Monday, April 9, 2018

HATIMAYE SPIKA WA BUNGE LA SOMALIA AJIUZURU

Hatimaye Spika wa Bunge la Somalia ajiuzulu
Spika wa Bunge la Federali la Somalia, Mohamed Sheikh Osman Jawari, hatimaye amejiuzulu baada ya nchi hiyo ye Pembe ya Afrika kushuhudia taharuki na mgogoro mkubwa wa kisiasa kwa wiki kadhaa.
Dahir Amin Jesow, mmoja wa wabunge ameliambia shirika la habari la Reuters kuwa, "Asubuhi ya leo tulikuwa tunajiandaa kujadili hoja ya kumuondoa madarakani Spika, mara ghafla Naibu Spika akaja na barua ya kujiuzulu Spika huyo na kuisoma mbele yetu. Tumepongeza hatua hiyo ya kujiuzulu ambayo inakubalika kikatiba, na tunatumai huu ndio mwisho wa mzozo wa kisiasa nchini." 
Wiki iliyopita, Rais Mohammed Abdullahi Farmajo wa Somalia alisimamisha kikao kingine cha Bunge kilichokusudia kujadili hoja hiyo ya kumuengua madarakani Spika wa bunge hilo.
Somalia imeshuhudia malumbano makali baina ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo Hassan Ali Khaire pamoja na kundi la wabunge wanaomuunga mkono kwa upande mmoja, na Spika wa Bunge la nchi hiyo ya Pembe ya Afrika kwa upande mwingine.
Image Caption
Mgogoro huo ulianza mapema mwezi jana, baada ya wabunge zaidi ya 100 wanaoegemea upande wa Waziri Mkuu, kuwasilisha hoja bungeni ya kutaka kuenguliwa madarakani Spika wa bunge, kwa madai kuwa amekuwa kizingiti kwenye shughuli za bunge hilo. 
Mohamed Osman Jawari, Spika wa Bunge la Somalia anatuhumiwa na wabunge kuwa anatumia vibaya madaraka yake na kuzuia kufanyiwa marekebisho katiba ya nchi hiyo. 

No comments:

Post a Comment