Friday, April 13, 2018

DRC YASUSIA MKUTANO WA UMOJA WA MATAIFA WA KUKUSANYA FEDHA ZA KUWASAIDIA RAIA WA NCHI HIYO

 DRC yasusia mkutano wa Umoja wa Mataifa wa kukusanya fedha za kuwasaidia raia wa nchi hiyo
Mkutano maalumu uliotishwa na Umoja wa Mataifa umeanza leo mjini Geneva Uswisi kwa kuchangisha fedha za kukabiliana na janga la kibinaadamu katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo huku serikali ya Kinshasa ikiususia mkutano huo.
Mashirika ya misaada yanasema kuwa, zaidi ya watu milioni 5 wamelazimika kuyakimbia makazi yao katika Jamhuri ya Kidemokrasia yya Congo kwa sababu ya mapigano katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo.
Aidha mkutano huo  wa wafadhili umeanza leo huku takwimu za Umoja wa Mataifa zikionesha kwamba, watu milioni 13 wanahitaji msaada huku thuluthi moja kati yao wakiwa  ni wakimbizi wa ndani  ambao wanahitaji msaada wa dharura wa kibinadamu mwaka huu.
Wafadhili hao wa kimataifa wanatafuta  kiasi cha dola bilioni 1.7 kuwasaidia watu hao wanaohitaji dawa, chakula na makazi mazuri.
Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Hata hivyo, serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imesusia mkutano huo, ikiyashutumu mashirika ya kiraia kwa kutoa takwimu za uongo na kulichafulia jina taifa hilo.
Uamuzi huo wa serikali ya Kinshasa wa kususia mkutano huo umekosolewa, huku baadhi ya wakosoaji wakisema kwamba, serikali yya Kinshasa ingeshiriki tu katika mkutano huo ili kuwashajiisha wafadhili watoe misaada kwani wanaoumia ni raia.
Hayo yanajiri katika hali ya ambayo, hivi karibuni Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa  lilionya kuwa, hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imeendelea kuwa mbaya na imefikia hatua ya kuwa janga kwenye baadhi ya maeneo ya nchi hiyo, huku mamilioni ya watu wakikabiliwa na njaa.

No comments:

Post a Comment