Tuesday, April 17, 2018

MAHAKIMU ZAIDI YA 250 WAFUTWA KAZI JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA CONGO

Mahakimu zaidi ya 250 wafutwa kazi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imewafuta kazi zaidi ya mahakimu 250 kwa sababu mbalimbali ikiwemo ya ufisadi.
Waziri wa Sheria Alexis Thambwe Mwamba amesema kuwa, mahakimu hao wamefutwa kazi kwa sababu za ufisadi na wengine kutokuwa na elimu ya taaluma hiyo.
Waziri thambwe amebainisha kuwa, hatua hii imechukuliwa ili kuwazuia watu waliokuwa wakiingia katika idara ya mahakama wakiwa na lengo la kujipatia fedha badala ya kuwatumikia raia wa nchi hiyo.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, idadi kamili ya mahakimu waliofutwa kazi na serikali ni 256 na kwamba, sababu kuu ni majaji hao kujihusisha na vitendo vya kupokea rushwa, kutokuwa na elimu ya taaluma hiyo na kundi la tatu limestaafishwa.
Alexis Thambwe Mwamba, Waziri wa Sheria wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Hii sio mara ya kwanza kwa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Kinshasa kuwachukulia hatua maafisa wa juu wa idara ya Mahakama. Mwaka 2009, Rais Joseph Kabila aliwafuta kazi majaji 96 baada ya kubainika kuwa walikuwa wakijihusha na vitendo vya ufisadi.
Hatua hiyo ya kufutwa kazi majaji hao inakuja kukiwa kumesalia miezi 7 kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu katika nchi hiyo inayokabiliwa na changamoto kubwa ya usalama. 
Uchaguzi huo uliokuwa ufanyike mwishoni mwa mwaka jana ulisogezwa mbele na sasa unatarajiwa kufanyika Desemba 23, mwaka huu ili kumpata mrithi wa Rais Joseph Kabila, ambaye muhula wake wa uongozi ulimalizika Desemba 20, 2016.

No comments:

Post a Comment