Friday, March 30, 2018

WAPALESTINA 8 WAUAWA SHAHIDI NA JESHI LA ISRAEL KATIKA MAANDAMANO YA SIKU YA ARDHI

Wapalestina 8 wauawa shahidi na jeshi la Israel katika maandamano ya Siku ya Ardhi
Kwa akali Wapalestina wanane wameuawa shahidi na wanajeshi katili wa Israel katika maandamano ya Siku ya Ardhi, ya kulaani hatua ya utawala huo ghasibu ya kupora ardhi zao, yaliyofanyika leo karibu na uzio wa kibaguzi wa Israel katika Ukanda wa Gaza.
Wizara ya Afya ya Palestina imesema mbali na Wapalestina wanane kuuawa shahidi kwa kumiminiwa risasi na wanajeshi katili wa Israel, wengine zaidi ya 550 wamejeruhiwa vibaya.
Kituo cha Kutetea Haki za Wapalestina cha Adalah kimelaani vikali mauaji hayo, na kueleza kusikitishwa kwake na kitendo cha jeshi la Israel kutumia risasi hai, vifaru na maroketi dhidi ya waandamanaji ambao hawana ulinzi. 
Kituo hicho kimesema mauaji hayo dhidi ya Wapalestina waliokuwa wakiandamana kutetea ardhi zao zilizoporwa ni kinyume cha sheria za kimataifa.
Siku ya Ardhi huadhimishwa Machi 30 kila mwaka
Maelfu ya Wapalestina wamejitokeza kushiriki maandamano hayo, licha ya idadi kubwa ya wanajeshi wa Israel waliojizatiti kwa silaha nzito kuuzingira uzio huo wa Gaza, na licha ya utawala huo haramu kutumia fatua za Saudi Arabia kuwashawishi Wapalestina hao kutoshiriki maandamano hayo.
Itakumbukwa kuwa, siku kama ya leo miaka 42 iliyopita, maandamano ya kwanza ya "Yaumul Ardh" au Siku ya Ardhi yalifanyika huko katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, kulaani hatua ya utawala wa Kizayuni ya kupora ardhi za raia wa Kiarabu wa Palestina.
Waarabu sita wa Israel ambao hawakuwa wamejizatiti kwa silaha waliuawa na askari wa Kizayuni katika maandamano hayo yaliyofanyika Machi 30 mwaka 1976.

No comments:

Post a Comment