Sunday, March 26, 2017

WANAJESHI KADHAA WA MISRI WAUAWA KATIKA MRIPUKO WA BOMU SINAI

Wanajeshi wanne wa Misri wameuawa baada ya gari lao kulengwa kwa bomu katika Peninsula ya Sinai.
Duru za kijeshi zimearifu kuwa, mlipuko huo ulitokea yapata kilomita 20, kusini mwa mji wa al-Arish, kaskazini mwa eneo la Sinai.
Habari zaidi zinasema kuwa, watu kadhaa wamejeruhiwa katika shambulizi hilo la bomu, linaloaminika kufanywa na magenge ya kigaidi yanayofungamana na kundi la kitakfiri la Daesh.
Vikosi vya Misri eneo la Sinai
Shambulizi hilo la jana limefanyika siku mbili baada ya hujuma nyingine kama hiyo ya bomu kuua askari 10 wa jeshi la Misri katikati mwa Peninsula ya Sinai. Hata hivyo, vyombo vya usalama vya nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika vilifanikiwa kuangamiza magaidi 15 katika operesheni hiyo, mbali ya kuwatia mbaroni wengine 7. 
Eneo la Sinai Kaskazini limekuwa likishuhudia mashambulizi ya mara kwa mara ya kundi la Ansar Baytul Muqaddas, tawi la genge la kigaidi la Daesh nchini Misri, hujuma zilizoshadidi baada ya kundi hilo kutangaza utiifu kwa kundi la kigaidi la Daesh mwaka 2014.

No comments:

Post a Comment