Monday, December 25, 2017

SAUDI ARABIA ILIMDHALILISHA WAZIRI MKUU WA LEBANON, SAAD HARIRI

Saudi Arabia ilimdhalilisha Waziri Mkuu wa Lebanon, Saad Hariri
Saudi Arabia ilimdhalilisha vibaya sana Waziri Mkuu wa Lebanon Saad Hariri katika safari yake ya hivi karibuni mjini Riyadh wakati alipolazimishwa kusoma taarifa ya kujiuzulu mbele ya televisheni.
Gazeti la The New York Times limeandika Hariri alikuwa ni kama mateka na alilazimishwa kusoma barua ya kujiuzulu akiwa sehemu isiyojulikana Saudia mnamo Novemba 4 ambapo pia alitoa tuhuma zisizo na msingi kuwa eti Iran na Hizbullah zinaingilia masuala ya ndani ya eneo na hivyo amelazimika kujiuzulu.
Lakini Rais wa Lebanon Michel Aoun alishuku kuwa Hariri alijiuzulu chini ya mashinikizo na hivyo hakukubali hatua hiyo na alimtaka arejee nyumbani kutoka Saudia. Vyombo vya usalama vya Lebanon vilithibitisha kuwa Hariri  alilazimishwa kujiuzulu na hatimaye alirejea Lebanon Novemba 22 baada ya upatanishi wa Ufaransa. Hariri hatimaye alibatilisha uamuzi wake wa kujiuzulu Disemba 5.
Rais Michel Aoun wa Lebanon
Taarifa zinasema kuwa Hariri alipowasili Saudia alidhani atapokewa rasmi lakini alipofika katika kasri ya mfalme alipokonywa simu zake za mkononi na walinzi wake walitimuliwa huku wakitukanwa na maafisa wa usalama wa Saudia. Hapo alikabidhiwa barua ya kujiuzulu na akaambiwa aisome katika televisheni ya taifa ya Saudia. Badala ya kuenda hotelini alipelekwa katika nyumba maalumu iliyokuwa chini ya ulinzi mkali wa askari wa Saudia na wala hakuruhusiwa kuonana na mke na watoto wake. Lengo la Saudia lilikuwa ni kupunguza ushawishi wa harakati ya Hizbullah katika serikali ya Lebanon lakini njama hizo zimegonga mwamba. 

No comments:

Post a Comment