Monday, April 9, 2018

ARAB LEAGUE YALAANI JINAI ZA KARIBUNI ZA UTAWALA WA KIZAYUMI DHIDI YA WAPALESTINA

Arab League yalaani jinai za karibuni za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League) amelaani jinai za wanajeshi wa utawala wa Kizayuni dhidi ya raia wa Palestina.
Ahmad Abul Ghait amelaani jinai za utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Ghaza na kulitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutekeleza majukumu yake katika kuwalinda raia wa Palestina mbele ya jinai za utawala wa Israel. 
Ahmad Abul Gheit, Katibu Mkuu wa Arab League
Mahmoud Afifi, msemaji wa Katibu Mkuu wa Arab League pia jana alitahadharisha kuhusu kuendelea jinai hizo za utawala wa Kizayuni huko Ghaza na kueleza kuwa hali ya mambo katika eneo hilo inahitajia uingiliaji wa jamii ya kimataifa. Afifi alisisitiza kuwa wale wote waliohusika na jinai dhidi ya raia wa Palestina huko Ghaza inapasa wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria. 
Maelfu ya Wapalestina tarehe 30 mwezi uliopita wa Machi walifanya maandamano ya amani katika maadhimisho ya mwaka wa 42 wa "Siku ya Ardhi" kuelekea katika mpaka wa Ghaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu; ambapo waandamanaji hao walikabiliwa na hujuma na mashambulizi ya utawala wa Israel. Katika siku hiyo ya maandamano hayo ya amani chini ya anuani ya "Haki ya Kurejea", Wapalestina 17 waliuliwa shahidi na wengine zaidi ya 1400 walijeruhiwa. Tangu siku hiyo hadi sasa, Wapalestina wasiopungua 29 wameshauliwa shahidi kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa Israel na wengine zaidi ya 3000 wamejeruhiwa. Nchi nyingi na vile vile taasisi za kimataifa zimelaani jinai hizo za Wazayuni.

No comments:

Post a Comment