Tuesday, January 31, 2017

AU: AFRIKA IKO TAYARI KUPOKEA WAKIMBIZI BAADA YA USKUFUNGA MIPAKA YAKE

Umoja wa Afrika umesema nchi za Afrika ziko tayari kupokea wakimbizi baada ya Marekani kupasisha sheria tata ya kibaguzi dhidi ya wakimbizi.
Akizungumza pambizoni mwa mkutano wa AU unaomalizika leo mjini Addis Ababa, Ethiopia, Smail Chergui, Kamishna Mkuu wa Masuala ya Amani na Usalama wa Umoja wa Afrika amesema kuwa, bara la Afrika linafaa kuwa mfano mzuri wa kuigwa duniani kwa kuendelea kuwapokea wakimbizi na wahamiaji, baada ya Marekani kutangaza kuwa itafunga mipaka yake kuzuia wakimbizi na wahamiaji kuingia nchini humo.
Ameongeza kuwa, historia inaonyesha kuwa nchi za Kiafrika zimekuwa zikiwapokea wakimbizi kwa moyo mkunjufu huku akitoa mfano wa Kenya, ambayo ina kambi kubwa zaidi ya wakimbizi duniani ya Dadaab.
Wakimbizi wa Iraq
Chergui amesema vikosi vya kieneo vinapigana kufa kupona kuyatokomeza makundi ya kigaidi kama al-Shabaab na Boko Haram, hivyo haingii akilini Marekani kutangaza kuwafungia nje wakimbizi kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi.
Smail Chergui, Kamishna Mkuu wa Masuala ya Amani na Usalama wa Umoja wa Afrika amesema kuwa, Marekani inafaa kutilia maanani wajibu wake wa kimataifa inapochukua uamuzi wowote wa kibaguzi na ambao unaweza kuhatarisha zaidi maisha ya wakimbizi.
Mwenyekiti anayeondoka wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Nkosazana Dlamini-Zuma hapo jana alikosoa mikakati ya kibaguzi inayochukuliwa na serikali ya Rais Donald Trump wa Marekani kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. 

No comments:

Post a Comment