Friday, March 10, 2017

RIPOTI: WATOTO KARIBU MILIONI 2 WANAKUFA KILA MWAKA KWA KUVUTA HEWA CHAFU

Kwa akali watoto milioni 1.7 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na kuvuta hewa chafu kote duniani.
Ripoti mpya ya Shirika la Afya Duniani (WHO) imefafanua kuwa, kiwango hicho ni sawa na asilimia 25 ya vifo vya watoto wadogo walio na umri wa chini ya miaka mitano kote duniani.
WHO imebainisha kuwa, mazingira machafu, hewa na maji machafu pamoja na moshi wa sigara yanasababisha robo ya vifo vya watoto wadogo kote duniani kila mwaka.
Watoto wadogo, wahanga wakuu wa hewa chafu
Margaret Chan, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani amesema kuwa, hewa na maji machafu yamechangia watoto wengi kupatwa na maradhi ya pumu, malaria, kutapika na kuendesha, magonjwa ambayo yanaongoza kwa vifo vya watoto wadogo duniani.
Mwaka jana 2016, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilionya kuwa hali ya uchafuzi wa hewa inazidi kuwa mbaya duniani kote huku zaidi ya asilimia 80 ya wakaazi wa miji mikubwa wakivuta hewa chafu na kuongeza hatari ya kupatwa na saratani ya mapafu na maradhi mengine hatari.

No comments:

Post a Comment