Monday, January 30, 2017

KUONGEZEKA CHUKI DHIDI YA WAISLAMU AMERIKA KASKAZINI

Baada ya kuongezeka hisia za chuki na uadui dhidi ya Waislamu huko Amerika Kaskazini hususan baada ya kuingia madarakani Rais Donald Trump nchini Marekani, hivi sasa matokeo mabaya ya jambo hilo yameanza kuonekana.
Jana Jumatatu, maafisa wa Canada walitangaza habari ya kushambuliwa msikiti mmoja na kuuliwa Waislamu watano huko Quebec na kujeruhiwa wengine kadhaa. Waislamu 40 walikuwemo msikitini humo wakati watu watatu wenye chuki za kidini walipowashambulia kwa risasi. Polisi wa Quebec wamesema. watu wawili kati ya watatu walioushambulia kwa risasi msikiti huo, wametiwa mbaroni.
Komesha chuki dhidi ya Waislamu
Tukio hilo linaonesha ni kiasi gani propaganda mbaya dhidi ya Waislamu zilivyo na madhara kiasi kwamba zinaweza kusababisha mauaji ya Waislamu. Hivi sasa propaganda za chuki dhidi ya Waislamu zimeshika kasi zaidi nchini Marekani, lakini madhara ya propaganda hizo chafu yanaonekana hadi nje ya mipaka ya Marekani. Ikumbukwe kuwa propaganda za chuki dhidi ya Waislamu nchini Canada ni ndogo ikilinganishwa na Marekani. Kabla ya hapo pia msikiti wa Ranchview katika mji wa Calgary wa jimbo la Alberta huko Canada ulishambuliwa na watu wenye chuki za kidini. Shambulio la jana Jumatatu dhidi ya Waislamu wa Canada limefanyika katika hali ambayo wiki za hivi karibuni, misikiti ya nchi hiyo ilifungua milango yake kwa ajili ya kuwahudumia watu wasio na makazi nchini humo.
Nukta ya kuzingatiwa hapa ni namna shambulio hilo lilivyosadifiana kwa kiasi fulani na amri iliyotolewa na Rais wa Marekani Donald Trump ya kuwazuia raia wa nchi saba za Kiislamu kuingia Marekani. Hatua hiyo ya serikali ya Marekani inakinzana kikamilifu na sehria za kimataifa. Hatua hiyo imelalamikiwa vikali kote ulimwenguni. Waendesha Mashtaka Wakuu wa majimbo 16 ya Marekani yakiwemo ya California, New York na Pennsylvania walitoa tamko siku ya Jumapili na kulaani amri ya Trump ya kuwapiga marufuku raia wa nchi hizo za Kiislamu kuingia Marekani.
Moja ya misikiti ya Waislamu wa Canada mjini Calgary katika jimbo la Alberta

Vitendo vya chuki na uadui dhidi ya Waislamu vimeongezeka sana huko Amerika Kaskazini tangu baada ya kutokea shambulio la kigaidi katika mji wa San Bernardino wa jimbo la California huko Marekani mwezi Disemba 2015. Vile vile mahambulizi ya kigaidi yaliyotokea hivi karibuni barani Ulaya yamezidi kuwapa kisingizio maadui wa Uislamu kuwasakama Waislamu na kudhihirisha waziwazi chuki zao dhidi ya wafuasi wa dini hiyo tukufu ya Mwenyezi Mungu. Wakati wa kampeni za uchaguzi nchini Marekani, Trump alitangaza kuwa atapiga marufuku kuingia Waislamu nchini humo kama njia ya kukabiliana na ugaidi. Matamshi hayo ya chuki yalilaaniwa vikali katika pembe mbalimbali za dunia, ndani na nje ya Marekani. Hata hivyo, rais huyo mwenye chuki za kidini hakujali malalamiko hayo makubwa ya walimwengu na ametoa amri ya kuzuia kijeuri na kinyama raia wa nchi saba za Waislamu kuingia nchini humo.
Waislamu wa Marekani wakilalamikia unyanyasaji
Hivi sasa kumejitokeza wasiwasi mkubwa wa kuongezeka vitendo vya kikatili na vya chuki za kidini dhidi ya Waislamu wasio na hatia. Shambulio la kikatili lililofanywa dhidi ya Waislamu tena nchini Canada ambako hakuna historia ya mashambulizi makali kama hayo dhidi ya Waislamu linaonesha kuwa wingu jeusi la chuki na uadui wa kidini dhidi ya Waislamu limezidi kutanda huko Amerika Kaskazini. Hali hiyo mbaya si tu ni hatari kubwa kwa usalama wa kikazi na kimakazi wa Waislamu wa nchini Marekani na Canada, lakini pia Waislamu wa nchi hizo hivi sasa wana hofu ya kupoteza roho zao hata wanapotembea mitaani na wanapokuwa kwenye nyumba zao za ibada, licha ya mapenzi makubwa wanayowaonesha wafuasi wa dini nyinginezo na kuwathibitishia kuwa propaganda zote dhidi yao zinatokana tu na chuki za kidini za maadui wa Uislamu.  

No comments:

Post a Comment