Wednesday, December 27, 2017

JESHI LA UGANDA LAUA WAASI ZAIDI YA 100 WA ADF KONGO DR

Jeshi la Uganda laua waasi zaidi ya 100 wa ADF Kongo DR
Jeshi la Uganda limetangaza habari ya kuua wanachama wasiopungua 100 wa kundi la waasi wa ADF katika makabiliano makali yaliyojiri mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Taarifa iliyotolewa jana Jumatano na Jeshi la Ulinzi la Uganda UPDF imesema kuwa, vikosi vyake vimefanya mashambulizi ya angani na ardhini dhidi ya maficho ya waasi hao katika mpaka wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki na Kongo DR, na kufanikiwa kuua zaidi ya 100 miongoni mwao na kujeruhi wengine wengi.
Hujuma hii dhidi ya waasi wa ADF imefanyika siku chache baada ya Uganda na Kongo DR kukubaliana kuimarisha utaratibu wa mawasiliano na kupeana taarifa za kiintelijensia kwa ajili ya kupambana na waasi hao wanaotokea Uganda, ambao wanaendesha harakati zao mashariki mwa DRC.
Askari wa Umoja wa Mataifa DRC
Itakumbukwa kuwa, askari 14 wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ)  waliuawa mwanzoni mwa mwezi huu wa Disemba, na 44 wengine walijeruhiwa katika kambi ya Semuliki mkoani Kivu Kaskazini katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, kufuatia hujuma ya waasi hao wa ADF.
Wanajeshi waliouawa walikuwa ni sehemu ya askari 3,000 wa timu ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa MONUSCO yenye askari kutoka Tanzania, Malawi na Afrika Kusini.

No comments:

Post a Comment