Sunday, April 8, 2018

UN: MYANMAR HAIPO TAYARI KUWAPOKEA WAKIMBIZI WAROHINGYA

UN: Myanmar haipo tayari kuwapokea wakimbizi Warohingya

Umoja wa Mataifa umesema Myanmar haipo tayari kuwapokea malaki ya wakimbizi Waislamu wa Rohingya wanaoishi kambini katika nchi jirani ya Bangladesh.

Ursula Mueller, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Kibinadamu ameyasema hayo baada ya kufanya ziara ya siku sita nchini Myanmar na kubainisha kuwa, mazingira yalivyo hivi sasa nchini humo hayaruhusu kurejea nyumbani wakimbizi wa Rohingya.

Amesema, "Kutokokana na kile nilichokishuhudia binafsi, hali mbaya ya kiafya, ukosefu wa dhamana ya usalama na kuendelea kufurushwa kwa wakimbizi wengine kutoka mkoani Rakhine ni miongoni mwa mambo yanayoonyesha kuwa Myanmar haijajiandaa kuwapokea Warohingya hao walioko Bangladesh.

Wakimbizi Waislamu wa Rohingya

Mwezi uliopita, Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa ilitahadharisha kuhusiana na kuendelea mauaji ya kizazi yanayofanywa na serikali ya Myanmar dhidi ya Waislamu wa jamii ya Rohingya magharibi mwa nchi hiyo, huku wakimbizi hao wakisisitiza watarejea nchini Myanmar kwa masharti mawili; mosi, wadhaminiwe usalama wao na pili wapewe uraia.

Mauaji hayo ya umati dhidi ya Waislamu nchini Myanmar tangu mwezi Agosti mwaka jana katika mkoa wa Rakhine magharibi mwa nchi, yamepelekea zaidi ya Waislamu laki saba kukimbilia hifadhi katika nchi jirani ya Bangladesh.

No comments:

Post a Comment