanya mambo yatakayopelekea yeye, mfumo na raia wa nchi yake kujiangamiza.
Moja ya makombora yanayoitia kiwewe Marekani na kumfanya Trump atokwe na matamshi ya ajabu
Kama hiyo haitoshi usiku wa Alkhamisi ya jana Trump alisaini dikrii mpya ambayo inaitaka Wizara ya Hazina ya Marekani kuwawekea vikwazo watu au taasisi za kigeni zinazoshirikiana kibiashara na Korea Kaskazini. Kabla ya hapo pia Korea Kaskazini iliwekewa vikwazo vipya na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutokana na kuyafanyia majaribio makombora yake ya balestiki na silaha za nyuklia. Pyongyang imekuwa ikisisitiza kuwa, itaendelea kujiimarisha kijeshi ili kukabiliana na chokochoko za Marekani na washirika wake dhidi yake.

No comments:

Post a Comment