Monday, December 25, 2017

MAGAIDI WA ISIS WASHAMBULIA IDARA YA USALAMA AFGHANISTAN,

Magaidi wa ISIS washambulia Idara ya Usalama Afghanistan, Sita wauawa
Kundi la kigaidi la ISIS limedai kuhusika na hujuma ya kigaidi iliyolenga Idara ya Usalama wa Taifa ya Afghanistan katika mji mkuu wa nchi hiyo, Kabul.
Watu wasiopungua sita wameuawa katika hujuma hiyo huku wengine wawili wakijeruhiwa baada ya gaidi aliyekuwa amejishehenesha mabomu kujiripua katika mlango mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa (NDS) mjini Kabul.
Hujuma hiyo imetokea wakati wafanyakazi walipokuwa wakiwasili katika ofisi kwa ajili ya kuanza kazi. Taarifa zinasema mwanamke mmoja ni miongoni mwa waliouawa katika hujuma hiyo.
Wiki iliyopita kituo kimoja cha Idara ya Usalama wa Taifa cha Afghanistan kilishambuliwa na magaidi na katika makabiliano hayo magaidi watatu waliuawa baada ya masaa matatu ya mapigano.
Wanajeshi wa Afghanistan katika oparesheni dhidi ya magaidi
Hayo yanajiri wakati Mjumbe maalumu wa rais wa Russia nchini Afghanistan akiwa ametoa indhari kuwa wanachama zaidi ya elfu kumi wa kundi la kigaidi na ukufurishaji la ISIS hivi sasa wako nchini Afghanistan na kwamba idadi yao inazidi kuongezeka kutokana na kubadilisha maskani yake kundi hilo baada ya kusambaratishwa katika nchi za Syria na Iraq.
Zamir Kabulov ametoa indhari hiyo katika mahojiano aliyofanyiwa na shirika la habari la Sputnik na kuongeza kuwa Russia ina wasiwasi wa kupanuka harakati za ISIS kwenye mikoa ya kaskazini mwa Afghanistan inayopakana na Tajikistan na Turkmenistan.
Ikumbukwe kuwa hivi sasa kuna wanajeshi wapatao 11,000 wa Marekani nchini Afghanistan. Washington na washirika wake katika muungano wa kijeshi wa NATO waliivamia kijeshi nchi hiyo mwaka 2001 kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi lakini si tu kuwa hawajafanikiwa bali pia ugaidi umeongezeka nchini humo.

No comments:

Post a Comment