Wednesday, December 20, 2017

MAREKANI YATENGWA KATIKA KIKAO BARAZA LA USALAMA KILICHAJADILI MAPATANO YA NYUKLIA YA IRANI

Marekani yatengwa katika kikao cha Baraza la Usalama kilichojadili mapatano ya nyuklia ya Iran
Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa ameashiria kufanyika Kikao cha Baraza la Usalama la umoja huo kuhusu azimio nambari 2231 la mapatano ya nyuklia ya Iran na kusema washiriki wa kikao hicho walitangaza kuunga mkono mapatano hayo na kwamba kikao hicho kilithibitisha namna Marekani ilivyotengwa.
Siku ya Jumanne, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liliitisha kikao kujadili mapatano ya nyuklia ya Iran yanayojulikana kama Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekelezwaji JCPOA yaliyofikiwa mwaka 2015 baina ya Iran na Russia, China, Uingereza, Ufaransa, Marekani na Ujerumani. Baada ya mapatano hayo, Baraza la Usalama lilipasisha azimio nambari 2231 kuhusu kuunga mkono utekelezwaji mapatano hayo.
Katika kikao cha Jumanne, Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Nikki Haley alitengwa na washiriki wote wa kikao wakiwemo Jeffrey Feltman Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Joanne Adamson Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya ambao wote waliunga mkono JCPOA.
Akizungumza katika kikao hicho, Gholamali Khoshroo mwakilishi wa kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa alisisitiza kuwa, Iran, kinyume na Marekani, inafungamana kikamilifu na JCPOA na hilo limethibitishwa katika ripoti 9 za Wakala wa Nyuklia wa Umoja wa Mataifa IAEA.
Gholamali Khoshroo mwakilishi wa kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa
Mwakilishi wa Iran pia akijibu madai ya Nikki Haley katika kikao hicho kuwa eti Iran inatoa msaada wa kijeshi kwa Yemen alisema: "Mwakilishi wa Marekani anatoa tuhuma bandia dhidi ya Iran pasina kuashiria namna harakati za kijeshi za serikali yake zinavyovuruga uthabiti wa eneo kwa kuuza silaha zenye thamani ya mabilioni ya dola na kukabidhi baadhi ya silaha hizo kwa makundi ya kigaidi kama vile ISIS au Daesh."
Katika kikao hicho Feltman pia amepinga madai hayo ya Haley.
Ikumbukwe kuwa tokea Machi 2015 hadi sasa, Marekani imekuwa ikiunga mkono hujuma ya kinyama ya Saudi Arabia dhidi ya Yemen na imekuwa ikiupa utawala huo wa Riyadh silaha ambazo hadi sasa zimewaua Wayemen zaidi ya 13,000, wengi wakiwa ni wanawake na watoto. 

No comments:

Post a Comment