Thursday, April 5, 2018

JESHI LA YEMEN LASHAMBULIA TENA KWA KOMBORA SHIRIKA LA MAFUTA LA SAUDIA ARAMCO

Jeshi la Yemen lashambulia tena kwa kombora Shirika la Mafuta la Saudia Aramco
Kwa mara nyingine, jeshi la Yemen kwa kushirikiana na Harakati ya Kiislamu ya Answarullah, limeshambulia kwa kombora ghala la kuhifadhia mafuta la Shirika kubwa la Mafuta nchini Saudia Aramco katika mji wa Jizan, kusini magharibi mwa nchi hiyo.
Taarifa iliyotolewa na jeshi la Yemen imesema kuwa, kombora lililotumika kushambulia ghala hilo la mafuta ni aina ya Badr-1 na kwamba lilifyatuliwa jana usiku. Wakati huo huo duru za serikali ya Saudia zimedai kwamba, ngao ya kuzuia makombora ya nchi hiyo lilifyatua kombora na kuliharibu kombora hilo la jeshi la Yemen kabla ya kufika eneo lengwa.
Kombora la Badr-1 la Answarullah
Hili ni shambulio la pili la kombora la balestiki kufanywa na jeshi la Yemen na Harakati ya Answarullah dhidi ya shirika la mafuta la Saudia katika kipindi cha wiki moja. Alkhamisi iliyopita pia, jeshi la Yemen lililishambulia kwa kombora la balestiki shirika kubwa la uzalishaji mafuta la Saudia ambapo wakati viongozi wa Riyadh wakidai pia kwamba kombora hilo lilizuiliwa, baadhi ya duru zilisema kuwa, kombora hilo lilifika eneo lengwa. Kadhalika viongozi wa Saudia walidai kwamba tarehe 25 mwezi jana, jumla ya makombora saba yalivurumishwa kutoka nchini Yemen ambapo matatu kati yake yalianguka katika mji wa Riyadh.
Hujuma za Saudia dhidi ya maeneo ya raia nchini Yemen
Mashambulizi ya makombora ya harakati ya Answarullah na jeshi la Yemen yanajiri huku hujuma za Saudia kwa kushirikiana na nchi kadhaa za Kiarabu na Magharibi dhidi ya Yemen zikiwa zimeingia mwaka wa nne. Aidha uwezo wa makombora ya harakati hiyo unashuhudiwa huku Yemen ikiwa imewekewa mzingiro wa kila upande na nchi wavamizi.

No comments:

Post a Comment