Friday, March 30, 2018

AL SISI ATANGAZWA MSHINDI WA KITI CHA URAIS WA MISRI

Al Sisi atangazwa mshindi wa kiti cha Rais wa Misri
Rais Abdul Fattah al-Sisi wa Misri ametangazwa mshindi wa uchaguzi tata wa rais uliofanyika Jumatatu iliyopita, kwa kuzoa asilimia 92 ya kura zote zilizopigwa.
Uchaguzi wa Rais wa Misri uliofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 26 Machi, ulimalizika juzi tarehe 28. Katika uchaguzi huo al Sisi alichuana na Moussa Mostafa Moussa wa chama cha al Ghad ambaye ametajwa na vyombo vya habari kuwa hakuwa mpinzani wa al Sisi bali alichomekwa kwenye kinyang'anyiro hicho kuhalalisha zoezi hilo.
Mambo mawili yametajwa kuwa sababu kuu za ushindi wa Abdul Fattah al Sisi hata kabla ya uchaguzi huo kufanyika.
Kwanza ni kukandamizwa kambi kuu ya upinzani katika kipindi chote cha uongozi wa miaka minne iliyopita ya utawala wa al Sisi. Kijadi, mpinzani mkuu wa kiongozi wa sasa wa Misri alipaswa kuwa mgombea yeyote wa harakati ya Ikhwanul Muslimin. Katika kipindi chote cha miongo kadhaa iliyopita watawala wa Misri wamefanya kila wawezalo kuhakikisha kwamba, harakati hiyo inakandamizwa, viongozi wake wanaoswekwa jela na wafuasi wao wanahukumiwa vifungo au hata adhabu ya kifo. Baada ya kuondolewa madarakani dikteta wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak katika mapinduzi ya wananchi ya mwaka 2011, harakati hiyo ilipata anga ya pumua kidogo na mgombea wake akashinda uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia uliofanyika nchini humo. Hata hivyo serikali ya Muhammad Mursi haikuishi zaidi ya mwaka mmoja. Serikali hiyo ya kwanza kuchaguliwa na wananchi kwa njia za kidemokrasia, iliondolewa madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Jenerali Abdul Fattah al Sisi. 
Sami Hafez Anan
Sababu kuu ya pili ya ushindi wa al Sisi ni kubinywa na hata kukamatwa wapinzani mashuhuri wa kiongozi huyo kabla kidogo ya zoezi la uchabuzi wa rais. Serikali ya Cairo iliwazuia wagombea mashuhuri kama Ahmad Shafiq, Sami Hafez Anan, Abdel Munim Abul Futuh kujitosa katika kinyang'anyiro hicho kwa kutumia visingizio mbalimbali. Hata Moussa Mustafa Moussa aliyechuana na al Sisi katika uchaguzi huo anajulikana kuwa muungaji mkono wa Abdul Fattah al Sisi.
Uchaguzi wa rais uliofanyika Misri ulifanyika kwa kuwa hakukuwa na budi kufanyika, na al Sisi alilazimika kuitisha zoezi hilo. Mchambuzi wa masuala ya siasa Hassan Shukri anasema: Uchaguzi wa rais uliofanyika Misri haukuwa ushindani baina ya wagombea wawili bali lilikuwa zoezi la kuhalalisha utawala wa al Sisi. Hata hivyo siasa za ngumi ya chuma zinazotekelezwa na al Sisi akisaidiwa na jeshi tangu miaka minne iliyopita, kutotimizwa ahadi zilizotolewa na kiongozi huyo kwa wananchi na kupuuzwa au kukanyagwa demokrasia na uhuru vimeshusha chini zaidi imani ya Wamisri kwa kiongozi huyo." 
Jenerali Abdul Fattah al Sisi
Ni kwa kutilia maanani sababu hizo mbili ndiyo maana Abdul Fattah al Sisi akaingia kwenye klabu ya viongozi wa nchi za Kiarabu wanaoshinda chaguzi za rais kwa kupata eti asimia zaidi ya 90 ya kura zilizopigwa! Pamoja na hayo wanaharakati wa masuala ya kisiasa na kijamii wanatarajia kuwa, jenerali huyo mstaafu hatafanya marekebisho ya katiba yanatakayomruhusu kubakia madarakani baada ya kumalizika muhula wake wa vipindi viwili kama wafanyavyo baadhi ya viongozi wa nchi za Kiafrika na Kiarabu.

No comments:

Post a Comment